Banner

Banner

FOLLOW US FACEBOOK

propertyfinder.co.tz

Thursday, November 15, 2012

RAISI KIKWETE AWAONYA CCM KUTEGEMEA POLISI...!


 Na : Julius Magodi na Habel Chidawali, Dodoma
RAIS Jakaya Kikwete juzi aliwaonya wanachama wa CCM akiwataka waache kubweteka kwa kuwategemea askari polisi katika masuala ya kisiasa, kwani kufanya hivyo watakuwa wanajidanganya.

Kikwete alitoa kauli hiyo wakati akifunga Mkutano Mkuu wa Nane wa CCM uliofanyika kwa siku tatu mfululizo katika Ukumbi wa Kizota mjini Dodoma.

Kikwete ambaye pia ni Mwenyekiti wa CCM, alisema kitendo cha wanaCCM kuishi katika siasa kwa kutegemea Jeshi la Polisi hakipaswi kukubaliwa kwani kimepitwa na wakati.

“Mnaishia kulalamika tu kila siku, eti wanatukana halafu mnaishia kusema ndiyo kawaida yao…au utasikia mtu anasema eti Serikali haipo! Kazi ya Serikali siyo hiyo, hiyo ni kazi ya kisiasa maana hao ndio wenzenu,”alisema Kikwete na kuongeza:

“Sasa mnataka wakisema Serikali ya CCM haijafanya kitu polisi wawafuate, au wakisema Kikwete nchi imemshinda, polisi wakawakamate? Kama wakisema hatujafanya kitu ni kazi yenu kusema kwamba tumefanya kitu, waonyesheni barabara, shule na mambo mengine.”

Licha ya kwamba hakuwataja moja kwa moja, kauli za Rais Kikwete zilikuwa zikielekezwa kwa uogozi wa Chadema ambao kimsingi kinaonekana kuwaumiza vichwa CCM.

Huku akirudia mara kadhaa maneno hayo alisema, “Nataka mfahamu ndugu zangu kuwa tukiishi kwa kutegemea Jeshi la Polisi kufanikisha mambo yetu, tutakwisha na tutakwisha kweli.”

Kikwete aliwatuhumu viongozi wa upinzani kwamba ni waongo na kwamba wakati mwingine wamekuwa wakizusha mambo ambayo hayapo, huku wakijifanya kuwa na ushahidi wa kimaandishi.

Alimtaja Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa kwamba kuna wakati aliwahi kuzusha kwamba yeye (Kikwete), na makada kadhaa wa chama hicho wakiwamo Rostam Aziz walikuwa jijini Mwanza usiku, wakati si kweli kwani siku waliyodai alikuwa Nachingwea mkoani Lindi kwenye mikutano ya kampeni za urais.

Katika mazingira hayo, aliwataka wanaCCM kila mahali kujibu hoja za wapinzani kwa kauli na vitendo na wasikubali kuburutwa kwani uongo ukiachwa kwa muda mrefu unageuka kuwa ni ukweli.

Aliwaeleza kuwa ukimya wao katika kujibu hoja za wapinzani ni sumu kwao na kwamba wenzao wameanza kuaminika zaidi yao licha ya kuwa CCM ndio wenye majibu yote.

“Mkijibu kwa hoja wanatulia, sio Polisi. Nakumbuka Mwigulu aliwajibu pale bungeni kuhusu bajeti yao mbadala. Walipoitoa kijana wetu akasimama na kupiga msumari kweli wakachanganyikiwa sasa hizo ndio kazi zinazotakiwa jamani,” alisisitiza Kikwete.

Mbali na hilo aliwaonya kuacha malumbano ya mara kwa mara akieleza kuwa hali hiyo inakibomoa chama.

Alisema baadhi ya wanaCCM wamekuwa wakitumia muda mwingi kukosoana wao kwa wao, huku wakitoa nafasi kwa adui zao.

Mwenyekiti huyo alisema hakuna mtu kutoka nje ya chama anayeweza kukidhoofisha CCM kwa hoja isipokuwa chama hicho kinaumizwa na wanachama wake ambao wamekuwa wakilumbana bila sababu.

Akizungumzia suala la wagombea urais aliwataka wanachama wenye nia kufuata taratibu zote za chama pamoja na kuvumiliana ili ifikapo Mei 2015, mkutano utafanya uamuzi wa nani anasimama kupeperusha bendera ya chama hicho.

“Kwa wale mnaotaka kugombea, andikeni hiyo tarehe tutakuja hapa kuteua, lakini msituvuruge lazima mfuate utaratibu. Utaratibu huo utatangazwa, maana mkianza kupita huko na huko ndiko tunakopata matatizo,” alisema Kikwete.

Kikwete juzi alichaguliwa kwa mara nyingine kuwa Mwenyekiti wa CCM baada ya kupata asilimia 99.92 ya kura zilizopigwa, huku kura mbili zikimkataa. Kadhalika mkutano huo uliwachagua Dk Ali Mohamed Shein kuwa Makamu Mwenyekiti (Tanzania – Zanzibar) na Phillip Mangula kuwa Makamu Mwenyekiti (Tanzania Bara).

No comments:

Post a Comment