Banner

Banner

FOLLOW US FACEBOOK

propertyfinder.co.tz

Tuesday, November 6, 2012

Mwakyembe awatemea cheche wahujumu TPA.!

Waziri wa Uchukuzi, Dk. Harrison Mwakyembe

Waziri wa Uchukuzi, Dk. Harrison Mwakyembe, ameahidi kuwachukulia hatua kali za kisheria ikiwamo kuwapeleka jela wanaoendeleza vitendo vya hujuma katika Bandari ya Dar es Salaam na hivyo kudhoofisha ufanisi wa kiutendaji wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA).
Waziri Mwakyembe alisema ni dhahiri kuwa baadhi ya watendaji wamekuwa na mazoea ya kusimamishwa kazi mara wanapofanya makosa, hatua ambayo alisema haijawa fundisho la kukomesha vitendoi hivyo.
Alisema mara atakapothibitisha ukweli wa watu hao kuhusika na hujuma hizo, sheria itafuata mkondo wake ili iwe fundisho kwa wengine.
Aliyasema hayo jana jijini Tanga alipokuwa akifungua kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Wizara ya Uchukuzi.
Alisema uko mtandao wa wizi na ubabaishaji uliojengeka miongoni mwa watendaji wa taasisi zote za Wizara hiyo.
“Nimesikia kupitia Gazeti la NIPASHE kuwa kuna hujuma katika Bandari ya Dar es Salaam, bado sijasoma habari hizo kiundani zaidi, lakini nitakapozisoma na kubaini kuwepo kwa hujuma kweli nitawapeleka jela kwa sababu ni bora kufanya maamuzi magumu, lakini kazi ziende kuliko kulea wahalifu wachache,” alisema.
Alisema siyo rahisi kuimarisha na kuboresha huduma za usafiri iwapo kuna mwendelezo wa vitendo vya ukiritimba, wizi na ufisadi miongoni mwa wafanyakazi wa Wizara hiyo ambao muda wote wanawaza kudhoofisha utendaji wa serikali.
Alisema inasikitisha kuona TPA inaposhindwa kusimamia kikamilifu bandari zake na hivyo kudhoofisha uchumi wa nchi kwa kushindwa kuchangia katika Pato la Taifa.
Alisema: “Sitaogopa mtu hata kama ana fedha nyingi, lakini kwa sababu fedha hizo ni za wizi nitamnyofoa tu kikubwa ni kwamba nitasimamia haki.”
Alisema kutokana na hujuma na wizi unaofanywa katika bandari mapato yanayopatikana hayaongezeki na kwamba kiasi kinachokusanywa kwa mwezi ni Sh. bilioni 32 tu ukilinganisha na Bandari ya Mombasa ambayo mapato yake ni zaidi ya bilioni 200 kwa mwezi.
Alilitaka Baraza hilo kuimarisha nidhamu, uadilifu, uaminifu na uzalendo nahali pa kazi kwa lengo la kuhakikisha kuwa sekta ya uchukuzi inapiga hatua katika kukuza uchumi wa nchi.
Dk. Mwakyembe alisema wakati umefika kwa kila mmoja kuhakikisha kuwa anatimiza wajibu wake na akishindwa ajiachishe kazi yeye mwenyewe.
Jana katika hili toleo la jana kulikuwa na habari kuhusu hujuma ambazo zinazodhoofisha ufanisi wa utendaji katika TPA.
CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment