Banner

Banner

FOLLOW US FACEBOOK

propertyfinder.co.tz

Thursday, May 16, 2013

HUU NDIO UFAFANUZI WA DAWA BANDIA ZA "ARV"

 
TAREHE 9 Mei 2013, Mhe. Dkt. Hussein A. Mwinyi (Mb) Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, katika kuhitimisha hoja ya bajeti ya Wizara alitolea ufafanuzi suala la dawa bandia ya ARV kufuatia hoja zilizokuwa zimetolewa na Mhe. Zarina S. Madabida (Mb) kuhusu kuhusika kwa kiwanda cha dawa chaTanzania Pharmaceutical Industries Ltd (TPI) katika sakata la dawa bandia za ARV.


Baada ya ufafanuzi huo wa Mhe. Waziri kutolewa, kumekuwa na taarifa mbalimbali kupitia vyombo vya habari zinazoleta mkanganyiko kwa wananchi kuhusu suala hili.

Ili kuondoa mkanganyiko ambao umeanza kujitokeza, Wizara inapenda kutoa ufafanuzi kuhusu tamko lililotolewa na Mhe. Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii.  
Aidha, kama ilivyoelezwa katika taarifa mbalimbali za umma zilizokwisha kutolewa na Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii pamoja na  TFDA  kuhusiana na suala hili, bado inasisitizwa kwamba kampuni ya TPI Ltd iliiuzia Bohari  ya Dawa (MSD) dawa bandia aina ya TT-VIR 30 toleo Na. 0C.01.85, kwa mujibu wa nyaraka zilizopo.
Tunapenda kusisitiza kwamba, Mhe. Waziri katika hotuba yake hakukanusha kuwa kampuni ya TPI Ltd iliiuzia MSD dawa bandia bali alieleza kwamba uchunguzi wa awali katika kiwanda cha kampuni hiyo haukuonesha dawa hiyo ilizalishwa na TPI Ltd  bali vifungashio ni vya TPI Ltd na nyaraka zinaonesha TPI Ltd kuiuzia MSD dawa hizo bandia. 
Aidha, alieleza kuwa vyombo vya usalama bado vinaendelea kulichunguza suala hilo ili kubaini chanzo na wahusika wakuu wa dawa hizo bandia.
Kwa kuzingatia unyeti wa suala hili, Wizara inatoa wito kwa vyombo vya habari kusubiri hatma ya uchunguzi unaofanywa na vyombo vya usalama na kuepuka kutoa taarifa ambazo zinaweza kupotosha umma na jitihada kubwa za Serikali katika kupambana na dawa bandia nchini.
Imetolewa na:
N. Mwamwaja
MSEMAJI
16 Mei 2013

No comments:

Post a Comment