Banner

Banner

FOLLOW US FACEBOOK

propertyfinder.co.tz

Monday, June 8, 2026

Makubaliano Nane ya Kimkakati: Ramani Mpya ya Ushirikiano wa Kiuchumi Kati ya Tanzania na Urusi Yafunuliwa

 


Na Mwandishi Wetu, TBN, Dar es salaam

Mikataba na hati za makubaliano manane (8) zilizosainiwa kati ya Tanzania na Urusi, ndizo zilizoweka msingi mkuu wa ushirikiano mpya wa kiuchumi, kijamii na kiteknolojia unaotarajiwa kupandisha hadhi ya nchi hizi mbili. 

Makubaliano haya makubwa, ambayo ni matunda ya moja kwa moja ya ziara ya kihistoria ya Rais Samia Suluhu Hassan nchini Urusi, yanajenga daraja imara la maendeleo katika sekta tisa za kipaumbele: kilimo, elimu, nishati, madini, viwanda, utalii, usafirishaji, uchumi wa kidijiti, pamoja na biashara na uwekezaji.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo, ameanika hadharani undani wa makubaliano hayo manane yanayobeba mustakabali wa nchi:

Kutoka Diplomasia ya Lugha Hadi Mapinduzi ya Afya na Elimu ya Juu

Katika makubaliano ya kwanza, Tanzania na Urusi zimeamua kutumia lugha kama silaha ya kidiplomasia. Kupitia hati ya ushirikiano kati ya Baraza la Kiswahili la Taifa (BAKITA) na Chuo Kikuu cha Mahusiano ya Kimataifa cha Urusi (MGIMO), lugha ya Kiswahili itazidishwa kasi ya kufundishwa nchini Urusi, huku Tanzania nayo ikijipanga kuanza kufundisha Kirusi kupitia Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM).

Makubaliano ya pili yamejikita kwenye sekta ya afya, ambapo Chuo Kikuu cha Muhimbili (MUHAS) kimeingia ubia na taasisi mbili za afya za Urusi kwa ajili ya kubadilishana utaalamu wa matibabu na kuongeza nguvu katika uzalishaji wa dawa nchini.

Kwenye upande wa elimu, makubaliano ya tatu na ya nne yanakuja kutatua changamoto za ajira na teknolojia ya kisasa:

Wizara za Elimu za nchi zote mbili zimesaini makubaliano ya kutambua vyeti na tuzo za kitaaluma zinazotolewa Urusi, hatua itakayowawezesha Watanzania waliosoma nchini humo kupata ajira kwa urahisi nyumbani.

Taasisi ya Teknolojia ya Dar es Salaam (DIT) imesaini mkataba na Chuo cha Urafiki  cha Urusi kuanzisha programu za pamoja za Shahada ya Kwanza na Uzamili katika fani za kisasa kabisa duniani—ikiwemo Sayansi ya Takwimu, Mfumo wa Anga, Akili Unde (AI), na Ujifunzaji wa Mashine (Machine Learning).

Kuvutia Mitaji ya Magharibi, Siri za Nishati na Ajira za Vijana

Makubaliano ya tano na ya sita yanalenga kufungua milango ya mitaji mikubwa. Kupitia Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalumu ya Kiuchumi Tanzania (TISEZA), nchi imepewa fursa ya kuhamasisha uwekezaji hadi kuelekea mataifa ya Ulaya. 

Zaidi ya hapo, Tanzania imeingia ushirikiano na Kampuni ya Roscongress ya Urusi—miamba ya kuandaa makongamano ya kimataifa—kwa lengo la kutengeneza miradi ya ubia na kuvutia wawekezaji sio tu kutoka Urusi, bali pia kutoka nchi za Magharibi.

Mkataba wa saba uligusa sekta nyeti ya nishati, ambapo Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) na Kampuni ya Mantra Tanzania Ltd (Kmapuni tanzu ya Shirika la Nyuklia la Urusi, Rosatom) zimesaini makubaliano ya kulinda na kutunza siri za taarifa za kimkakati katika miradi ya nishati.

Kama kilele cha makubaliano hayo, kubaliano la nane ni mpango kabambe wa miaka mitano unaolenga kukuza uchumi na kuzalisha fursa za ajira kwa vijana wa Kitanzania nchini Urusi.

"Haya ni matunda halisi ya kiuchumi yaliyotokana na maono ya mheshimiwa Rais," alisisitiza Profesa Kitila Mkumbo, akibainisha kuwa utekelezaji wa makubaliano haya unaenda kuweka alama ya kudumu katika soko la ajira na uwekezaji nchini.

Dakika Tatu za Dhahabu za Rais Samia Urusi Zafungua Milango ya Shilingi Trilioni 5

Na Mwandishi Wetu, TBN, Dar es salaam

Ziara ya kihistoria ya Rais Samia Suluhu Hassan nchini Urusi imeendelea kuzaa matunda makubwa baada ya Serikali kutangaza kuwa kampuni kubwa za nchi hiyo zimeonesha nia thabiti ya kuwekeza kiasi cha Dola za Marekani bilioni mbili (sawa na Shilingi za Kitanzania trilioni tano) ndani ya miaka mitatu ijayo. 

Uwekezaji huu mkubwa unalenga kimkakati sekta tano kuu za kipaumbele, huku ukichangiwa kwa kiasi kikubwa na ushawishi wa kipekee wa Rais Samia kiuchumi.

Akitolea ufafanuzi mafanikio hayo, Mkurugenzi wa Biashara ya Kimataifa na Diplomasia ya Uchumi kutoka Wizara ya Mambo ya Nje, Balozi John Ulanga, alifichua siri ya mafanikio hayo kuwa ni "dakika tatu za dhahabu" alizopewa Rais Samia kuzungumza katika Jukwaa la Uchumi la Kimataifa la Petersburg nchini Urusi. 

Kupitia ubunifu na maono yake makubwa, Rais alitumia muda huo mfupi kwa umahiri mkubwa kutangaza fursa za Tanzania, hatua iliyoziteka akili za miamba ya biashara nchini Urusi na kuamsha hamu kubwa ya kuwekeza nchini.

Miamba ya Nishati na Madini Kuja kwa Kasi

Katika sekta ya madini na nishati, Urusi tayari imeweka mguu wake nchini kupitia Shirika lake la Nishati ya Atomiki la Serikali (ROSATOM), ambalo limewekeza Dola bilioni 1.2 katika mradi wa kimkakati wa madini ya Urani, Nickel na madini mengine. Kasi hii inatarajiwa kuongezeka kufuatia ziara hiyo, kwani kampuni nyingi zaidi zilizotembelea banda la Tanzania zimeonesha nia ya kuja kuwekeza.

Sambamba na hilo, kampuni kubwa ya nishati duniani, Gazprom, inayomiliki soko kubwa la gesi asilia Ulaya Magharibi, imeingia kwenye mazungumzo na Tanzania ikieleza nia yake thabiti ya kushirikiana na kuwekeza katika sekta ya gesi nchini.

Mapinduzi ya Chanjo, Kilimo cha Kisasa na Tehama

Sekta ya afya na dawa nayo inatarajiwa kushuhudia mapinduzi makubwa. Kampuni za Urusi zilizotangulia kuwekeza nchini katika uzalishaji wa chanjo zimebainisha kuwa, ndani ya miaka mitano ijayo, zikishirikiana na makampuni mengine ya Urusi, zitakuwa na uwezo wa kuzalisha chanjo milioni 20 za magonjwa mbalimbali nchini Tanzania.

Kwenye kilimo na uongezaji thamani, makubaliano yamejikita katika kilimo endelevu kinachotunza mazingira na ununuzi wa bidhaa za Tanzania kama kahawa, korosho na chai kwa ajili ya soko la Urusi. Tayari wafanyabiashara zaidi ya 50 wa Kitanzania waliokuwa Urusi wameingia makubaliano ya kuleta mbolea, vinywaji vikali, na kuuza mazao yetu huko. Katika Tehama, taasisi za sayansi za Urusi ziko tayari kuja nchini kukuza uchumi wa kidijiti kwa kufundisha teknolojia hii kuanzia shuleni hadi vyuoni.

Angani Kufunguka: ATCL Kuanza Safari za Moja kwa Moja Moscow

Kama kilele cha mafanikio ya ziara hiyo, sekta ya utalii inatarajiwa kulipuka kwa mafanikio kufuatia tangazo la kihistoria kuwa Shirika la Ndege la Tanzania (ATCL) litaanza safari za moja kwa moja kati ya Dar es Salaam na Moscow ifikapo Julai 2, mwaka huu.

"Tuliona mtiririko mkubwa wa kampuni za waongoza utalii kutoka Urusi wakivutiwa na tangazo hili. Moja ya vitu vinavyovutia watalii ni upatikanaji wa usafiri wa uhakika, wa moja kwa moja na rahisi zaidi," alisisitiza Balozi Ulanga.

Hatua hii ya ATCL si tu kwamba inarahisisha usafiri, bali inafungua njia ya moja kwa moja kwa maelfu ya watalii na wawekezaji kutoka Urusi kumiminika nchini, ikithibitisha nguvu ya diplomasia ya uchumi inayotekelezwa na Serikali ya Awamu ya Sita.

Jinsi Ziara ya Rais Samia Nchini Urusi Ilivyoteka Fikira za Kidiplomasia Duniani



Na Mwandishi Wetu, TBN, Dar es salaam

Katika ulimwengu wa diplomasia ya kimataifa, kuna matukio yanayobadilisha mwelekeo wa upepo wa kiuchumi, na ziara ya Rais Samia Suluhu Hassan nchini Urusi imeandikwa kama mojawapo ya matukio hayo. 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mahmoud Thabit Kombo, amebainisha kuwa safari hiyo ya kihistoria kuanzia Juni 3 hadi 5, mwaka huu, imeleta "mtikisiko chanya" kote duniani, ikionyesha nafasi ya kipekee ya Tanzania kama lango kuu la bara la Afrika.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Balozi Kombo alifafanua kuwa mshtuko huu wa kidiplomasia unatokana na ukweli kwamba, hakuna nchi nyingine ya Afrika iliyowahi kufanya ziara ya kimkakati ya namna hiyo nchini Urusi katika muktadha wa sasa.

"Dunia nzima ina watu bilioni 7.5; Urusi anafanya biashara na watu bilioni 6. Ni bilioni 1.5 tu ndio waliomwekea vikwazo. Katika kutanua uchumi wake Afrika, Urusi inaiangalia Tanzania kama kiungo muhimu zaidi," alieleza Balozi Kombo.


Tanzania Kama Lango Kuu la Kimkakati Afrika

Kwanini dunia imetikisika? Jibu liko kwenye jiografia ya kiuchumi ya Tanzania. Balozi Kombo alieleza kuwa Urusi inaitazama Afrika kupitia kanda nne kuu, lakini Tanzania inasimama kama nchi ya pekee yenye uwezo wa kufungua milango ya soko la nchi zote saba za Afrika Mashariki (EAC) na nchi 16 za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC). Kupitia ushawishi wa Rais Samia, Tanzania imekuwa daraja linaloiunganisha Urusi na soko la Waafrika bilioni 1.2.


Ziara hii inabeba uzito mkubwa wa kihistoria, kwani ni ziara ya pili tu ya Mkuu wa Nchi wa Tanzania kutembelea Urusi tangu nchi hiyo ipate uhuru, ikitenganishwa na miaka 57 tangu Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, alipofanya ziara kama hiyo Oktoba 11, 1969.


Kutoka Dola Milioni 70 Hadi Milioni 500: Mapinduzi ya Biashara na Fursa za Vijana

Mkakati wa Rais Samia nchini Urusi haukuwa tu wa kisiasa, bali ulijikita katika kuleta mabadiliko ya mfukoni kwa Mtanzania. Serikali imeweka lengo kubwa la kukuza mauzo ya bidhaa za ndani kwenda Urusi kutoka Dola za Marekani milioni 70 za sasa hadi kufikia Dola milioni 500 (zaidi ya Shilingi trilioni 1.3) ndani ya miaka mitano ijayo. Juhudi za kuwaunganisha wazalishaji wa ndani na wafanyabiashara wa Urusi zimeshaanza nchini.

Mbali na biashara, ziara hiyo imefungua milango mipya kwa vijana wa Kitanzania katika maeneo yafuatayo:

Ajira: Serikali imeomba rasmi nafasi 500 za masomo kwa ajili ya vijana wa Kitanzania nchini Urusi, huku kampeni ya kuongeza fursa hizo ikiendelea.

Elimu Nafuu: Kumefanyika mazungumzo na vyuo vikuu vya umma na binafsi vya Urusi ili kuwapa wanafunzi wa Kitanzania nafasi ya kusoma shahada mbalimbali kwa gharama nafuu ya Dola 5,000 tu kwa mwaka—gharama ambayo ni ndogo ukilinganisha na nchi nyingine zilizoendelea.

Mtikisiko huu chanya ulioripotiwa na Balozi Kombo unathibitisha namna Tanzania inavyoendelea kuchanja mbuga kimataifa, ikijitofautisha kama nchi inayojua kutumia fursa za kijiografia na kidiplomasia kwa maslahi ya kiuchumi ya watu wake.

Saturday, June 6, 2026

PUTIN AIKUBALI TANZANIAtin NA KUELEZEA JINSI ILIVYO MUHIMU

 


Na Beda Msimbe, TBN, Petersburg

Rais Vladimir Putin wa Urusi amesema Tanzania ni lango kuu la kimkakati linalounganisha soko la Afrika Mashariki na masoko ya kimataifa.

Aidha amesema katika uchumi wa dunia unaozidi kubadilika kuelekea mifumo ya nguzo nyingi za kiuchumi, taifa la Tanzania umuhimu  mkubwa katika kuyfanikisha ustawi wa jamii mbalimbalio. 

Akizungumza Juni 5 katika Jukwaa la Kimataifa la Uchumi la St. Petersburg la mwaka 2026 Rais Putin amesema kuwa Tanzania katika utendaji ni taifa la kimkakati  katika ukanda wa Afrika Mashariki unaofanana na ule wa nchi ya Uzbekistan katika ukanda wa Asia ya Kati ikifanya kazi kama kiungo muhimu sana kati ya uchumi wa kikanda na vituo vikuu vya biashara ya kimataifa duniani. 

Kiongozi huyo amebainisha hayo wakati akizungumzia mataifa ambayo kutokana na nafasi zao za kijiografia na mahusiano yao ya kiuchumi yanageuka kuwa madaraja muhimu kati ya kanda tofauti duniani na kuongeza kuwa mataifa yenye uwezo wa kuoanisha maendeleo yao ya ndani na miunganisho madhubuti kwenye vituo vipya vya ukuaji wa uchumi wa kimataifa yanazidi kuwa muhimu wakati mifumo ya biashara ya kimataifa inavyoendelea kubadilika.

Kauli hizi nzito kutoka kwa Rais Putin zinakuja wakati ambao Tanzania inaendelea kupanua kwa kasi miundombinu yake ya usafirishaji ikiwemo bandari na njia za biashara za kikanda ili kuimarisha nafasi yake kama kitovu kikuu cha biashara kwa ukanda mzima wa Afrika Mashariki na Kati na hivyo kutafsiri kwa vitendo malengo makubwa ya ukuaji wa kiuchumi.

Rais Samia Suluhu Hassana alishiriki katika jukwaa hilo amnbapo alipata nafasi ya kuelezea mambo mbalimbali yanayohusiana na uwekezaji na pia biashara.

Aidha alisema kwamba Tanzania ipo tayari kushirikiana na mataifa yoyote ikiwamo Russia ili kupeleka fursa mbalimbali za maendeleo kwa wananchi wake. Akijibu swali kwamba Russia ina vikwazo, Rais Samia alisema Tanzania haina vikwazo inafanyakazi na washirika wote wanaoitakia mema nchi yake.

mwisho

RAIS SAMIA AWASILI NCHINI AKITOKEA ZIARA YA MAFANIKIO URUSI

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na Makamu wa Rais Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel John Nchimbi pamoja na Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Balozi Dkt. Asha-Rose Migiro mara baada ya kuwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere tarehe 06 Juni, 2026 baada ya kuhitimisha Ziara yake ya Kitaifa, St. Petersburg nchini Urusi tarehe 05 Juni, 2026 kufuatia mwaliko wa Rais wa Nchi hiyo Mhe. Vladmir Putin.







Samia Suluhu Hassan akisalimiana na viongozi mbalimbali baada ya kuwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere tarehe 06 Juni, 2026 baada ya kuhitimisha Ziara yake ya Kitaifa, St. Petersburg nchini Urusi tarehe 05 Juni, 2026

RAIS SAMIA SULUHU HASSAN ATANGAZA UTALII ALIPANIA SOKO LA URUSI

 

Na Beda Msimbe,TBN, Petersburg, Urusi

Ushirikiano wa miaka 65 ya kidiplomasia kati ya Tanzania na Urusi sasa unatafsiriwa kuwa daraja imara la maendeleo ya kiuchumi na kijamii, huku sekta ya utalii ikichukua mwelekeo mpya wa kimkakati kuvutia masoko ya kimataifa likiwemo la Urusi. 

Alisema anatambua soko la Urusi ni kubwa naTanzania ipo tayari kulihudumia kwa kuondoa vikwazo kadhaa ikiwamo kuwezesha kupatikana kwa safari za moja kwa moja kutoka Moscow hadi Dar es Salaam na Zanzibar.

Rais alisema hayo wakati akihutubia wawakilishi kutoka nchi 130 duniani zilizoshiriki mkutano wa kiuchumi wa kimkataifa wa Petersburg Juni 5, 2026.

Katika jukwaa hilo la kiuchumi, Rais  Samia  alitangaza kuwa kuanzia Julai 2 mwaka huu, Shirika la Ndege la Tanzania, Air Tanzania, litaanza safari za moja kwa moja kati ya Dar es Salaam, Moscow, na Zanzibar kwa lengo la kuongeza idadi ya watalii hadi kufikia laki tano ifikapo mwaka 2030 na hatimaye milioni moja. 

Hatua hii inaenda sambamba na ushindi wa tuzo za kimataifa ambapo hifadhi ya Serengeti imetajwa kuwa bora zaidi Afrika na Zanzibar kupewa tuzo kama eneo bora la mikutano na mapumziko. 

Rais Samia alihitimisha kwa kutoa rai kuwa dunia inabadilika kwa kasi kubwa na nchi za Afrika ziko tayari kukua kupitia mifumo yao kama soko huru la Afrika, akisisitiza kuwa Tanzania imefungua milango yote kwa wabunifu na wafanyabiashara wanaotaka kushiriki katika safari hii mpya ya mabadiliko.

mwisho

Friday, June 5, 2026

RAIS WA JMT. DKT. SAMIA SULUHU HASSAN AHITIMISHA ZIARA YAKE URUSI KWA KUINADI TANZANIA KATIKA JUKWAA LA BIASHARA ST. PETERSBURG




Na Beda Msimbe, TBN, St Petersburg
                
Rais Samia Suluhu Hassan leo anahitimisha ziara yake nchini Urusi kwa kushiriki katika kongamano la kibiashara kati ya Tanzania na Urusi sanjari na Jukwaa la Kimataifa la Biashara la St Petersburg.                     
Katika jukwaa hilo Rais Samia anatarajiwa kuinadi Tanzania katika sekta za uwekezaji na biashara.   
          
Ziara ya Rais Samia imekuwa na mafanikio makubwa hasa hakikisho la ushiriano wa karibu na Urusi katika nyanja mbalimbali ikiwemo elimu ya uendelezaji wa rasilimaliwatu na ukuzaji wa teknolojia.  

Ziara hiyo katika taifa lenye nguvu kubwa kiteknolojia, uchakataji na uzalishaji kwenye kilimo au viwandani imekuja wakati Tanzania inajiandaa kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050 inayolenga kulifanya taifa kuwa na pato la dola trilioni moja kwa mwaka.                       
Kwa sasa serikali imesema Pato la Taifa kwa mwaka 2025 lilikua kwa wastani wa asilimia 5.9 ikilinganishwa na asilimia 5.5 mwaka 2024 kauli ilitolewa na Waziri wa Fedha, Balozi Khamis Mussa Omar wakati akiwasilisha Mapitio ya Utekelezaji na Mpango wa Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2025/2026 na Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027 bungeni Dodoma hivi karibuni.

Balozi Omar alisema ukuaji huo ulichangiwa na kuongezeka kwa mikopo kwa sekta binafsi, kuimarika kwa miundombinu ya usafiri na usafirishaji na kuimarika kwa shughuli za kilimo.

Alitaja sababu nyingine ni kuongezeka kwa uzalishaji wa madini na shughuli za ujenzi wa umma na binafsi na utekelezaji wa miradi ya kimkakati, hususani katika sekta za nishati, usafirishaji na huduma za jamii. 

Mwisho.