Banner

Banner

FOLLOW US FACEBOOK

propertyfinder.co.tz

Thursday, September 27, 2012

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete amemwambia Mwenyekiti wa Taasisi ya Mapinduzi ya Kijani katika Afrika (AGRA), Mheshimiwa Kofi Annan kuwa Afrika haiwezi kuzungumza ama kupata maendeleo ya maana bila kumshirikisha mkulima mdogo.
Aidha, Rais Kikwete amemwambia Mheshimiwa Annan, Katibu Mkuu wa zamani wa Umoja wa Mataifa (UN) kuwa bila mkulima mdogo wa Afrika kusaidiwa hawezi kutoka kwenye umasikini kwa sababu anakabiliwa na changamoto nyingi ambazo peke yake hawezi kupambana nazo.
“Huwezi kuzungumzia maendeleo ya aina yoyote katika Afrika bila kumshirikisha mkulima mdogo. Huwezi kufanikiwa kwa kumtenga mkulima mdogo. Kwa bahati mbaya sana, mkulima mdogo katika Afrika amebakia anatumia zana zile zile za jadi, jembe la mkono, pekee yake hawezi kupiga hatua bila kusaidiwa kwa sababu anakabiliwa na changamoto nyingi mno,” amesema Rais Kikwete.
Rais Kikwete ameyasema hayo usiku wa jana, Jumatano, Septemba 26, 2012, kwenye Hoteli ya Ngurdoto, Arusha wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na Mheshimiwa Annan.
Viongozi hao wamefikia kwenye Hoteli ya Ngurdoto ambako wamewasili jana kuhudhuria Mkutano wa Pili wa AGRA ambao umeanza jana kwenye hoteli hiyo. Rais Kikwete amewasili jioni ya jana tayari kuufungua rasmi mkutano huo.
Huu ni mkutano wa pili wa AGRA baada ya wa kwanza uliofanyika Ghana miaka miwili iliyopita. Agenda kuu ya AGRA ni kujaribu kuleta mageuzi ya kilimo katika Afrika.
Katika mkutano kati ya viongozi hao, Rais Kikwete amemwambia Mheshimiwa Annan kwamba kwa sababu kilimo kinaajiri watu wengi nchini na kwa sababu kinakua kwa kasi ndogo sana, kwa asilimia nne tu, bado kinamvuta chini kila mmoja nchini.
“Uchumi wetu unakua kwa kasi ya kuridhisha sana na hasa katika sekta za mawasiliano, miundombinu, madini na utalii, lakini bado mafanikio hayo hayajaanza kuonekana kwa wazi kwa wananchi kwa sababu kilimo ambacho kinaajiri Watanzania wengi zaidi kinakua kwa kasi ndogo. Kasi hii inamvuta kila mmoja kurudi chini.”
Mheshimiwa Annan amemsifu Rais Kikwete kwa uongozi shupavu katika eneo la kilimo kutokana na program mbali mbali ambazo Serikali imezianzisha. “Nakupongeza sana Mheshimiwa Rais kwa uongozi. Umekuwa mfano wa kuigwa katika Bara letu kwa uongozi wako katika eneo hili la kilimo”.

Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu.
Dar es Salaam.
27 Septemba, 2012

No comments:

Post a Comment