Banner

Banner

FOLLOW US FACEBOOK

propertyfinder.co.tz

Thursday, October 25, 2012

MUSWADA WA MAFAO WAWALIZA WAFANYAKAZI..!

Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Jaji Frederick Werema

Muswada wa marekebisho ya sheria ya Mifuko ya Hifadhi ya Jamii ambao unatarajiwa kuwasilishwa katika mkutano wa Kumi wa Bunge, umewaacha solemba wanachama wa mifuko mingine baada ya marekebisho hayo kurejesha fao hilo kwa mfuko mmoja pekee.

Sheria ya mafao ilipitishwa katika mkutano wa Bunge wa Aprili mwaka huu na kuwazuia wanachama wa mifuko ya hifadhi ya jamii kuruhusiwa kuchukua mafao yao hadi wafikishe umri kati ya miaka 55 na 60.

Baada ya wanachama wa mifuko hiyo na wadau wengine wakiwamo wabunge kuipinga sheria hiyo, serikali iliahidi kuwa itaifanyia marekebisho na kuwasilisha muswada kwa hati ya dharura.

Tayari Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Jaji Frederick Werema, amekwishawasilisha muswada huo katika Ofisi Ndogo za Bunge, jijini Dar es Salaam, ikiwa na maana kuwa utajadiliwa kwenye Mkutano wa Bunge unaotarajiwa kuanza wiki ijayo.

Muswada huo unakusudia kufanya marekebisho ya sheria mbalimbali.

Kwa mujibu wa muswada huo, ambao NIPASHE imeuona, sehemu ya sita inapendekeza marekebisho kwenye Sheria ya Mfuko wa Pensheni wa Mashirika ya Umma (PPF), sura ya 372 kwa kuongeza kifungu kipya cha 44 ili kutoa fursa kwa mfuko huo kutoa fao la kujitoa kwa mwanachama wake.

Kwa maana nyingine ni kwamba wanachama wa mifuko mingine kama NSSF itaendelea kutumia sheria ambayo imelalamikiwa na wafanyakazi.

HOJA YA JAFO YAZIKWA

Akizungumza jijini Dar es Salaam jana, Mbunge wa Kisarawe (CCM), Seleman Jafo, ambaye wakati wa mkutano wa Bunge wa Bajeti, alitaka kuwasilisha muswada binafsi, alisema amepata barua kutoka kwa Katibu wa Bunge, Dk. Thomas Kashillilah, ikimtaarifu kwamba, serikali itawasilisha muswada wa marekebisho hayo, hivyo hana sababu ya kuandika muswada mpya.

Jafo alisema kwa kuwa alikwishawasilisha hoja ya kutaka marekebisho kwenye sheria ya hifadhi ya jamii, Bunge lilimweleza kwamba ni fursa kwa serikali au Kamati ya Bunge ya Maendeleo ya Jamii; hivyo serikali imeazimia kuiwasilisha kwenye mkutano ujao.

“Lakini kwa hali hii ni kwamba serikali haitatatua matatizo ya msingi ya hoja yangu, muswada unatakiwa uguse mifuko yote kwa sababu malalamiko ni ya wafanyakazi wote,” alisema.

SUGU AIONYA SERIKALI

Kwa upande wake, Mbunge wa Mbeya Mjini (Chadema), Joseph Mbilinyi maarufu kama Sugu, aliionya serikali kutochezea wafanyakazi kwa kuwa  kufanya hivyo ni kuhamasisha fujo.

Alisema ni vyema marekebisho yatakayowasilishwa bungeni yakarejesha fao la kujitoa kwa mifuko yote kwa kuwa wafanyakazi wengi hawana usalama kazini.

“Tunajua faida ya pensheni uzeeni kwa sababu ni msaada mtu anapostaafu, lakini kwa mfumo wa nchi yetu ambayo wafanyakazi hawana usalama wa kazi haiwezi kufanyakazi ipasavyo,” alisema.

Sugu alisema wafanyakazi kama wa migodini au hostelini wanafanyakazi katika mazingira magumu na wanaweza kuachishwa kazi wakati wowote hivyo fao la kujitoa litawasaidia.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), Dk. Ramadhan Dau, alisema fao la kujitoa katika mifuko ya hifadhi ya jamii halimo katika sheria za kimataifa.

Dk. Dau, alisema hayo alipokuwa akijibu hoja za wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC) katika kikao kati ya kamati hiyo na bodi na menejimenti ya shirika hilo, katika Ofisi Ndogo za Bunge, jijini Dar es Salaam jana.

Alisema pia ni Tanzania Bara pekee ndiko ambako kuna fao la kujitoa katika mifuko hiyo, lakini katika nchi za Kenya, Uganda, duniani kote, hata Zanzibar, suala hilo halipo.

Hata hivyo, alisema mwanachama wa NSSF anapoamua kujitoa, anaupunguzia Mfuko mzigo wa kumtunzia pensheni yake ya uzeeni, badala yake na kujiumiza mwenyewe.

Shinikizo la kutaka serikali kuirekebisha sheria hiyo ili wanachama wa mifuko walipwa mafao wakati wanapoacha kazi, liliilazimisha  serikali kukubali  yaishe na kuahidi kuwasilisha muswada wa marekebisho ya sheria ya mifuko ya Hifadhi ya Jamii wa mwaka 2012.

Waziri wa Kazi na Ajira, Gaudensia Kabaka, aliliambia Bunge la bajati kwamba kabla ya kuwasilishwa, muswada huo utapelekwa kwa wadau ili watoe maoni na pia Mamlaka ya Hifadhi ya Jamii (SSRA) itatoa elimu kuhusu fao la kujitoa.

Hata hivyo, alisema wapo baadhi ya watu waliotafsiri kuwa kusitishwa kwa fao la kujitoa kwamba mifuko ya hifadhi ya jamii imefilisika kwa kuwa imewekeza kwenye miradi mibaya, jambo alilosema sio la kweli.

Kabaka alisema kuwa mifuko hiyo haina hali mbaya kifedha wala haijafilisika na kwamba kuzuia fao la kujitoa ni utekelezaji wa sheria.

Waziri Kabaka alisema mchakato wa kuwasilisha muswada huo utaanza mara moja kwa kuwashirikisha wadau wote wa Sekta ya Hifadhi ya Jamii.

Kabla ya kauli ya Kabaka, Bunge lilipitisha Azimio lililowasilishwa na Jafo, la kuletwa bungeni muswada wa dharura wa marekebisho ya Sheria Na. 5 ya mwaka 2012 inayozungumzia marekebisho ya Sheria ya Mifuko ya Hifadhi ya Jamii ambayo ndani yake inaelezea kuzuiwa kwa fao la kujitoa kwa wafanyakazi.

Kutokana na mapendekezo ya muswada huo kutowatuhusu wanachama wa mifumo kingine kuchukua mafao kabla ya miaka 55 au 60, wanachama hao huenda wakashinikiza kwa njia za maadamano na migomo.

Aidha, upo uwezekano wa kuzuka mjadala mkali bungeni kwa kuwa na wabunge nao ni wanachama wa m
ifuko hiyo.

No comments:

Post a Comment