Na Mwandishi Wetu, TBN, Dar es salaam
Mikataba na hati za makubaliano manane (8) zilizosainiwa kati ya Tanzania na Urusi, ndizo zilizoweka msingi mkuu wa ushirikiano mpya wa kiuchumi, kijamii na kiteknolojia unaotarajiwa kupandisha hadhi ya nchi hizi mbili.
Makubaliano haya makubwa, ambayo ni matunda ya moja kwa moja ya ziara ya kihistoria ya Rais Samia Suluhu Hassan nchini Urusi, yanajenga daraja imara la maendeleo katika sekta tisa za kipaumbele: kilimo, elimu, nishati, madini, viwanda, utalii, usafirishaji, uchumi wa kidijiti, pamoja na biashara na uwekezaji.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo, ameanika hadharani undani wa makubaliano hayo manane yanayobeba mustakabali wa nchi:
Kutoka Diplomasia ya Lugha Hadi Mapinduzi ya Afya na Elimu ya Juu
Katika makubaliano ya kwanza, Tanzania na Urusi zimeamua kutumia lugha kama silaha ya kidiplomasia. Kupitia hati ya ushirikiano kati ya Baraza la Kiswahili la Taifa (BAKITA) na Chuo Kikuu cha Mahusiano ya Kimataifa cha Urusi (MGIMO), lugha ya Kiswahili itazidishwa kasi ya kufundishwa nchini Urusi, huku Tanzania nayo ikijipanga kuanza kufundisha Kirusi kupitia Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM).
Makubaliano ya pili yamejikita kwenye sekta ya afya, ambapo Chuo Kikuu cha Muhimbili (MUHAS) kimeingia ubia na taasisi mbili za afya za Urusi kwa ajili ya kubadilishana utaalamu wa matibabu na kuongeza nguvu katika uzalishaji wa dawa nchini.
Kwenye upande wa elimu, makubaliano ya tatu na ya nne yanakuja kutatua changamoto za ajira na teknolojia ya kisasa:
Wizara za Elimu za nchi zote mbili zimesaini makubaliano ya kutambua vyeti na tuzo za kitaaluma zinazotolewa Urusi, hatua itakayowawezesha Watanzania waliosoma nchini humo kupata ajira kwa urahisi nyumbani.
Taasisi ya Teknolojia ya Dar es Salaam (DIT) imesaini mkataba na Chuo cha Urafiki cha Urusi kuanzisha programu za pamoja za Shahada ya Kwanza na Uzamili katika fani za kisasa kabisa duniani—ikiwemo Sayansi ya Takwimu, Mfumo wa Anga, Akili Unde (AI), na Ujifunzaji wa Mashine (Machine Learning).
Kuvutia Mitaji ya Magharibi, Siri za Nishati na Ajira za Vijana
Makubaliano ya tano na ya sita yanalenga kufungua milango ya mitaji mikubwa. Kupitia Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalumu ya Kiuchumi Tanzania (TISEZA), nchi imepewa fursa ya kuhamasisha uwekezaji hadi kuelekea mataifa ya Ulaya.
Zaidi ya hapo, Tanzania imeingia ushirikiano na Kampuni ya Roscongress ya Urusi—miamba ya kuandaa makongamano ya kimataifa—kwa lengo la kutengeneza miradi ya ubia na kuvutia wawekezaji sio tu kutoka Urusi, bali pia kutoka nchi za Magharibi.
Mkataba wa saba uligusa sekta nyeti ya nishati, ambapo Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) na Kampuni ya Mantra Tanzania Ltd (Kmapuni tanzu ya Shirika la Nyuklia la Urusi, Rosatom) zimesaini makubaliano ya kulinda na kutunza siri za taarifa za kimkakati katika miradi ya nishati.
Kama kilele cha makubaliano hayo, kubaliano la nane ni mpango kabambe wa miaka mitano unaolenga kukuza uchumi na kuzalisha fursa za ajira kwa vijana wa Kitanzania nchini Urusi.
"Haya ni matunda halisi ya kiuchumi yaliyotokana na maono ya mheshimiwa Rais," alisisitiza Profesa Kitila Mkumbo, akibainisha kuwa utekelezaji wa makubaliano haya unaenda kuweka alama ya kudumu katika soko la ajira na uwekezaji nchini.







.jpeg)

.jpeg)

