Banner

Banner

FOLLOW US FACEBOOK

propertyfinder.co.tz

Monday, August 20, 2012

BAADA YA KUBEBA UJAUZITO KWA MIAKA MITATU AJIFUNGUA MTOTO ASIYEKUWA WA KAWAIDA...!

Msichana mkazi wa kijiji cha Mpasa mwambao mwa Ziwa Tanganyika wilayani Nkasi mkoani Rukwa amejifungua mtoto asiye wa kawaida baada ya ujauzito wa zaidi ya miaka mitatu.

Mtoto aliyekuwa kivutio na gumzo kijijini hapo na kwingineko, alizaliwa Agosti mosi, akiwa na meno 32 ambayo ni idadi ya mtu mzima na nywele zenye mvi utosini huku mzazi Lucia Sabastiano (18) akidai kuwa hakuwahi kukutana kimwili na mwanamume yeyote maishani mwake.

Mtoto huyo ambaye alifariki dunia baada ya siku mbili, alikuwa wa kiume, huku pia akiwa na sehemu za siri zilizokomaa kama za mtu mzima ambazo zilikuwa na nywele ndefu sehemu hizo.

Maumbile mengine ambayo yalionekana kuwa ya ajabu ni pamoja na midomo kuwa myekundu, mikono na miguu yenye kucha ndefu na viungo vingine vikionekana sawa na vya mtu mzima.

Akizungumzia tukio hilo jana, Ofisa Mtendaji wa Kijiji cha Mpasa, Privatous Maliyatabu alisema msichana huyo ambaye alipata ujauzito huo akiwa mwanafunzi wa darasa la tano, alijifungua saa 10 alasiri nyumbani kwa mjomba wake aliyetajwa kwa jina moja la Mwelela.
Maliyatabu alisema Lucia alijifungua kwa msaada wa mkunga wa jadi aliyejulikana pia kwa jina moja la Mama Pashaa, baada ya kupewa dawa ya kunywa na mganga wa jadi, Maneti Mazimba.

Kwa mujibu wa Lucia, licha ya kupata ujauzito huo, bila kukutana kimwili na mwanamume maishani mwake, alidai kutojua jinsi alivyopata ujauzito huo na kudumu nao miaka mitatu,
“Nakumbuka siku moja nilisimama mlangoni mwa nyumba yetu na ghafla nikaona kama mwujiza, mwanga mkali mbele yangu na kisha kujitokeza sura ya mwanaume ambaye siwezi kuhadithia umbile lake na akatoweka na tangu hapo, nilianza kuhisi tumbo kujaa na kuhisi kiumbe kikicheza,” alidai Lucia.

Baadaye aliwaeleza wazazi wake ambao walimpeleka hospitali baada ya kuona tumbo lake linaongezeka siku hadi siku, lakini kwa nyakati tofauti Lucia alipimwa katika hospitali tofauti na kuambiwa hakuwa na ujauzito.
Alisema:“Kila waliponipima waliniambia kuwa sina mimba, lakini miye nilikuwa nikihisi kitu kama mtoto kinacheza tumboni kwa kipindi chote cha miaka mitatu, hali hiyo ilizidi kunishangaza.”

Mmoja wa ndugu wa Lucia ambaye hakutaka jina lake litajwe, alisema wana uhakika ndugu yao hajawahi kukutana na mwanamume maishani mwake na familia nzima ilishangazwa na ujauzito wake,
“Lucia ni miongoni mwa watoto watatu katika tumbo la mama yetu, na amekuwa akitushangaza kwa yaliyokuwa yakimtokea tangu apate ujauzito huu, kwani mara nyingi usiku amekuwa akiweweseka, hali iliyofanya tuanze kuhangaika naye kwa waganga wa jadi baada ya hospitali kutueleza kuwa hana kitu tumboni,” alisema mwanandugu huyo aliyejitambulisha kuwa ni dada yake.

Kaimu Mganga Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, Dkt. Emmanuel Mtika alisema kitaalamu ujauzito unatakiwa kuwa kati ya wiki 38 na 40 na ikizidi sana wiki 42 hadi kujifungua na kuongeza kuwa hakuna ujauzito wa miaka mitatu,
“Inawezekana huyu mwanamke alikuwa na matatizo ya uvimbe tumboni kwa muda mrefu na akapata ujauzito wa muda wa kawaida ihali yeye akiamini kuwa alikuwa mjamzito kwa kipindi kirefu kumbe sivyo,” alisema Dkt. Mtika.

Alisema kinachoshangaza ni maelezo ya kudai kuwa mjamzito bila kukutana na mwanamume, kwani hakuna mwanamke anayeweza kupata ujauzito kwa hali hiyo,
“Inawezekana kuna mwanamume alitaka kufanya naye mapenzi kwa nguvu, lakini hakufikia sehemu mwafaka na labda mbegu za kiume zilimwagika karibu na sehemu zake za siri na kumwingia, hapo uwezekano wa kupata ujauzito upo,” alisema Daktari.

Hata hivyo, Dkt. Mtika alisema mwanamke huyo hakwenda hospitali kubwa kupata vipimo ili kubaini tatizo lililokuwa likimsumbua kwa kipindi chote hicho.

No comments:

Post a Comment