Banner

Banner

FOLLOW US FACEBOOK

propertyfinder.co.tz

Tuesday, July 7, 2026

WAZIRI MKUU: TUTAFUTE MBINU MPYA ZA KUKIENEZA KISWAHILI

 


WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amesema kuna haja ya kutafuta mbinu mpya ya kukieneza Kiswahili baada ya kuwa kimepata hadhi ya kimataifa.

“Kadiri Kiswahili kinavyoendelea kupata hadhi ya kimataifa, ni muhimu sasa kuanza kutazama hatua inayofuata ya kukieneza duniani. Mataifa mengi yamefanikiwa kueneza lugha na utamaduni wao kupitia vituo vya utamaduni vilivyoanzishwa katika nchi mbalimbali duniani,” amesema.

Ametoa wito huo leo (Jumanne, Julai 7, 2026) wakati akizungumza na washiriki waliohudhuria kilele cha Maadhimisho ya Tano ya Siku ya Kiswahili Duniani kwenye ukumbi wa mikutano wa ofisi za makao makuu ya UNESCO jijini Paris, Ufaransa. 

“Serikali itaendelea kuimarisha matumizi ya Kiswahili ndani na nje ya nchi kupitia elimu, tafiti, uchapishaji, tafsiri, teknolojia za kidijiti na diplomasia ya lugha. Tutaendelea kushirikiana na UNESCO, nchi mbalimbali, vyuo vikuu, taasisi za kimataifa na wadau mbalimbali katika kuendeleza lugha hii kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho,” amesema.

Waziri Mkuu ambaye alikuwa mgeni rasmi kwa niaba ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema sasa hivi Kiswahili kimeshatambulika kuwa lugha rasmi ya EAC na SADC. “Kiswahili ndiyo utambulisho wetu wana jumuiya ya Afrika Mashariki. Mtu akiongea Kiswahili anajulikana kuwa anatokea Tanzania, Burundi, Congo au Sudan Kusini. Na pia kimekuwa moja ya lugha rasmi za Umoja wa Afrika (AU),” amesema.

“Si hivyo tu, sasa hivi Kiswahili kinatambulika kuwa ni lugha rasmi ya mikutano mikubwa ya UNESCO kutokana na pendekezo lililopitishwa kwa kaulimoja Novemba, 2025 wakati wa Mkutano Mkuu wa 43 wa UNESCO, uliofanyika Samarkand, Uzbekistan.”

Amesema kwa mujibu wa wataalamu wa lugha, Kiswahili kinazungumzwa na watu kati ya milioni 300 hadi milioni 500 na idadi hiyo inaendelea kuongezeka kutokana na matumizi yake katika elimu, biashara, vyombo vya habari, teknolojia ya habari na mawasiliano pamoja na mitandao ya kijamii.

“Hali hiyo inaonesha kwamba Kiswahili siyo mali ya Watanzania pekee bali ni urithi wa Afrika na zawadi ya Afrika na dunia. Kiswahili kinaunganisha watu, Kiswahili kinaunganisha biashara, Kiswahili kinaunganisha jamii,” amesisitiza.

Mapema, Mkurugenzi Mkuu wa UNESCO, Prof. Khaled El-Enany aliwaeleza washiriki wa maadhimisho hayo kwamba shirika lake limesaidia kufadhili uandaaji wa kamusi ya Kifaransa kwenda Kiswahili.

“Mbali na matumizi ya kawaida kwa watalii au watu wanaojifunza lugha, tunatarajia kwamba uwepo wa kamusi hiyo na nyaraka nyingine kutasaidia kuongeza fursa kwa walimu na wanafunzi wanaojifunza Kifaransa na Kiswahili,” amesema.

Amesema uzuri wa Kiswahili ni lugha ambayo imekuwa ikiendelea kukua na kuvuka mipaka bila kupoteza uasili wake na imeunganisha watu bila kulazimika kuvuka mipaka ya nchi zao.

Akimkaribisha Waziri Mkuu kuzungumza na washiriki hao, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda alisema Tanzania ina lugha za makabila zaidi ya 150 katika maeneo mbalimbali lakini wananchi wake wameweza kuunganishwa na lugha moja ya Kiswahili.

Alisema wakati jijini Paris, Ufaransa wakiadhimisha kilele cha maadhimisho hayo na kongamano la pili lililoandaliwa na UNESCO kwa kushirikiana na Serikali ya Tanzania, nchi nyingine tatu za Uingereza, Algeria na Burundi nazo pia leo zimeadhimisha makongamano kama hayo.

Awali, Balozi wa Tanzania nchini Ufaransa, Bw. Saidi Othman Yakub alisema maadhimisho hayo ya tano ambayo yanafanyika sambamba na Kongamano la Pili la Siku ya Kiswahili Duniani, yamevutia washiriki zaidi ya 300 kutoka nchi 16 duniani. 

Amezitaja nchi hizo kuwa ni Comoro, Tanzania, Ujerumani, Marekani, Canada, Uingereza, Italia, Luxembourg, Sweden, Ubelgiji, Austria, Uturuki, Misri, Kenya, Uganda na wengi kutoka Tanzania.

“Tangu tarehe 4 Julai hadi leo tarehe 7 Julai, 2026 tumeshuhudia shughuli mbalimbali zilizolenga kuendeleza na kukitangaza Kiswahili duniani. Shughuli hizo zilijumuisha matembezi ya hamasa katika mitaa maarufu ya Jiji la Paris, hafla za vyakula vya Kiswahili kwa Diaspora, kongamano kuhusu nafasi ya Kiswahili katika biashara na uchumi, semina na warsha mbalimbali hapa UNESCO.

Amesema waliandaa pia tamasha la Usiku wa Mswahili lililofanyika chini ya Mnara wa Eiffel kandokando ya Mto Seine, maonesho ya filamu na chakula pamoja na kazi za Kiswahili.






Sunday, June 28, 2026

Mhe. ABDALLAH ULEGA ATAKA BARABARA ZA AFCON ZIKAMILIKE KWA WAKATI

 

Waziri wa Ujenzi, Abdallah Ulega, ameagiza kujengwa kwa kasi zaidi kwa miradi ya miundombinu itakayohusika na Mashindano ya AFCON ambayo Tanzania itakuwa mwenyeji mwakani. 

Ulega ameyasema hayo leo mjini Arusha wakati akikagua maendeleo ya ujenzi wa barabara ya Mbauda - Losinyai yenye urefu wa km 70 ambayo ni miongoni mwa barabara muhimu kwa AFCON. 

“Nimekagua barabara hii na nimemsisitiza Mkandarasi kuongeza idadi ya vifaa, watalaam na wafanyakazi wa kutosha katika mradi huo na kuweka kambi zinazojitegemea ili kuondoa ucheleweshaji wa kuhamisha vifaa na mitambo kutoka eneo moja hadi jingine”, amesisitiza Ulega.

Barabara hiyo inajengwa na mkandarasi, kampuni ya China Civil Engineering Cinstruction Corporation  (CCECC) na inahusu barabara ya Mbauda - Losinyai (km 70) hususan sehemu ya barabara Mbauda - Morongo hadi Makutano ya Arusha na T/Packers (Moshono) hadi Kiserian (km 13).

Waziri huyo amemtaka Mkandarasi huyo kufanya kazi kazi usiku na mchana ili mradi huo ukamilike viwango vya ubora kabla ya kuanza kwa AFCON. 

Barabara  hiyo inajengwa  kuwa njia nne kwa utaratibu wa Sanifu, Jenga. 

Ulega ameeleza kuwa Mhe Rais Dkt. Samia Suluhh Hassan ameendeela kutoa kipaumbele kwa ujenzi wa miundombinu ya kisasa ili kuboresha maisha ya wananchi na kukuza pato la Taifa.

Ameongeza kuwa mradi huo ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kuimarisha mtandao wa barabara ndani ya jiji la Arusha ukiunganisha maeneo mbalimbali muhimu ya Mbauda, kwa mrombo, barabara ya Bypass, Soko la Kilombero hadi Uwanja wa Ndege wa Kisongo hadi Uwanja wa AFCON.

Aidha, Ulega ametoa maelekezo kwa TANRAODS na Mkandarasi kuhakikisha wanatoa fursa za ajira kwa vijana hususani wa Mkoa wa Arusha wanaopitiwa na mradi kupitia ngazi ya ofisi ya Mkuu wa Wilaya ili mradi huo uweze kuwanufaisha kuongeza kipato na shughuli zao za kiuchumi.

Vilevile, Ulega amezitaka Taasisi za TANESCO na AUWASA kuharakisha kuhamisha miundombinu ya maji na umeme iliyopo katika barabara hiyo ili kuharikisha utekelezaji wake kwa urahisi na kwa ufanisi.

Kadhalika, Ulega ametoa rai kwa wananchii kuendelea kutoa ushirikiano kwa uongozi wa ngazi ya Wilaya, timu ya wataalam na mkandarasi na ili kazi ziende kwa haraka.

Naye, Mbunge wa Jimbo la Arusha, ambaye pia ni Waziri wa Habari, Utamaduni Sanaa na Michezo Paul Makonda ameeleza kuwa Arusha mpya yenye miundombinu bora inakuja chini ya Rais Dkt Samia Suluhu Hassan na hii inaonesha dhahiri kila kona unapokwenda katika Mkoa huu barabara zinajengwa.

Kwa upande wake, Meneja wa TANROADS mkoa wa Arusha, Mhandisi Reginald Masawe amesema kuwa mkataba wa mradi huo wenye thamani ya Shilingi Bilioni 221 ulianza kutekelezwa Aprili 10, 2026 baada ya Mkandarasi kulipwa malipo na kupewa kibali cha kuanza kazi na unatarajiwa kukamilika Machi 25, 2029

Ameeleza kuwa barabara hiyo itajengwa kwa kiwango cha kisasa, ikiwa na njia za watembea kwa miguu, mifereji ya kisasa ya maji pamoja na taa za barabarani.

Tuesday, June 16, 2026

RAIS SAMIA ATUMA UJUMBE MAALUM KWA UMOJA WA MATAIFA

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Mahmoud Thabit Kombo (Mb), amewasilisha ujumbe maalum wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Mhe. António Guterres, na kusisitiza dhamira ya Tanzania ya kuimarisha ushirikiano wa kimataifa, amani na maendeleo endelevu.

Baada ya mazungumzo yao, Mhe. Mahmoud Thabit Kombo (Mb) alimkabidhi Mhe. António Guterres zawadi ya kitabu kuhusu Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Rais wa Kwanza wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kutambua kuvutiwa kwa muda mrefu kwa Katibu Mkuu huyo na maono, uongozi na mchango wa Mwalimu Nyerere katika kuhimiza amani, maendeleo na ushirikiano wa kimataifa.

MAMA NEEMA MWIGULU AHIMIZA TAASISI KUUNGA MKONO JUHUDI ZA SERIKALI KUPITIA UWAJIBIKAJI KWA JAMII

Mwenza wa Waziri Mkuu, Mama Neema Mwigulu Nchemba, amehimiza taasisi za umma na binafsi kuendelea kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuboresha huduma za kijamii kupitia utekelezaji wa programu za uwajibikaji kwa jamii (CSR).

Mama Neema amesema hayo leo Jumanne, Juni 16, 2026 katika hafla ya kukabidhi vifaa vya hospitali vilivyotolewa na Shirika la Viwango Tanzania (TBS) katika Hospitali ya Wilaya ya Chamwino, Mkoa wa Dodoma, ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 50 ya shirika hilo.

Mama Neema ambae alikuwa mgeni rasmi katika hafla hiyo, amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imefanya uwekezaji mkubwa katika sekta ya afya kupitia ujenzi wa miundombinu ya kutolea huduma za afya, ajira kwa wataalamu wa afya, upatikanaji wa dawa na vifaa tiba pamoja na kuimarisha huduma za kibingwa na ubingwa bobezi.

“Tunashuhudia maboresho makubwa katika sekta ya afya kutokana na uwekezaji unaoendelea kufanywa na Serikali. Leo tunajivunia huduma nyingi ambazo hapo awali zilikuwa zinapatikana nje ya nchi kupatikana hapa nchini,” amesema.

Mama Neema amewapongeza viongozi wa Shirika la Viwango Tanzania kwa kuendelea kutekeleza kwa vitendo sera ya uwajibikaji kwa jamii na kuchangia ustawi wa wananchi kupitia sekta ya afya pamoja na makundi mbalimbali yenye mahitaji maalum.

Amesema vifaa vilivyotolewa vitasaidia kuboresha utoaji wa huduma katika Hospitali ya Wilaya ya Chamwino na kuongeza ustawi wa mama na mtoto.

Vifaa hivyo vinajumuisha vitimwendo 20, vitanda vya kujifungulia vitano, vitanda vya kufanyia uchunguzi vitano, vitanda vitano vya kulaza wagonjwa, machela moja ya kisasa, makabati matatu ya kuhifadhia vifaa tiba pamoja na mabeseni yenye vifaa mbalimbali kwa ajili ya akinamama 30 waliojifungua.

Awali, akimkaribisha mgeni rasmi kuzungumza katika hafla hiyo, Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga amesema Serikali itaendelea kuhimiza taasisi zake kutekeleza kwa vitendo sera ya uwajibikaji kwa jamii ili kuchangia kuboresha huduma za kijamii na maisha ya wananchi.

Amesema msaada uliotolewa na Shirika la Viwango Tanzania (TBS) katika Hospitali ya Wilaya ya Chamwino ni sehemu ya mchango wa taasisi za umma katika kuunga mkono jitihada za Serikali za kuimarisha huduma za afya nchini pamoja na kuendelea kuyaishi maono ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuboresha ustawi wa wananchi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Viwango Tanzania (TBS), Dkt. Ashura Katunzi amesema shirika hilo limeendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya kijamii katika sekta ya afya, elimu na makundi maalum ikiwa ni sehemu ya mchango wake kwa maendeleo ya jamii.

Amesema TBS itaendelea kushirikiana na Serikali na wadau mbalimbali katika kuboresha maisha ya wananchi kupitia programu zake za uwajibikaji kwa jamii.

Monday, June 15, 2026

TAARIFA KWA UMMA

 

Ofisi ya Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, inapinga na kukanusha vikali taarifa ya uongo na upotoshaji inayosambaa mitandaoni, ikidai kuwa Dkt. Kikwete anahusishwa na mradi unaodaiwa kuwa wa uwekezaji unaowaahidi Watanzania kipato cha uhakika kupitia jukwaa la kifedha linalotumia teknolojia ya akili mnemba.

Taarifa hiyo inadai kuwa maelfu ya Watanzania tayari wamenufaika na mradi huo baada ya kuwekeza kiasi cha shilingi 653,000, huku wakiahidiwa kupata zaidi ya shilingi 9,200,000 kwa mwezi. Madai hayo si ya kweli hata kidogo.

Ofisi ya Rais Mstaafu inapenda kuweka wazi kwamba Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete hajawahi kushiriki, kuidhinisha, kutangaza, kuunga mkono, wala kuhusika kwa namna yoyote ile na mpango huo wa kifedha. Ofisi yake haijawahi kuruhusu matumizi ya jina, picha, au heshima yake kuhusishwa na mradi huo unaodaiwa, na haitajihusisha na shughuli za aina hiyo.

Wananchi wanashauriwa kupuuza taarifa hiyo ya uongo na kuwa makini dhidi ya miradi ya kitapeli na vitendo haramu vya aina hiyo. Mtu yeyote atakayekutana na taarifa kama hizo za upotoshaji anapaswa kuzichukulia kama habari za uongo, kuepuka kuzisambaza, kujisajili, au kutuma fedha kwa mtu au jukwaa lolote linalohusishwa nazo.

TAARIFA YA UONGO IPUUZWE.

Marekani na Iran Zafikia Makubaliano ya Amani

 


#HABARI Baada ya miezi ya mvutano uliotikisa Mashariki ya Kati, Marekani na Iran zimetangaza kufikia makubaliano ya awali ya kumaliza mzozo uliokuwa ukiendelea kati yao. 

Hatua hiyo imeelezwa kama mafanikio makubwa ya kidiplomasia yanayolenga kurejesha utulivu katika eneo hilo.

Rais wa Marekani Donald Trump alitangaza kuwa makubaliano hayo yamekamilika, huku Waziri Mkuu wa Pakistan Shehbaz Sharif akisema nchi yake ilisaidia katika mazungumzo yaliyowezesha kufikiwa kwa mwafaka huo. 

Makubaliano hayo yanajumuisha kusitishwa mara moja kwa operesheni zote za kijeshi katika maeneo ya mapigano, ikiwemo Lebanon.

Aidha, Iran imethibitisha kuwa shughuli za kijeshi zitasitishwa kuanzia Jumatatu usiku. 

Makubaliano hayo pia yanatarajiwa kufungua tena Mlango-Bahari wa Hormuz, njia muhimu ya usafirishaji wa mafuta na gesi duniani, hatua inayoweza kusaidia kuimarisha biashara na uchumi wa kimataifa.

Sunday, June 14, 2026

WAZIRI SHEMDOE AAGIZA UJENZI WA BARABARA ZA AFCON KUJENGWA USIKU NA MCHANA

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM -TAMISEMI) Prof. Riziki Shemdoe amemshukuru Rais wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uwekezaji mkubwa alioufanya Mkoani Arusha katika ujenzi wa barabara kuelekea katika mashindano ya Mpira wa miguu kwa Mataifa ya Afrika (AFCON 2027) inayotarajiwa kuchezwa katika Mikoa ya Arusha, Dar Es Salaam na Visiwani Zanzibar.

Profesa Shemdoe ametoa shukrani hizo leo Jumapili Juni 14, 2026 wakati wa ziara yake Mkoani Arusha, akiambatana na Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mhe. CPA Amos Gabriel Makalla na viongozi wengine wa Serikali na Chama Cha Mapinduzi CCM, kukagua mradi wa uwanja wa AFCON pamoja na barabara ya kuingia katika uwanja huo unaojengwa kwenye Kata ya Olmot, Jijini Arusha, akiagiza kasi zaidi katika kukamilisha kazi hizo.

"Kwa kazi hizi kwakweli najisikia fahari kuwa Mtanzania. Nielekeze kazi ya ujenzi wa barabara ifanyike usiku na mchana, niagize pia uadilifu katika usimamizi na utoaji wa  fidia kwa wananchi waliopisha ujenzi wa barabara hii. Nimshukuru sana Mhe. Rais kwa kutoa zaidi ya Shilingi Bilioni 80 ya ujenzi wa barabara hizi na zipo pia Bilioni 14.8 kwaajili ya fidia kwa wananchi." Amesema Mhe. Waziri.

Kwa upande wake Mhe. Makalla ameahidi kusimamia kikamilifu maelekezo yote ya Mhe. Waziri Shemdoe, ikiwemo usimamizi wa ujenzi wa uwanja huo wa AFCON pamoja na miundombinu ya barabara na maboresho ya viwanja vya ndege, ikiwemo barabara za kutoka Uwanja wa Ndege wa Kilimanjaro mpaka kufika katika uwanja huo wa Michezo.

Mapema katika maelezo yao, Msimamizi wa uwanja wa AFCON kutoka Wizara ya Habari, Utamaduni, sanaa na Michezo Bw. Martin Chomo na Mkurugenzi wa barabara kutoka Wakala wa barabara za Vijijini na Mijini TARURA, Injinia Venant Komba, wameeleza kuhusu maendeleo ya miradi hiyo na kuahidi kukamilisha kwa wakati ikiwemo viwanja vidogo vitano vitakavyotumika kwaajili ya mazoezi kwa Timu zitakazopangiwa kucheza Michezo yake Mkoani hapa.