Banner

Banner

FOLLOW US FACEBOOK

propertyfinder.co.tz

Friday, October 12, 2012

Polisi wammiminia risasi Ofisa Uhamiaji

Ofisa Uhamiaji mkoani Mwanza, Albert Buchafwe, amenusurika kuuawa baada ya askari polisi kumiminia risasi tano kwa kile kilichodaiwa kuwa walimfananisha na jambazi sugu.

Akisimulia mkasa huo wa aina yake, Buchafwe alisema mkasa huo ulitokea usiku wa kuamkia jana saa 4:00 usiku alipokuwa akirejea nyumbani kwake maeneo ya Mhandu, Nyakato jijini hapa.

Alisema akiwa njiani kurejea nyumbani akiendesha gari aina ya Land Rover Discovery yenye namba za usajili T318 BJE, alipofika eneo la Machinjioni, aliona gari kwa mbele yake ambayo ilimmulika kwa taa zenye mwanga mkali kama ishara ya kumtaka asimame.

Aliongeza kuwa kama vile haitoshi, gari hilo lilimsogelea kwa kasi na kumzuia mbele, kitendo kilichomshtua na kulazimika kushusha kioo kujua kulikoni.

Kwa mujibu wa Buchafwe, baada ya kushusha kioo cha gari alimuona askari mmoja akishuka kutoka kwenye gari aina ya Suzuki rangi nyekundu iliyompita kwa kasi na akamtambua mtu huyo kuwa ni Abuu ambaye ni askari polisi.

“Baada ya lile gari kunizuia mbele, aliteremka mtu mmoja kunifuata huku akinitaka niteremke kutoka kwenye gari, mimi nikashusha kioo cha gari na kumuita kwa jina nikisema, Abuu ni mimi bwana kwani vipi?", alisema.

Aliongeza kwamba licha ya kumuita kwa jina, askari huyo (Abuu), alimjibu kwa sauti ya ukali akimtaka ateremke haraka kutoka kwenye gari vinginevyo atampiga risasi.

Alifafanua kuwa akiwa amepigwa butwaa, alitokea askari mwingine aliyekuwa na bunduki aina ya SMG huku Abuu naye akitoa bastola zake mbili.

Ofisa Uhamiaji huyo alidai kuwa baada ya kuona hali hiyo, aliamua kugeuza gari haraka na kuondoka kwa kasi huku nyuma askari hao wakimfyatulia risasi zipatazo tano ambazo hata hivyo, ziliishia kupiga bodi ya gari lake.

“Nilipoondoa gari kwa kasi, wao waliendelea kunirushia risasi, namshukuru Mungu hakuna iliyonipata, nikaamua kwenda kulala Igoma badala ya nyumbani kwangu,” alisema.

Alisema ilipofika asubuhi, alielekea ofisini kwake ambako aliamua kumsimulia bosi wake (Ofisa Uhamiaji  wa Mkoa) kuhusu mkasa huo ambaye naye alimpigia simu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Liberatus Barlow, kumweleza kilichotokea.

Kwa mujibu wa Buchafwe, Kamanda Barlow alimweleza Ofisa Uhamiaji wa mkoa kwamba (Buchafwe) alikuwa ameingia kwenye mtego wa polisi na kwamba ilikuwa auawe kwa kupigwa risasi.

Alipoulizwa jana kuhusiana na tukio hilo, Kamanda Barlow alithibitisha na kusema kwamba Ofisa Uhamiaji huyo alifananishwa kwa kila kitu na jambazi aliyekuwa anakusudia kwenda kuvamia na kupora katika ghala moja maeneo ya Nyakato ambalo hata hivyo hakulitaja.

“Ni kweli kuna tukio kama hilo, lakini yalikuwa ni mashambulizi ya gizani kwa sababu askari walimfananisha Ofisa Uhamiaji na jambazi waliyekuwa wamemwekea mtego, nadhani ana bahati kwani ndiyo kawaida yetu huwa hatubembelezani na majambazi,” alisema.

No comments:

Post a Comment