Banner

Banner

FOLLOW US FACEBOOK

propertyfinder.co.tz

Tuesday, June 9, 2026

Mkuu Wa Wilaya ya Lindi, Mhe. Victoria Mwanziva Amechaguliwa Kuiwakilisha Tanzania Katika Programu Mahususi ya Uongozi Kwa Wanawake


Mkuu wa Wilaya ya Lindi, Mhe. Victoria Mwanziva amechaguliwa kuiwakilisha Tanzania katika programu mahususi ya Uongozi kwa Wanawake inayoongozwa na Rais Mstaafu wa Liberia, Ellen Johnson Sirleaf.

Programu hiyo inajulikana kama “Amujee Leadership Initiative” ikiwa chini ya Ellen Johnson Sirleaf Presidential Centre for Women and Development- EJS Centre inaungana na Wanawake Viongozi wengine waliopata fursa na heshima ya kushiriki.

Viongozi wengine ni Waziri wa Afya na Maendeleo ya Jamii Namibia, Dkt. Esperance Luvindao, Waziri wa Mazingira wa Guinea, Djami Diallo, Wabunge mbalimbali akiwemo Anta Diack wa Senegal na Dkt. Anneline Chetty ambaye ni Mtendaji Mkuu wa Kituo cha Biashara, Viwanda na Uwekezaji Afrika Kusini.

Kwa mujibu wa taarifa, Victoria ni miongoni mwa Wanawake 15 walioteuliwa barani Afrika baada ya mchujo mkali uliovutia zaidi ya waombaji 600. Uteuzi wake umetokana na mchango wake katika Uongozi wa Jamii, hususan kazi za maendeleo Vijijini na uwezeshaji wa Vijana kupitia nafasi yake ya Uongozi wa Wilaya.

Programu hii inalenga kukuza ushirikiano wa Viongozi Wanawake barani Afrika na kuimarisha ajenda za maendeleo jumuishi, huku ikitarajiwa kuongeza fursa za ushirikiano kati ya Mataifa ya Afrika.

Dkt. Samia: Tanzania Haifungamani na Upande Wowote, Inasaka Fursa za Kiuchumi Kila Pembe ya Dunia.

 

Na Beda Msimbe, TBN, aliyekuwa Petersburg, Urusi

Ulimwengu wa sasa wa diplomasia ya kijiografia unatawaliwa na ushindani mkubwa wa nguvu za kisiasa na kiuchumi kati ya mataifa makubwa ya Magharibi na yale ya Mashariki. 

Katika mazingira haya, mataifa yanayoendelea mara nyingi hujikuta yakitazamwa kwa darubini ya shaka pale yanapochukua hatua za kimkakati kupanua wigo wa washirika wao wa kimaendeleo. 

Ziara ya hivi karibuni ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan nchini Urusi, imezua minong'ono na hisia mbalimbali miongoni mwa wachambuzi wa mambo, wengi wao wakihofia kuwa huenda Tanzania sasa inabadili mwelekeo wake wa sera ya mambo ya nje kwa kuitupa mkono Magharibi na kugeukia upande wa Mashariki. 

Hofu hii haina msingi wowote, kwani majibu thabiti na ya kizalendo aliyoyatoa Rais Samia mbele ya waandishi wa habari pembezoni mwa Jukwaa la Kimataifa ya Uchumi la St. Petersburg (SPIEF) nchini Urusi, yanadhihirisha ukomavu wa diplomasia ya Tanzania inayojali maslahi ya taifa kwanza kabisa.

Katika mazungumzo hayo maalum yaliyowashirikisha waandishi wa habari 13 walioambatana naye, akiwemo mwakilishi kutoka Mtandao wa Bloggers Tanzania (TBN), Rais Samia alikuwa wazi na alinyoosha maelezo bila kusita. 

Alifafanua kuwa Tanzania haihamishi nguvu zake kutoka upande mmoja kwenda mwingine, bali inaongeza wigo wa washirika ili kuhakikisha malengo ya maendeleo ya kiuchumi yanatimizwa kwa faida ya wananchi wake. 

Hii ina maana kwamba wale wote wenye hofu au mashaka kuhusu ushirikiano wa karibu kati ya Tanzania na Urusi wanapaswa kuondoa shaka hiyo mara moja, kwani serikali haifuati mtu au upande wowote wa kiitikadi, bali inafuata yeyote mwenye nia njema ya kushirikiana katika kuinua maisha ya Watanzania.

Msimamo huu wa Rais Samia si jambo geni wala la kubahatisha, bali ni muendelezo wa misingi imara ya kihistoria iliyowekwa na Muasisi wa Taifa letu, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere. 

Miaka 57 iliyopita, Mwalimu Nyerere alipotembelea Urusi (wakati huo ikiwa Muungano wa Sovieti), alitamka maneno yaleyale yanayosikika leo kutoka kwa Rais Samia: kwamba Tanzania ni nchi isiyofungamana na upande wowote. Mwalimu alisisitiza kuwa Tanzania itajichanganya na marafiki zake kwa jinsi marafiki hao wanavyotaka kuwa na Tanzania, mradi tu hawataingilia uhuru na mamlaka ya nchi. Falsafa hiyo ya kihistoria ndiyo inayomwongoza Rais Samia hadi leo katika ulimwengu huu unaozidi kuwa na vitovu vingi vya nguvu ya kiuchumi na kiteknolojia.

Sera ya Tanzania ya kutofungamana na upande wowote (Non-Aligned Policy) imekuwa silaha kuu ya kulinda uhuru wa Tanzania wa kufanya maamuzi ya kimkakati. Katika kile kinachoitwa Diplomasia ya Maslahi ya Kitaifa (National-Interest Diplomacy), kigezo kikuu cha kupima ubora wa uhusiano wa kimataifa si itikadi za kisiasa, bali ni mchango gani uhusiano huo unaingiza katika uchumi wa nchi, ajira kwa vijana, na uhamishaji wa teknolojia. 

Rais Samia alifafanua kuwa ziara yake nchini Urusi ilikuja na maombi saba ya kimkakati kutoka Tanzania, na wenyeji wao wa Urusi wakavutiwa kiasi cha kuongeza maombi mengine mawili na kufanya jumla ya maeneo tisa ya ushirikiano. Hii inadhihirisha kuwa pande zote mbili zinazungumza lugha moja inayolenga ustawi wa kiuchumi na maendeleo ya jamii.

Ili kuelewa kwa nini Tanzania inapaswa kuendelea kushirikiana na Urusi pamoja na ulimwengu mzima, ni lazima kuangalia uwiano wa washirika wetu duniani kote. 

Serikali ya Awamu ya Sita haijafunga milango kwa mataifa ya Magharibi; badala yake washirika wetu wa kitamaduni wanaendelea kuwa nguzo muhimu. Kwa mfano, Marekani bado ni mshirika mkubwa sana wa kiuchumi na kibiashara nchini Tanzania, ikiongoza katika kuleta watalii wengi na kuwekeza kupitia kampuni kubwa zaidi ya 500 zilizopo nchini, hususan katika sekta ya madini na uwekezaji mbalimbali wa kimkakati. Vivyo hivyo, mataifa ya Ulaya yameendelea kuwa washirika  wakuu katika biashara na utoaji wa misaada pamoja na uwezeshaji wa kifedha. Uhusiano huu wa karibu na Magharibi haujatikisika, na unazidi kuimarika kila uchao.

Wakati huo huo, Tanzania imeendelea kunufaika na uhusiano mkubwa na mataifa ya Asia. China imekuwa mshirika  mkuu wa kihistoria na wa sasa katika kuwezesha miradi mikubwa ya miundombinu ya usafirishaji na uchukuzi, huku India nayo ikiwa miongoni mwa washirika wakubwa wa kibiashara .

Japan haikuachwa nyuma, kwani imeendelea kuwekeza kwa nguvu katika sekta za nishati, elimu, na ujenzi wa miundombinu ya kijamii. Hata mataifa mengine kama Australia, Uingereza, na Ufaransa yamekuwa yakija nchini kwa kasi kupitia mipango mbalimbali kama vile mpango wa Matei wa Ufaransa ili kuwezesha maendeleo ya kiuchumi. 

Kwa mtazamo huu, Urusi inaingia kama mshirika mwingine muhimu wa kimkakati baada ya Tanzania kumaliza changamoto zilizotokana na masharti magumu ya mabadiliko ya kiuchumi ya Benki ya Dunia katika miaka ya 1980, ambayo wakati huo yalilazimu Tanzania kuangalia upande mmoja tu wa mlango.

Ni dhahiri kuwa Diplomasia ya sasa ya Tanzania inatawaliwa na ukomavu na uhuru wa kuchagua. Kama alivyowahi kunukuu Waziri wa Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo, kuhusu methali maarufu ya kiuchumi: "Tanzania haihitaji kujua rangi ya paka, mradi tu paka huyo ana uwezo wa kukamata panya." 

Maneno haya yana maana kwamba Tanzania haichagui wala haibagui mshirika kwa kuangalia sura au mfumo wake wa kisiasa, bali inaangalia uwezo na utayari wa mshirika huyo kushirikiana nayo katika kutatua changamoto za umaskini na kukuza uchumi. Kila taifa linaloheshimu mamlaka ya Tanzania na liko tayari kuchangia katika ustawi linakaribishwa kwa mikono miwili.

Mkakati huu wa kutafuta washirika wengi kwa wakati mmoja una umuhimu mkubwa sana katika kulinda usalama wa kiuchumi wa Tanzania. Hakika kuweka mayai yote kwenye kikapu kimoja ni hatari kubwa katika ulimwengu wa sasa uliopasuka kutokana na vikwazo vya kiuchumi na migogoro ya kikanda. Kuwa na washirika mbalimbali kunatoa nguvu kubwa ya majadiliano (bargaining power) kwenye meza za kimataifa, kwani hatutegemei chanzo kimoja tu cha mitaji au teknolojia. Kama soko moja likiyumba au kukiwa na mabadiliko ya kisiasa upande mmoja, Tanzania inaweza kuendelea kusonga mbele kwa kutumia milango mingine iliyo wazi.

Kwa kuwa, dira yetu ya maendeleo ya taifa ya 2050 ndiyo dira kuu inayoongoza Tanzania hivi sasa ni vyema kama taifa kutumia diplomasia ya kiuchumi kutekeleza Dira ya Maendeleo ya Taifa ya Mwaka 2050, lengo likiwa ni kukuza uchumi kwa kiwango kikubwa na kufikia thamani ya uchumi wa dola bilioni 1,000 (trilioni moja) ifikapo mwishoni mwa utekelezaji wake. 

Ili kufikia lengo hili kubwa la kihistoria, serikali inahitaji mitaji mikubwa, miundombinu ya kisasa, na teknolojia ya hali ya juu kutoka kila kona ya dunia. Tanzania haiwezi kufikia malengo hayo makubwa kwa kujifungia milango au kwa kuchagua upande mmoja wa kidunia. Ndiyo maana Rais Samia anapiga hatua kwa ujasiri, akifungua milango kila mahali—iwe ni Washington, Beijing, Brussels, au Moscow—kuhakikisha kuwa maslahi ya taifa yanalindwa na fursa za kiuchumi zinawafikia wananchi wote.

mwisho.

Monday, June 8, 2026

Makubaliano Nane ya Kimkakati: Ramani Mpya ya Ushirikiano wa Kiuchumi Kati ya Tanzania na Urusi Yafunuliwa

 


Na Mwandishi Wetu, TBN, Dar es salaam

Mikataba na hati za makubaliano manane (8) zilizosainiwa kati ya Tanzania na Urusi, ndizo zilizoweka msingi mkuu wa ushirikiano mpya wa kiuchumi, kijamii na kiteknolojia unaotarajiwa kupandisha hadhi ya nchi hizi mbili. 

Makubaliano haya makubwa, ambayo ni matunda ya moja kwa moja ya ziara ya kihistoria ya Rais Samia Suluhu Hassan nchini Urusi, yanajenga daraja imara la maendeleo katika sekta tisa za kipaumbele: kilimo, elimu, nishati, madini, viwanda, utalii, usafirishaji, uchumi wa kidijiti, pamoja na biashara na uwekezaji.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo, ameanika hadharani undani wa makubaliano hayo manane yanayobeba mustakabali wa nchi:

Kutoka Diplomasia ya Lugha Hadi Mapinduzi ya Afya na Elimu ya Juu

Katika makubaliano ya kwanza, Tanzania na Urusi zimeamua kutumia lugha kama silaha ya kidiplomasia. Kupitia hati ya ushirikiano kati ya Baraza la Kiswahili la Taifa (BAKITA) na Chuo Kikuu cha Mahusiano ya Kimataifa cha Urusi (MGIMO), lugha ya Kiswahili itazidishwa kasi ya kufundishwa nchini Urusi, huku Tanzania nayo ikijipanga kuanza kufundisha Kirusi kupitia Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM).

Makubaliano ya pili yamejikita kwenye sekta ya afya, ambapo Chuo Kikuu cha Muhimbili (MUHAS) kimeingia ubia na taasisi mbili za afya za Urusi kwa ajili ya kubadilishana utaalamu wa matibabu na kuongeza nguvu katika uzalishaji wa dawa nchini.

Kwenye upande wa elimu, makubaliano ya tatu na ya nne yanakuja kutatua changamoto za ajira na teknolojia ya kisasa:

Wizara za Elimu za nchi zote mbili zimesaini makubaliano ya kutambua vyeti na tuzo za kitaaluma zinazotolewa Urusi, hatua itakayowawezesha Watanzania waliosoma nchini humo kupata ajira kwa urahisi nyumbani.

Taasisi ya Teknolojia ya Dar es Salaam (DIT) imesaini mkataba na Chuo cha Urafiki  cha Urusi kuanzisha programu za pamoja za Shahada ya Kwanza na Uzamili katika fani za kisasa kabisa duniani—ikiwemo Sayansi ya Takwimu, Mfumo wa Anga, Akili Unde (AI), na Ujifunzaji wa Mashine (Machine Learning).

Kuvutia Mitaji ya Magharibi, Siri za Nishati na Ajira za Vijana

Makubaliano ya tano na ya sita yanalenga kufungua milango ya mitaji mikubwa. Kupitia Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalumu ya Kiuchumi Tanzania (TISEZA), nchi imepewa fursa ya kuhamasisha uwekezaji hadi kuelekea mataifa ya Ulaya. 

Zaidi ya hapo, Tanzania imeingia ushirikiano na Kampuni ya Roscongress ya Urusi—miamba ya kuandaa makongamano ya kimataifa—kwa lengo la kutengeneza miradi ya ubia na kuvutia wawekezaji sio tu kutoka Urusi, bali pia kutoka nchi za Magharibi.

Mkataba wa saba uligusa sekta nyeti ya nishati, ambapo Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) na Kampuni ya Mantra Tanzania Ltd (Kmapuni tanzu ya Shirika la Nyuklia la Urusi, Rosatom) zimesaini makubaliano ya kulinda na kutunza siri za taarifa za kimkakati katika miradi ya nishati.

Kama kilele cha makubaliano hayo, kubaliano la nane ni mpango kabambe wa miaka mitano unaolenga kukuza uchumi na kuzalisha fursa za ajira kwa vijana wa Kitanzania nchini Urusi.

"Haya ni matunda halisi ya kiuchumi yaliyotokana na maono ya mheshimiwa Rais," alisisitiza Profesa Kitila Mkumbo, akibainisha kuwa utekelezaji wa makubaliano haya unaenda kuweka alama ya kudumu katika soko la ajira na uwekezaji nchini.

Dakika Tatu za Dhahabu za Rais Samia Urusi Zafungua Milango ya Shilingi Trilioni 5

Na Mwandishi Wetu, TBN, Dar es salaam

Ziara ya kihistoria ya Rais Samia Suluhu Hassan nchini Urusi imeendelea kuzaa matunda makubwa baada ya Serikali kutangaza kuwa kampuni kubwa za nchi hiyo zimeonesha nia thabiti ya kuwekeza kiasi cha Dola za Marekani bilioni mbili (sawa na Shilingi za Kitanzania trilioni tano) ndani ya miaka mitatu ijayo. 

Uwekezaji huu mkubwa unalenga kimkakati sekta tano kuu za kipaumbele, huku ukichangiwa kwa kiasi kikubwa na ushawishi wa kipekee wa Rais Samia kiuchumi.

Akitolea ufafanuzi mafanikio hayo, Mkurugenzi wa Biashara ya Kimataifa na Diplomasia ya Uchumi kutoka Wizara ya Mambo ya Nje, Balozi John Ulanga, alifichua siri ya mafanikio hayo kuwa ni "dakika tatu za dhahabu" alizopewa Rais Samia kuzungumza katika Jukwaa la Uchumi la Kimataifa la Petersburg nchini Urusi. 

Kupitia ubunifu na maono yake makubwa, Rais alitumia muda huo mfupi kwa umahiri mkubwa kutangaza fursa za Tanzania, hatua iliyoziteka akili za miamba ya biashara nchini Urusi na kuamsha hamu kubwa ya kuwekeza nchini.

Miamba ya Nishati na Madini Kuja kwa Kasi

Katika sekta ya madini na nishati, Urusi tayari imeweka mguu wake nchini kupitia Shirika lake la Nishati ya Atomiki la Serikali (ROSATOM), ambalo limewekeza Dola bilioni 1.2 katika mradi wa kimkakati wa madini ya Urani, Nickel na madini mengine. Kasi hii inatarajiwa kuongezeka kufuatia ziara hiyo, kwani kampuni nyingi zaidi zilizotembelea banda la Tanzania zimeonesha nia ya kuja kuwekeza.

Sambamba na hilo, kampuni kubwa ya nishati duniani, Gazprom, inayomiliki soko kubwa la gesi asilia Ulaya Magharibi, imeingia kwenye mazungumzo na Tanzania ikieleza nia yake thabiti ya kushirikiana na kuwekeza katika sekta ya gesi nchini.

Mapinduzi ya Chanjo, Kilimo cha Kisasa na Tehama

Sekta ya afya na dawa nayo inatarajiwa kushuhudia mapinduzi makubwa. Kampuni za Urusi zilizotangulia kuwekeza nchini katika uzalishaji wa chanjo zimebainisha kuwa, ndani ya miaka mitano ijayo, zikishirikiana na makampuni mengine ya Urusi, zitakuwa na uwezo wa kuzalisha chanjo milioni 20 za magonjwa mbalimbali nchini Tanzania.

Kwenye kilimo na uongezaji thamani, makubaliano yamejikita katika kilimo endelevu kinachotunza mazingira na ununuzi wa bidhaa za Tanzania kama kahawa, korosho na chai kwa ajili ya soko la Urusi. Tayari wafanyabiashara zaidi ya 50 wa Kitanzania waliokuwa Urusi wameingia makubaliano ya kuleta mbolea, vinywaji vikali, na kuuza mazao yetu huko. Katika Tehama, taasisi za sayansi za Urusi ziko tayari kuja nchini kukuza uchumi wa kidijiti kwa kufundisha teknolojia hii kuanzia shuleni hadi vyuoni.

Angani Kufunguka: ATCL Kuanza Safari za Moja kwa Moja Moscow

Kama kilele cha mafanikio ya ziara hiyo, sekta ya utalii inatarajiwa kulipuka kwa mafanikio kufuatia tangazo la kihistoria kuwa Shirika la Ndege la Tanzania (ATCL) litaanza safari za moja kwa moja kati ya Dar es Salaam na Moscow ifikapo Julai 2, mwaka huu.

"Tuliona mtiririko mkubwa wa kampuni za waongoza utalii kutoka Urusi wakivutiwa na tangazo hili. Moja ya vitu vinavyovutia watalii ni upatikanaji wa usafiri wa uhakika, wa moja kwa moja na rahisi zaidi," alisisitiza Balozi Ulanga.

Hatua hii ya ATCL si tu kwamba inarahisisha usafiri, bali inafungua njia ya moja kwa moja kwa maelfu ya watalii na wawekezaji kutoka Urusi kumiminika nchini, ikithibitisha nguvu ya diplomasia ya uchumi inayotekelezwa na Serikali ya Awamu ya Sita.

Jinsi Ziara ya Rais Samia Nchini Urusi Ilivyoteka Fikira za Kidiplomasia Duniani



Na Mwandishi Wetu, TBN, Dar es salaam

Katika ulimwengu wa diplomasia ya kimataifa, kuna matukio yanayobadilisha mwelekeo wa upepo wa kiuchumi, na ziara ya Rais Samia Suluhu Hassan nchini Urusi imeandikwa kama mojawapo ya matukio hayo. 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mahmoud Thabit Kombo, amebainisha kuwa safari hiyo ya kihistoria kuanzia Juni 3 hadi 5, mwaka huu, imeleta "mtikisiko chanya" kote duniani, ikionyesha nafasi ya kipekee ya Tanzania kama lango kuu la bara la Afrika.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Balozi Kombo alifafanua kuwa mshtuko huu wa kidiplomasia unatokana na ukweli kwamba, hakuna nchi nyingine ya Afrika iliyowahi kufanya ziara ya kimkakati ya namna hiyo nchini Urusi katika muktadha wa sasa.

"Dunia nzima ina watu bilioni 7.5; Urusi anafanya biashara na watu bilioni 6. Ni bilioni 1.5 tu ndio waliomwekea vikwazo. Katika kutanua uchumi wake Afrika, Urusi inaiangalia Tanzania kama kiungo muhimu zaidi," alieleza Balozi Kombo.


Tanzania Kama Lango Kuu la Kimkakati Afrika

Kwanini dunia imetikisika? Jibu liko kwenye jiografia ya kiuchumi ya Tanzania. Balozi Kombo alieleza kuwa Urusi inaitazama Afrika kupitia kanda nne kuu, lakini Tanzania inasimama kama nchi ya pekee yenye uwezo wa kufungua milango ya soko la nchi zote saba za Afrika Mashariki (EAC) na nchi 16 za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC). Kupitia ushawishi wa Rais Samia, Tanzania imekuwa daraja linaloiunganisha Urusi na soko la Waafrika bilioni 1.2.


Ziara hii inabeba uzito mkubwa wa kihistoria, kwani ni ziara ya pili tu ya Mkuu wa Nchi wa Tanzania kutembelea Urusi tangu nchi hiyo ipate uhuru, ikitenganishwa na miaka 57 tangu Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, alipofanya ziara kama hiyo Oktoba 11, 1969.


Kutoka Dola Milioni 70 Hadi Milioni 500: Mapinduzi ya Biashara na Fursa za Vijana

Mkakati wa Rais Samia nchini Urusi haukuwa tu wa kisiasa, bali ulijikita katika kuleta mabadiliko ya mfukoni kwa Mtanzania. Serikali imeweka lengo kubwa la kukuza mauzo ya bidhaa za ndani kwenda Urusi kutoka Dola za Marekani milioni 70 za sasa hadi kufikia Dola milioni 500 (zaidi ya Shilingi trilioni 1.3) ndani ya miaka mitano ijayo. Juhudi za kuwaunganisha wazalishaji wa ndani na wafanyabiashara wa Urusi zimeshaanza nchini.

Mbali na biashara, ziara hiyo imefungua milango mipya kwa vijana wa Kitanzania katika maeneo yafuatayo:

Ajira: Serikali imeomba rasmi nafasi 500 za masomo kwa ajili ya vijana wa Kitanzania nchini Urusi, huku kampeni ya kuongeza fursa hizo ikiendelea.

Elimu Nafuu: Kumefanyika mazungumzo na vyuo vikuu vya umma na binafsi vya Urusi ili kuwapa wanafunzi wa Kitanzania nafasi ya kusoma shahada mbalimbali kwa gharama nafuu ya Dola 5,000 tu kwa mwaka—gharama ambayo ni ndogo ukilinganisha na nchi nyingine zilizoendelea.

Mtikisiko huu chanya ulioripotiwa na Balozi Kombo unathibitisha namna Tanzania inavyoendelea kuchanja mbuga kimataifa, ikijitofautisha kama nchi inayojua kutumia fursa za kijiografia na kidiplomasia kwa maslahi ya kiuchumi ya watu wake.

Saturday, June 6, 2026

PUTIN AIKUBALI TANZANIAtin NA KUELEZEA JINSI ILIVYO MUHIMU

 


Na Beda Msimbe, TBN, Petersburg

Rais Vladimir Putin wa Urusi amesema Tanzania ni lango kuu la kimkakati linalounganisha soko la Afrika Mashariki na masoko ya kimataifa.

Aidha amesema katika uchumi wa dunia unaozidi kubadilika kuelekea mifumo ya nguzo nyingi za kiuchumi, taifa la Tanzania umuhimu  mkubwa katika kuyfanikisha ustawi wa jamii mbalimbalio. 

Akizungumza Juni 5 katika Jukwaa la Kimataifa la Uchumi la St. Petersburg la mwaka 2026 Rais Putin amesema kuwa Tanzania katika utendaji ni taifa la kimkakati  katika ukanda wa Afrika Mashariki unaofanana na ule wa nchi ya Uzbekistan katika ukanda wa Asia ya Kati ikifanya kazi kama kiungo muhimu sana kati ya uchumi wa kikanda na vituo vikuu vya biashara ya kimataifa duniani. 

Kiongozi huyo amebainisha hayo wakati akizungumzia mataifa ambayo kutokana na nafasi zao za kijiografia na mahusiano yao ya kiuchumi yanageuka kuwa madaraja muhimu kati ya kanda tofauti duniani na kuongeza kuwa mataifa yenye uwezo wa kuoanisha maendeleo yao ya ndani na miunganisho madhubuti kwenye vituo vipya vya ukuaji wa uchumi wa kimataifa yanazidi kuwa muhimu wakati mifumo ya biashara ya kimataifa inavyoendelea kubadilika.

Kauli hizi nzito kutoka kwa Rais Putin zinakuja wakati ambao Tanzania inaendelea kupanua kwa kasi miundombinu yake ya usafirishaji ikiwemo bandari na njia za biashara za kikanda ili kuimarisha nafasi yake kama kitovu kikuu cha biashara kwa ukanda mzima wa Afrika Mashariki na Kati na hivyo kutafsiri kwa vitendo malengo makubwa ya ukuaji wa kiuchumi.

Rais Samia Suluhu Hassana alishiriki katika jukwaa hilo amnbapo alipata nafasi ya kuelezea mambo mbalimbali yanayohusiana na uwekezaji na pia biashara.

Aidha alisema kwamba Tanzania ipo tayari kushirikiana na mataifa yoyote ikiwamo Russia ili kupeleka fursa mbalimbali za maendeleo kwa wananchi wake. Akijibu swali kwamba Russia ina vikwazo, Rais Samia alisema Tanzania haina vikwazo inafanyakazi na washirika wote wanaoitakia mema nchi yake.

mwisho

RAIS SAMIA AWASILI NCHINI AKITOKEA ZIARA YA MAFANIKIO URUSI

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na Makamu wa Rais Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel John Nchimbi pamoja na Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Balozi Dkt. Asha-Rose Migiro mara baada ya kuwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere tarehe 06 Juni, 2026 baada ya kuhitimisha Ziara yake ya Kitaifa, St. Petersburg nchini Urusi tarehe 05 Juni, 2026 kufuatia mwaliko wa Rais wa Nchi hiyo Mhe. Vladmir Putin.







Samia Suluhu Hassan akisalimiana na viongozi mbalimbali baada ya kuwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere tarehe 06 Juni, 2026 baada ya kuhitimisha Ziara yake ya Kitaifa, St. Petersburg nchini Urusi tarehe 05 Juni, 2026