Banner

Banner

FOLLOW US FACEBOOK

propertyfinder.co.tz

Friday, June 12, 2026

DKT. MWIGULU: SERIKALI INATHAMINI MCHANGO WA SEKTA BINAFSI KATIKA KUINUA UBORA WA ELIMU NCHINI

 


Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali itaendelea kuthamini na kuimarisha ushirikiano na sekta binafsi katika sekta ya elimu kutokana na mchango wake mkubwa kwenye kuongeza ubora wa elimu na kuandaa rasilimali watu yenye maarifa, ujuzi na maadili yanayohitajika katika maendeleo ya Taifa.

Dkt. Mwigulu amesema hayo alipokuwa Mgeni Rasmi katika Mahafali ya 11 ya wahitimu wa Kidato cha Nne (Year 11–IGCSE) wa mwaka wa masomo 2025/2026 ya Shule ya Kimataifa ya Feza yaliyofanyika Salasala, Dar es Salaam, leo Ijumaa, Juni 12, 2026.

"Nimekuja leo kwa kuwa Serikali inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, inatambua ubia huu muhimu ambao shule yenu imekuwa ikifanya katika sekta ya elimu. Hatuwezi kuyataja mafanikio katika sekta ya elimu bila kutaja mchango wa shule za sekta binafsi, na kwa umuhususi shule za Feza," amesema Dkt. Mwigulu.

Amesema Taasisi ya Feza ni miongoni mwa taasisi zilizochangia kwa kiasi kikubwa mageuzi ya elimu nchini kwa kuweka viwango vya juu vya ubora wa elimu vinavyotambulika ndani na nje ya Tanzania.

"Hatungeweza kutaja mabadiliko na mageuzi makubwa yaliyofanyika katika sekta ya elimu bila kutaja mchango wa shule za Feza. Mmekuwa chachu ya mageuzi makubwa yaliyofanyika katika sekta ya elimu," amesema.

Aidha, Waziri Mkuu ameipongeza Taasisi ya Feza kwa kuendelea kuvutia wanafunzi kutoka mataifa mbalimbali duniani, hatua inayoonesha kiwango cha ubora wa elimu inayotolewa na taasisi hiyo.

"Sina shaka nyote mtakubaliana nami kuwa viwango vya ubora wa shule hizi vimekuwa chachu ya kuvutia wanafunzi kutoka mataifa mbalimbali ikiwemo India, Uturuki, China, Falme za Kiarabu, Lebanon, Somalia, Marekani na nchi nyingine," amesema.

Waziri Mkuu amesema Serikali inaendelea kutekeleza mageuzi mbalimbali katika sekta ya elimu ili kuhakikisha mfumo wa elimu unaendana na mahitaji ya sasa ya dunia pamoja na maendeleo ya sayansi na teknolojia.

Amesema mojawapo ya hatua hizo ni utekelezaji wa Sera ya Elimu na Mafunzo ya Mwaka 2014, Toleo la 2023, inayolenga kuimarisha upatikanaji wa elimu bora na kufanya elimu ya lazima kuwa ya miaka 10.

"Tumeyafanya mageuzi haya kwa kuzingatia mabadiliko makubwa yanayotokea duniani na kwa lengo la kuwaandaa vijana wa Kitanzania kukabiliana na changamoto na fursa za dunia ya sasa," amesema.

Sambamba na hilo, Dkt. Mwigulu ameipongeza Taasisi ya Feza kwa mchango wake katika utekelezaji wa miradi ya uwajibikaji kwa jamii ikiwemo kusaidia wanafunzi wenye uhitaji, kuboresha miundombinu ya shule za umma na kuchimba visima vya maji katika maeneo mbalimbali nchini.

Akizungumzia nafasi ya elimu katika maendeleo ya Taifa, Waziri Mkuu amesema uwekezaji katika rasilimali watu ndiyo msingi wa maendeleo endelevu ya nchi yoyote duniani.

"Hakuna nchi yoyote iliyowahi kuendelea bila kuwekeza katika rasilimali watu ya kiwango cha juu. Hizi rasilimali nyingine zinaweza zisiwepo, lakini ukiwa na watu wenye maarifa, ujuzi na maadili unaweza kujenga Taifa lenye maendeleo makubwa," amesema.

Aidha, amewataka wahitimu kuendelea kuwa na nidhamu, kutumia maarifa waliyojifunza kwa manufaa ya jamii na Taifa, pamoja na kutumia mitandao ya kijamii kwa tija.

"Mkawe mabalozi wazuri wa mafunzo mliyoyapata hapa. Mafanikio ya kweli hayatapimwa kwa matokeo ya mitihani pekee, bali kwa aina ya watu mtakaokuwa baada ya hapa," amesema.

RAIS SAMIA AONGOZA MAADHIMISHO YA MIAKA 60 YA BENKI KUU YA TANZANIA




Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameshiriki Maadhimisho ya Miaka 60 ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT) yaliyofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam tarehe 12 Juni, 2026.

Maadhimisho hayo yamekuwa fursa ya kutafakari mchango mkubwa wa Benki Kuu katika kusimamia uthabiti wa uchumi, mfumo wa fedha na maendeleo ya sekta ya kifedha nchini kwa kipindi cha miongo sita.

Katika kipindi cha miaka 60, Benki Kuu ya Tanzania imeendelea kuwa nguzo muhimu katika kuimarisha uchumi wa taifa, kudhibiti mfumuko wa bei, kusimamia sera za fedha na kuimarisha mazingira ya uwekezaji yanayochochea ukuaji wa uchumi na maendeleo ya wananchi.

Ushiriki wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika maadhimisho hayo unaonesha dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita ya kuendelea kuimarisha sekta ya fedha na kujenga uchumi imara, shindani na jumuishi kwa manufaa ya Watanzania wote.

Thursday, June 11, 2026

NDG RABIA KUZUNGUMZA NA MAKUNDI MBALIMBALI YA KIJAMII, TAASISI, NGO’s NA VYAMA MBALIMBALI VYA KIJAMII

Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa Idara ya Mambo ya Siasa na Uhusiano wa Kimataifa-SUKI Ndg Rabia Abdalla Hamid anatarajia kufanya ziara ya kuzungumza na Makundi mbalimbali ya Kijamii, Taasisi, NGO’s na vyama vya kijamii katika mikoa ya Lindi, Mtwara, Ruvuma na Njombe, kama ifuatavyo;

1. Tarehe 14/06/2026 Lindi

2. ⁠Tarehe 15/06/2026 Mtwara

3. ⁠Tarehe 17/06/2026 Ruvuma

4. ⁠Tarehe 18/06/2026 Njombe

Makundi ya kijamii ya wakulima, wafugaji, wachimbaji wa madini, wavuvi, wenye mahitaji Maalum, wanavyuo, Vyama vya ushirika, Wajane, Mama Lishe na Baba lishe, Maafisa Usafirishaji (Bodaboda, bajaji, daladala, maguta), vikundi mbalimbali vya wajasiliamali nyote mnakaribishwa kusema changamoto mbalimbali zinazowakabili, CCM ndio kimbilio la Makundi yote ya kijamii, Ndg Rabia Abdalla Hamid atakusikiliza na kutatua kero inayokabili kikundi chochote cha jamii katika jamii.

Aidha, Mwenyekiti wa CCM na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amedhamiria kuacha Tabasamu kwa kila Mtanzania.

SERIKALI YAPUNGUZA KODI KUCHOCHEA MATUMIZI YA NISHATI SAFI YA KUPIKIA

 


Serikali imependekeza hatua mbalimbali za kikodi zitakazolenga kuongeza matumizi ya nishati safi ya kupikia na kuharakisha matumizi ya teknolojia rafiki kwa mazingira nchini katika mwaka wa fedha 2026/2027.

Hatua hizo zimetangazwa leo Juni 11, 2026 bungeni jijini Dodoma na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar, wakati akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2026/2027.

Miongoni mwa mapendekezo hayo, Serikali imependekeza kusamehe Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) kwenye mita janja za gesi ya mitungi ya kupikia (LPG Smart Meter) zinazoingizwa nchini ili kuongeza upatikanaji na matumizi ya nishati safi ya kupikia katika ngazi ya kaya.

Aidha, Serikali imependekeza kuendelea kutoa vivutio mbalimbali vya kikodi katika sekta ya gesi na umeme ikiwemo msamaha wa kodi kwenye vifaa vinavyotumika kubadilisha magari kutoka mfumo wa matumizi ya mafuta kwenda matumizi ya gesi na umeme pamoja na vifaa vya miundombinu ya gesi.

Waziri Omar amesema hatua hizo ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kuhamasisha matumizi ya nishati safi na mbadala nchini huku ikipunguza utegemezi wa mafuta yanayoagizwa kutoka nje ya nchi.

Katika hatua nyingine, Serikali imependekeza kupunguza ushuru wa forodha kutoka asilimia 25 hadi asilimia 10 kwa baadhi ya magari yanayotumia umeme pamoja na kusamehe kodi kwenye vifaa vinavyotumika katika vituo vya kuchaji magari hayo.

Hatua hizo zinatarajiwa kuongeza matumizi ya nishati safi katika sekta ya usafiri na majumbani, kupunguza gharama za matumizi ya nishati kwa wananchi na kuchangia juhudi za kuhifadhi mazingira sambamba na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.

TMDA YAIHAKIKISHIA KAMATI YA BUNGE UDHIBITI WA DAWA FEKI NA DUNI NCHINI


Na Shaban Juma, Dodoma

Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba Tanzania (TMDA) imeihakikishia Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Afya na Masuala ya UKIMWI juu ya kuendelea kuimarisha udhibiti wa dawa feki na duni nchini kwa lengo la kulinda afya za wananchi na kuboresha utoaji wa huduma za afya.

Hayo yameelezwa na Naibu Waziri wa Afya, Dkt. Florence Samizi, wakati wa ziara ya mafunzo ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Afya na Masuala ya UKIMWI iliyofanyika leo Juni 10, 2026, kwa lengo la kujifunza huduma zinazotolewa na TMDA chini ya usimamizi wa Wizara ya Afya.

Dkt. Samizi amesema Serikali imeendelea kuwekeza vya kutosha katika rasilimali mbalimbali ikiwemo vifaa vya kisasa, mifumo ya uchunguzi pamoja na wataalamu ili kubaini dawa duni na feki kabla hazijaleta madhara kwa wananchi.

Amesema uwekezaji huo umeiwezesha TMDA kuimarisha uwezo wa udhibiti wa ubora wa dawa na vifaa tiba vinavyoingia na vinavyotumika nchini, hatua inayosaidia kuhakikisha wananchi wanapata dawa salama, bora na zenye ufanisi.

“Serikali itaendelea kuimarisha mifumo ya udhibiti wa dawa na vifaa tiba ili kuhakikisha afya na usalama wa Watanzania vinaendelea kulindwa,” amesema Dkt. Samizi.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Afya na Masuala ya UKIMWI, Dkt. Johannes Lukumay, ameipongeza TMDA kwa kazi kubwa ya kusimamia ubora wa dawa na vifaa tiba nchini.

Aidha, ameishauri Serikali kuendelea kuwekeza zaidi katika rasilimali mbalimbali zitakazowezesha kubaini kwa ufanisi dawa duni na feki pamoja na vifaa tiba visivyo salama, ili kuimarisha ulinzi wa afya za Watanzania.

Amesema jitihada hizo zitasaidia kuongeza imani ya wananchi katika mfumo wa afya na kuhakikisha bidhaa za afya zinazotumika nchini zinakidhi viwango vinavyotakiwa.


Wednesday, June 10, 2026

SERIKALI ITAENDELEA KUBORESHA MAZINGIRA YA UWEKEZAJI – DKT. MWIGULU

 

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali itaendelea kuondoa vikwazo na kuimarisha ushirikiano na sekta binafsi ili kuboresha mazingira ya uwekezaji nchini.

Ameyasema hayo leo (Jumatano, Juni 10, 2026), wakati akizindua ghala la forodha la kampuni ya Ciwaye Trading Co. Ltd Wilayani Chamwino mkoani Dodoma.

“Kama tunavyoheshimu sekta ya umma, tunatakiwa kuheshimu sekta binafsi kwa uzito ule ule, kama mataifa mengine yaliyoendelea, uchumi wa mataifa hayo nguzo yake ni sekta binafsi.”

Dkt. Mwigulu aliongeza kwa kusema “Kwa kuheshimu hilo, nimeona nije kuzindua mradi huu, kama ambavyo nimepita kwenye ziara kuzindua miradi ya Serikali, ndiyo maana nimeona na hapa nije mwenyewe.”

Aidha, ameeleza kuwa mradi huo una umuhimu mkubwa katika maendeleo ya nchi, hivyo hauna budi kulelewa.

“Ukubwa wa jambo hili haupimwi kwa majengo, bali kwa uthubutu na matokeo yanayoakisi Dira yetu ya maendeleo na maono ya Rais wetu ya kuhakikisha mradi kama huu unatoa matokeo yaliyokusudiwa.” Amesisitiza Waziri Mkuu Mwigulu.

Waziri Mkuu ameongeza kuwa mradi huo unatazamwa na Serikali kama mradi wa kielelezo wa kutekeleza Dira 2050 na ndiyo maana Serikali imekuwa ikiboresha mazingira ya uwekezaji nchini, ikiwemo maboresho ya sheria za uwekezaji.

“Zimebadilishwa Sheria za uwekezaji ili kuhakikisha wazawa wananufaika na kuushika uchumi, zamani vivutio vya uwekezaji viliwanufaisha wageni, lakini sasa wazawa wanapata vivutio hivyo,” ameeleza Waziri Mkuu.

Ameongeza kuwa: “Mfano katika sekta ya uzalishaji, zamani miradi yote mikubwa ilikuwa inatekelezwa na wageni, lakini mabadiliko hayo ya sheria yamewezesha wazawa kutekeleza miradi mikubwa, na sasa wanaweza kuajiri wageni katika utekelezaji wa miradi hiyo.”

Waziri Mkuu Mwigulu amesema mkakati mwingine unaoenda sambamba na mabadiliko ya sheria, ni pamoja na kuondoa zaidi ya tozo 270 ili kuwapunguzia mzigo wafanyabiashara na walaji wa mwisho.

Akizungumzia utekelezaji wa mradi huo, Waziri Mkuu ameeleza kufurahishwa na hatua zilizofikiwa katika utekelezaji wake, kwani umetekelezwa ndani ya muda mfupi lakini viwango vya ubora vimezingatiwa.

Amesema uamuzi wa kuanzisha ghala hilo mkoani Dodoma ni wa kimkakati kwani Dodoma ipo katikati ya nchi, ikiunganisha maeneo mengine ya nchi na fursa zilizopo katika maeneo hayo, ambapo amewataka wafanyakazi wa mradi huo kuwa waaminifu ili mradi uwe na faida endelevu, kwao binafsi na jamii.

Pia Waziri Mkuu Mwigulu amewahimiza Wakuu wa Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kuhamasisha wawekezaji kuwekeza kwenye mikoa na maeneo yao kwa kuweka miundombinu inayochochea vyanzo vya mapato na kukua kwa uchumi.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu Mwigulu ameuagiza Wakala wa Barabara za Mijini na Vijini (TARURA) kukaa kwa haraka na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) na kufanya tathmini ya ujenzi wa barabara ya kiwango cha lami ya kilometa 25 kuanzia Chamwino kwenda kituo cha treni cha Igandu ili kusaidia ufanisi wa ghala lililojengwa kwani barabara hiyo itaunufaisha mradi huo.

Kwa upande wake Meneja Masoko wa ghala hilo, Leroy Nelson amesema mradi huo umegharimu zaidi ya shilingi bilioni tatu ambapo utekelezaji wake umekamilika kwa asilimia 100.

Tuesday, June 9, 2026

Mkuu Wa Wilaya ya Lindi, Mhe. Victoria Mwanziva Amechaguliwa Kuiwakilisha Tanzania Katika Programu Mahususi ya Uongozi Kwa Wanawake


Mkuu wa Wilaya ya Lindi, Mhe. Victoria Mwanziva amechaguliwa kuiwakilisha Tanzania katika programu mahususi ya Uongozi kwa Wanawake inayoongozwa na Rais Mstaafu wa Liberia, Ellen Johnson Sirleaf.

Programu hiyo inajulikana kama “Amujee Leadership Initiative” ikiwa chini ya Ellen Johnson Sirleaf Presidential Centre for Women and Development- EJS Centre inaungana na Wanawake Viongozi wengine waliopata fursa na heshima ya kushiriki.

Viongozi wengine ni Waziri wa Afya na Maendeleo ya Jamii Namibia, Dkt. Esperance Luvindao, Waziri wa Mazingira wa Guinea, Djami Diallo, Wabunge mbalimbali akiwemo Anta Diack wa Senegal na Dkt. Anneline Chetty ambaye ni Mtendaji Mkuu wa Kituo cha Biashara, Viwanda na Uwekezaji Afrika Kusini.

Kwa mujibu wa taarifa, Victoria ni miongoni mwa Wanawake 15 walioteuliwa barani Afrika baada ya mchujo mkali uliovutia zaidi ya waombaji 600. Uteuzi wake umetokana na mchango wake katika Uongozi wa Jamii, hususan kazi za maendeleo Vijijini na uwezeshaji wa Vijana kupitia nafasi yake ya Uongozi wa Wilaya.

Programu hii inalenga kukuza ushirikiano wa Viongozi Wanawake barani Afrika na kuimarisha ajenda za maendeleo jumuishi, huku ikitarajiwa kuongeza fursa za ushirikiano kati ya Mataifa ya Afrika.