Banner

Banner

FOLLOW US FACEBOOK

propertyfinder.co.tz

Thursday, September 6, 2012

BARAZA LA USALAMA LA UN KUAMUA HATMA YA KUMBUKUMBU ZA ICTR...!

John Hocking, Msajili wa Taasisi ya Kimataifa itakayorithi kazi za Mahakama za Kimataifa (MICT), Jumanne aliliambia Shirika la Habari la Hirondelle kwamba hatma ya mahali pa kuhifadhi kumbukumbu za Mahakama ya Kimataifa ya Mauaji ya Kimbari ya Rwanda (ICTR) iko mikononi mwa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa.
Rwanda imekuwa ikidai haki ya kuhifadhi kumbukumbu za ICTR baada ya kuhitimisha kazi zake kwa maelezo kwamba yenyewe ndiyo yenye haki ya kiasili ya kupokea kumbukumbu hizo kutokana na ukweli kwamba mauaji ya kimbari yalifanyikia nchini Rwanda.
Wakati wa uzinduzi rasmi wa MICT, tawi la Arusha, Julai 2, 2012, Mwendesha Mashitaka Mkuu wa Rwanda, Martin Ngoga alisema wanahitaji majadiliano ya wazi katika masuala mbalimbali likiwemo hilo la uhifadhi wa kumbukumbu.
Lakini wakati wa mahojiano maalum na Shirika la Habari la Hirondelle,Msajiliwa MICT, John Hocking alisema ‘’Azimio la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa namba 1966 litafanyiwa tathmini baada ya miaka minne ijayo na siwezi kujua nini kitatokea baada ya miaka minne. Ni wazi kwamba sina mwelekeo kamili juu ya hili lakini kwa hivi sasa ninachokifanyia kazi ni azimio la Baraza la Usalama, ambalo limeelekeza kwamba, kumbukumbu hizo zihifadhiwe mahali zilizopo mahakama hizo za Umoja wa Mataifa.’’
Kwa mujibu wa azimio hilo la Baraza la Usalama lililoidhinishwa mwishoni mwa mwaka 2010, kuanzishwa kwa MICT ni kwa ajili ya kurithi kazi zitakazoachwa na ICTR, yenye makao yake makuu, Arusha, Tanzania na mahakama nyingine ya Umoja wa Mataifa ya Uhalifu wa Kivita Katika Yugoslavia ya zamani (ICTY) iliyopo The Hague, Uholanzi.
‘’Katika azimio hilo, Baraza la Usalama lilieleza kwamba, kumbukumbu za ICTR zihifadhiwe Arusha na zile za ICTY zihifadhiwe The Hague,’’ alisisitiza Hocking.
Msajili huyo aliendelea kufafanua kwamba tawi la MICT la Arusha lilipoanza kazi Julai 1, mwaka huu shughuli mbalimbali za ICTR zilihamishiwa kwa taasisi hiyo mpya ikiwa ni pamoja na kumbukumbu za baadhi ya kesi zilizokwishahitimishwa na ulinzi wa watu waliotoa ushahidi katika kesi hizo.
Shughuli nyingine zilizohamishiwa kwenye taasisi hiyo mpya ni pamoja na kusaidia juhudi za mataifa yanayofanya uchunguzi dhidi ya watuhumiwa wa mauaji hayo nchini mwao na kuendelea kuwasaka watuhumiwa tisa ambao bado hawajatiwa mbaroni.
Kwa mujibu wa Hocking pia jukumu la kusimamia adhabu walizopewa wafungwa  waliopo katika nchi za Mali na Benin pia lilihamishiwa kwenye taasisi hiyo kuanzia tarehe hiyo.
Alipoulizwa juu ya usalama wa wafungwa wanaotumikia adhabu zao nchini Mali kutokana na tishio la hali ya usalama nchini humo, Hocking alijibu kuwa Idara ya Ulinzi na Usalama ya Umoja wa Mataifa na Mratibu Mkazi wa Umoja wa Mataifa nchini Mali wamemhakikishia kwamba wafungwa wote wako salama.
Hivi sasa wako wafungwa 19 wanaotumikia adhabu zao nchini Mali.

No comments:

Post a Comment