Banner

Banner

FOLLOW US FACEBOOK

propertyfinder.co.tz

Tuesday, October 2, 2012

Bodi ya Mikopo yasema imeshapeleka fedha vyuoni...!

Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dodoma (Udom), Profesa Idris Kikula

Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) imesema imeshapeleka fedha za chakula na malazi katika vyuo vyote vyenye sifa ya kupata huduma hiyo tangu wiki iliyopita.

Kauli hiyo ya HESLB, ilitolewa na Afisa Habari wake, Veneranda Malima, jijini Dar es Salaam jana.


Alisema kuhusu utaratibu wa wanafunzi kupata fedha hizo siyo jukumu la HESLB bali ni viongozi wa vyuo hivyo kwa utaratibu waliojipangia wenyewe.


Hata hivyo, Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE) cha jijini Dar es Salaam, kimesema fedha hizo hazijafika, lakini kimeahidiwa na HESLB kuwa zitapelekwa katikati ya wiki hii.


Waziri wa Mikopo wa Chuo hicho, Alek George, alisema:  “Sio kweli kwamba, fedha zimeshatumwa hapa chuoni, walituambia kuwa wiki hii watatupatia, lakini mpaka sasa bado.”


Wakati CBE wakisema hivyo, Chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFM) kilisema kupitia kwa Kaimu Afisa wake wa Mikopo, Rajabu Kufiri, kuwa wameshasaini fedha hizo tangu wiki iliyopita na kwa sasa wako katika utaratibu wa kuwapatia wanafunzi fedha hizo.


Chuo cha Tumaini Kampasi ya Dar es Salaam kilisema bado hawajapewa fedha hizo kutokana na kuchelewa kufungua chuo, na kwa sasa utaratibu wa kuwasajili wanafunzi unaendelea ili kupata idadi kamili ya wanafunzi wanaoendelea na masomo.


Afisa Mikopo wa Chuo hicho, Ukende Mwakitwange, alisema juzi HESLB waliwapatia orodha ya wanafunzi waliosajiliwa katika chuo hicho, lakini fedha hawajapatiwa.


Makamu  Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dodoma (Udom), Profesa Idris Kikula, alisema: “Bado hatujapata mikopo na leo hii (jana) nimetoka kuzungumza na wenzangu kuhusiana na suala hilo la mikopo kwa wanafunzi.”


Alisema kutokana na hali hiyo utawala umeamua kumtuma mtu kwa ajili ya kufuatilia suala hilo HESLB.


Afisa Habari wa Chuo Kikuu cha St. John, Karim Meshack, alisema HESLB imewapelekea majina ya wanafunzi wa mwaka wa kwanza, ambao wanastahili kupata mikopo.


Alisema mikopo hiyo inaweza kufika chuoni hapo mara baada ya wanafunzi hao kufanyiwa usajili.


Naye Afisa Mikopo wa Chuo cha Mipango, Daud Nyagalu, alisema: “Bado hatujapata mikopo na tunaendelea kufuatilia.”


Mkuu wa Chuo Kikuu Kishiriki cha Ushirika na Biashara (MUCCoBS), Profesa Faustine Bee, alisema: “Tunatarajia kufungua chuo Oktoba 15, mwaka huu, wanafunzi watakapofika chuoni ndio tutakuwa kwenye nafasi nzuri ya kuzungumzia kama wametuingizia fedha au la, matarajio yetu ni kupata fedha hizo kwa wakati.”


Uongozi wa Chuo cha Kumbukumbu ya Stephano Moshi (Smmuco), ulisema chuo bado hakijafunguliwa na baada ya kufunguliwa ndio watakuwa kwenye nafasi nzuri ya kueleza juu ya fedha za wanafunzi hao kama zimeingizwa kwenye akaunti au la.


Chuo cha Ustawi wa Jamii hakipapata fedha hizo na habari kutoka ndani ya uongozi zinaeleza kuwa chuo kilichelewa kufanya mitihani na kupeleka majina katika Bodi.


Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) kilisema fedha hizo zingepelekwa chuoni hapo Alhamisi iliyopita, jana kilishindwa kuthibitisha kuzipokea baada ya Makamu Mkuu wa Chuo hicho, Profesa Rwekaza Mukandara, kueleza kuwa alikuwa mbali na chuo.


Hata hivyo, Naibu Makamu Mkuu wa UDSM (Utawala), Profesa Yunus Mgaya na Kaimu Makamu Mkuu wa Chuo hicho, Profesa Frolence Luoga, hawakupatikana.


Imeandikwa na Gwamaka Alipipi, Amos Mbungu na Issaya Kisimbilu, Dar; Jacqueline Massano, Dodoma; na Salome Kitomari, Moshi.
CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment