Banner

Banner

FOLLOW US FACEBOOK

propertyfinder.co.tz

Wednesday, June 3, 2026

URUSI KUFUNGUA FURSA LUKUKI TANZANIA

 

Na muandishi wa TBN, Urusi.                 

 Urusi imesema taifa hilo litafungua fursa lukuki kwa taifa la Tanzania kwa manufaa ya pande zote mbili.

Aidha taifa hilo lenye miradi 70 yenye thamani ya dola za Marekani milioni434.22 ikiwa imewezesha ajira 3018 tanzania limesema kuwa litatangaza fursa hizo katika mkutano wa uchumi wa kimataifa kesho kutwa.             Akizungumza na waandishi wa habari baada ya kikao chake na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kiongozi wa Urusi Vladimir Putin amesema Urusi imekuwa ikifuatilia kwa makini mageuzi yanayofanyika nchini tanzania na wanaona inavyokua.        Amesema amekuwa na mazungumzo yenye manufaa makubwa kwa jamii ya pande zote mbili na kuahidi kuendelea na ushirikiano na Tanzania.        Naye rais Samia amesema kuwa ziara yake katika Shirikisho la Urusi ina umuhimu mkubwa wa kihistoria kwake binafsi na kwa taifa la Tanzania kwa ujumla. 

“Ziara yangu ina umuhimu wa pekee wa kihistoria kwangu binafsi na kwa nchi yangu. Imepita zaidi ya nusu karne tangu kufanyika kwa ziara ya mwisho ya kiserikali ya Tanzania nchini Urusi. Hivyo, kwangu hii ni safari ya kihistoria sana kuja Urusi kujadili masuala mbalimbali ya ushirikiano wa pande mbili, pamoja na maendeleo endelevu kwa wananchi wetu. Kwa niaba yangu na wananchi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, napenda kutoa shukrani zetu za dhati kwa mwaliko huu,” alisema Rais Samia.

Aidha, Rais Samia alikumbusha mchango mkubwa wa Urusi katika harakati za Tanzania za kupigania uhuru na kumpongeza Rais Putin kwa maadhimisho ya miaka 81 ya Ushindi katika Vita Kuu ya Pili ya Dunia yaliyofanyika Mei 9 mwaka huu.

Rais Samia aliwasili Moscow kwa ziara yake ya kwanza nchini Urusi, ambayo pia ni ziara ya kwanza ya kiongozi wa Tanzania nchini humo katika kipindi cha zaidi ya miaka 50, kwa ajili ya mazungumzo na Rais Putin.

Viongozi hao kwa mujibu wao walijadili masuala mbalimbali yanayohusu kuimarisha zaidi uhusiano wa kirafiki na ushirikiano kati ya nchi hizo mbili. Vilevile, walibadilishana mawazo kuhusu masuala muhimu yanayohusu ajenda za kimataifa na kikanda.

Mwisho.

RAIS WA JAMUHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA MHE. DKT. SAMIA SULUHU HASSAN AWEKA SHADA KWENYE KABURI LA ASKARI ASIYEFAHAMIKA


 Na mwandishi wa TBN, Urusi

KENGELE kubwa iliyogongwa mara tisa, bendi ya jeshi ikiongoza nyimbo za maombolezo Rais Dk Samia Suluhu Hasan majira ya saa tano na dakika 23 aliweka shada la maua kwa kaburi la askari asiyefahamika, mjini hapa.

Aidha Baada ya shughuli la uwekaji wa taji hilo katika eneo ambalo moto huwaka daima ikiwa ni kumbukumbu ya wapiganaji wa Urusi waliopoteza maisha katika vita kuu ya pili, gadi tatu zilipita kwa mwendo wa haraka na kutoa heshima kwa Rais Samia baada ya kupigwa kwa wimbo wa taifa la Tanzania.

Hali ya  askari katika uwanja huo walioonesha nidhamu ya hali ya juu ya kusimama tisti katika maeneo yao bila kutikisika , ubadilishanaji wa gadi za ulinzi na pia mwendo wa pole ambao ulimsindikiza Rais Samia kwenda kwenye tukio la uwekeaji wa shahada. Vilikuwa vitu vinavyovutia kuangalia.

Rais Samia ambaye yupo katika ziara ya kiserikali nchini hapa  baadaye alienda kukutana na mwenyeji wake Rais Vladmir Putin.

Zaidi ya maofisa 300 wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania JWTZ wamepata nafasi ya masomo katika nchi ya Urusi kwa ajili ya shahada ya kwanza na ya pili.

Askari hao wameenda kujifunza masuala ya kupambana na ugaidi, sayansi na teknolojia,mafunzo ya kijeshi, ulinzi wa amani, ununuzi na uhifadhi wa silaha,namna ya kukabiliana na majanga.

Tanzania na Urusi zina ushirikiano wa kijeshi kwa kuzingatia makubaliano ya ushirikiano wa kijeshi yaliyosainiwa mwaka 2016  na makubaliano ya mwaka 2018 ya ushirikiano wa kifundi wa kijeshi.

Tanzania yenye ukuaji wa uchumi wa asilimia 5.5 kwa mwaka 2024 na ikikadiriwa kufikia asilimia 6 mwaka huu na ikiwa na mkakati wa kuhakikisha kwamba Dira ya maendeleo ya mwaka2050 inatekelezwa ziara ya Rais Samia nchini Urusi inatarajiwa kuzaa matunda yanayotarajiwa  ya kuinua sekta ya ajira kukuza biashara na kuimarisha uwekezaji.

Mwisho

RAIS WA JA.HURI YA MUUNGANO WA TANZANIA MHE. DKT. SAMIA SULUHU HASSAN ANATARAJIWA KUTUNUKIWA SHAHADA YA UZAMIVU NA CHUO KIKUU CHA RUDIN NCHINI URUSI

Rais Dkt Samia Suluhu Hassan ambaye yupo hapa shirikisho la Urusi kwa ziara ya kitaifa anatarajiwa kutunukiwa shahada ya uzamivu na Chuo Kikuu cha Rudin nchini hapa.

Tuzo hiyo inatokana na kutambua kazi yake na mchango wake katika jami ya Tanzania na dunia katika masuala ya msingi yanayohusu Maisha ya binadamu.

Chuo cha RUDIN chenye wanafunzi wa kitanzania 570 kufikia mwaka 2025 katika miaka zaidi ya 65 ya RUDIN, watanzania 1,132 wamepitia chuo hicho.

RUDIN kimesomesha zaidi ya wataalamu 200,000 duniani na sasa ina watu 44,000 kutoka nchi 160 duniani. Chuo hiki ni cha 367 kwa ubora duniani kwa mujibu wa QS World University Ranking ya mwaka 2025.

Rais Dkt Samia ambaye amepokelewa jana na Waziri wa maendeleo ya Uchumi wa Russia Maxim Reshetnikov anatarajiwa kukutana na mwenyeji wake Rais Vladimir Putin na kufanya mazungumzo ya ana kwa ana kwa ajili ya kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia na kiuchumi.

Aidha akiwa nchini hapa, akiwa kiongozi wa pili wa Tanzania kutembelea Urusi, ziara ya kwanza ikiwa imefanywa na baba wa taifa Mwalimu Julius Nyerere, atashiriki Jukwaa la uchumi la St Petersburg ambapo tanzania itanadi fursa za uwekezaji, na diplomasia ya Uchumi kwa viongozi, wawekezaji na watunga sera wa kimataifa.

Katika kufanikisha dira ya Maendeleo 2050 ziara hii ni kikolezo cha utekelezaji kwa mafanikio ya dira hiyo ambayo inahitaji raslimali watu wenye utaalamu na upeo mkubwa kusimamia na kuendesha miradi ya kimkakati itakayopelekea ajira, viwanda na biashara zitakazoingiza dola trilioni moja na kuwa katika uchumi wa kati wa juu.

Katika WhatsApp yake Rais Samia amesema Ziara hiyo ni muhimu hasa taifa linapoelekea kuanza utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050 ambayo inataka ushiriki mkubwa wa sekta binafsi. "Tutafanya mazungumzo na wenyeji wetu yanayolenga kuimarisha ushirikiano katika sekta za kimkakati zinazogusa maisha ya wananchi." 

"Aidha, tutashiriki majukwaa ya biashara na uwekezaji na kutatangaza fursa zilizopo nchini, pamoja na kufungua zaidi fursa za masoko kwa bidhaa za Tanzania nchini Urusi."

Mwisho

RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA MHE. DKT. SAMIA SULUHU HASSAN AMEWASILI JIJINI MOSCOW KWAAJILI YA YA ZIARA YA KITAIFA NCHINI URUSI





 Na Beda Msimbe, TBN, Moscow

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amewasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Vnukovo, uliopo Jijini Moscow kwa ajili ya Ziara ya Kitaifa, nchini Urusi

Katika ziara hii ya kihistoria ikifanywa kwa mara ya pili katika historia ya uhusiano wa Tanzania na Urusi, ya kwanza ilikuwa ni miaka ya 1960 iliyofanywa na baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere, Rais Samia anaendeleza kampeni kubwa ya kuhakikisha Tanzania inanufaika pia kiuchumi na uhusiano mzuri na mataifa mbalimbali

 Kwa mujibu wa shughuli atakazofanya Rais Samia akiwa hapa nchini kwa lengo la kuimarisha uhusiano wa Kidiplomasia, kisiasa, kiuchumi na kihistoria baina ya Tanzania na Urusi,Rais amekuja kuiweka Tanzania katika ramani ya uwekezaji kwa ushiriki wake katika mkutano mkubwa wa uwekezaji jijini St Petersburg na pia kuona namna ya kutengeneza raslimali watu ambayo taifa inahitaji sana katika kufanikisha utekelezaji wa dira ya maendeleo ya 2050. 

Alipowasili nchini hapa katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Vnukovo, Jijini Moscow  majira ya saa mbili na dakika 25 usiku , japo jua bado lilikuwa linawaka,  Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan alipokea heshima ya wimbo wa Taifa pamoja na gwaride.

Rais Samia alipokewa uwanjani na Waziri wa Maendeleo ya Uchumi wa Shirikisho la Urusi Mhe. Maxim Reshetnikov. 

Kwa mujibu wa ratiba leo asubuhi ataanza na kuweka shada ka maua kwa kaburila askari asiyejulikana kabla ya kwenda Ikuku ya Kremlin kwa mazungumzo na Rais Vladmir Putin.

mwisho

Friday, May 29, 2026

MIAKA 18 BAADAYE: JK AKUTANA TENA NA CATHERINE, BINTI ALIYEFANYIWA UPASUAJI WA MOYO AKIWA NA MIAKA MINNE


Rais mstaafu wa Awamu ya Nne Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, leo Mei 29, 2026 amekutana tena na Bi. Catherine P. Conrad Minja, aliyefanyiwa upasuaji wa moyo kwa mafanikio akiwa na umri wa miaka minne katika taasisi ya  Muhimbili Orthopaedic Institute  (MOI) miaka 18 iliyopita.

Wakati huo madaktari bingwa wa Moyo wa Taasisi ya Moyo ya JKCI walikuwa wakitumia majengo ya MOI kabla jengo lao halijakamilika.

Mara ya kwanza wawili hao walikutana Novemba 14, 2008 wakati Dkt. Kikwete akiwa Rais alipokwenda kumjulia hali Catherine  hapo MOI baada ya kufanyiwa upasuaji wa moyo mapema wiki hiyo. Wakati huo Catherine alikuwa mmoja wa wagonjwa wa mwanzo kufanyiwa upasuaji huo katika taasisi hiyo.

Miaka 18 baadaye, Catherine amekua na sasa ni mwanafunzi wa mwaka wa kwanza wa Shahada ya Udaktari katika Chuo Kikuu cha Kairuki  jijini Dar es salaam.

Alifika ofisini kwa Rais Mstaafu kumsabahi na kumshukuru kwa mchango wake katika kuanzisha na kuimarisha huduma za matibabu ya magonjwa ya moyo nchini.

Dkt. Kikwete alimpongeza Catherine kwa kutimiza ndoto yake ya kusomea udaktari, jambo ambalo aliahidi kulifanya alipokuwa mtoto. Alisema amefurahishwa kumuona akiwa mwenye afya njema na akijiandaa kulitumikia taifa kupitia taaluma ya tiba.

Kwa upande wake, Catherine alisema anatamani kuwa Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo ili kuwasaidia wagonjwa wenye changamoto kama aliyowahi kupitia yeye mwenyewe, akieleza kuwa hiyo itakuwa ni moja ya njia ya kumshukuru Mungu kwa zawadi ya maisha na afya njema.

Wednesday, May 20, 2026

CRDB Bank Yaongeza Ushirikiano na Majeshi Kupitia Mkutano wa Kimataifa.

MONACO - Benki ya CRDB imeendelea kudhihirisha dhamira yake ya kuunga mkono maendeleo ya Taifa kupitia sekta mbalimbali kwa kushiriki katika Mkutano Mkuu wa 81 wa Michezo ya Majeshi Duniani (81st CISM General Assembly) uliofanyika nchini Monaco kuanzia tarehe 1 hadi 9 Mei 2026.

Mkutano huo wa kimataifa uliwakutanisha viongozi wa kijeshi na wadau wa michezo kutoka zaidi ya nchi 130 duniani kwa lengo la kuimarisha mshikamano, diplomasia ya michezo na amani kupitia kaulimbiu ya “Friendship Through Sport.”
Benki ya CRDB, ikiwa miongoni mwa wadau wakubwa wa maendeleo nchini, imeendelea kuunga mkono jitihada za vyombo vya ulinzi na usalama pamoja na michezo ya majeshi, hatua inayoimarisha ushirikiano wake na taasisi za Serikali katika kukuza ustawi wa askari na familia zao.

Ujumbe wa Tanzania katika mkutano huo uliongozwa na Brigedia Jenerali Saidi Hamisi Saidi, akisaidiana na Luteni Kanali Penina Anthony Igwe. Kutoka CRDB, ujumbe unajumuisha Meneja wa Kitengo cha Wateja Maalum, Crispin Sichalwe pamoja na Meneja Mawasiliano na Uhusiano kwa Umma, Emmanuel Tupeligwe.

Akizungumza kwenye mkutano huo, Sichalwe alisema CRDB imeendelea kutoa huduma maalum za kifedha kwa wanajeshi ndani na nje ya nchi, ikiwemo mikopo nafuu, bima na huduma za kifedha zinazowafikia popote walipo.

“Tunatambua mchango mkubwa wa majeshi katika usalama wa Taifa, hivyo tunahakikisha wanapata huduma bora na za haraka kupitia kitengo chetu maalum,” alisema.
Kwa upande wake, Tupeligwe alisisitiza kuwa CRDB itaendelea kushirikiana kwa karibu na Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) kupitia elimu ya fedha na huduma zinazowafikia wanajeshi hata wakiwa katika maeneo ya mbali au majukumu ya kimataifa.

Aidha, benki hiyo imeendelea kuimarisha ushirikiano wake wa kimkakati na JWTZ ili kuhakikisha wanajeshi wanapata huduma bora za kifedha kwa urahisi, ikiwa ni sehemu ya mchango wake katika maendeleo na usalama wa Taifa.

Wednesday, December 31, 2025

SALAMU ZA MWAKA MPYA 2026 KUTOKA KWA MWENYEKITI WA TANZANIA BLOGGERS NETWORK (TBN)


Ndugu Wasomaji na Watumiaji wa Blogu Tanzania.

Tunapouaga mwaka 2025, nachukua fursa hii, kwa niaba ya wanachama wote wa Tanzania Bloggers Network (TBN), kuwapongeza Watanzania wenzangu kwa kumaliza mwaka huu "kibabe". 

Tumekuwa na mwaka wenye matukio mengi ya kihistoria, na ninyi wasomaji wetu mmekuwa wadau muhimu kwa kufuatilia habari, uchambuzi, na taarifa mbalimbali kupitia majukwaa yetu ya kidijitali.

Kuelekea Mwaka 2026: Makubwa Zaidi Yanakuja! Mwaka 2026 unakwenda kuwa mwaka wa mageuzi makubwa kwa TBN. Tunatarajia kuleta maudhui yenye ubunifu wa hali ya juu, habari za kina, na teknolojia ya kisasa zaidi katika kuhabarisha umma. Wanachama wetu wamejipanga kuwa daraja imara zaidi kati ya serikali na wananchi, tukihakikisha kila Mtanzania anapata habari sahihi na kwa wakati.

Ombi Langu kwa Watanzania: Tunapoingia 2026, rai yangu ni kuendelea kudumisha amani na utulivu. Tuepuke vurugu na migawanyiko, badala yake tujikite katika umoja wetu kama Taifa. Huu ni wakati wa kuungana kwa nguvu moja kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 (Vision 2050). Lengo letu ni moja: kuhakikisha kila Mtanzania, kuanzia mjini hadi vijijini, anafaidi "keki ya taifa" na kupata maendeleo ya kweli.

Mwaka 2026 uwe mwaka wa neema, baraka, na mafanikio tele katika kazi na shughuli zenu za kila siku.

Heri ya Mwaka Mpya 2026!

Beda Msimbe

Mwenyekiti, Tanzania Bloggers Network (TBN).