Banner

Banner

FOLLOW US FACEBOOK

propertyfinder.co.tz

Sunday, January 6, 2013

MTUHUMIWA KESI YA DR. ULIMBOKA ATOA SIRI NZITO...!

Na Martin Malera
SIKU moja baada ya Jeshi la Polisi Makao Makuu na Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam kutoa kauli tata kuhusu uchunguzi wa tukio la kutekwa, kuteswa kwa Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari, Dk. Steven Ulimboka, mtuhumiwa pekee katika kesi hiyo hadi sasa, raia wa Kenya, Joshua Mulundi, ameibuka na kutoa kauli na siri nzito ya tukio hilo.

Mtuhumiwa huyo ambaye yuko mahabusu, ameliambia gazeti hili kuwa anataka upelelezi wa kesi yake ukamilike haraka ili atendewe haki, lakini kubwa kuliko yote ameitaka serikali imlete Dk. Ulimboka mahakamani ili aweze kumtambua.

Akizungumza kwa kificho kwa njia ya simu kutoka ndani ya Gereza la Keko alikohifadhiwa, raia huyo wa Kenya alisema ameamua kutoa kauli hiyo baada ya kusoma taarifa ya gazeti hili juzi ilikionesha polisi wakirushiana mpira na kutoa kauli zinazopingana kuhusu tukio la Dk. Ulimboka.

Alisema hadi sasa haoni maendeleo ya kesi hiyo kwani kila ikifika mahakamani, upande wa mashitaka hutoa hoja ya kutaka iahirishwe kwa madai kuwa upelelezi haujakamilika.

“Kila ninapoenda mahakamani naiomba mahakama imlete Dk. Ulimboka anitambue, nahoji kwanini upelelezi haujakamilika. Kwa bahati mbaya sana siku hizi kesi hii inapokuja mahakamani, hata vyombo vya habari havijulishwi. Nashukuru Mungu nimepata namba zenu za simu kutoka kwenye gazeti lenu ili nitoe ya moyoni...

“Naomba Dk. Ulimboka aletwe mahakamani ili anitambue, kama atasema mimi ndiye niliyemteka na kumtesa, basi kesi iendelee na sheria ichukue mkondo wake, kama atasema sikuhusika, basi kesi iishe maana sioni sababu ya mimi kuteseka hapa gerezani kwa kusubiri upelelezi ambao haujulikani utaisha mwaka gani,” alisema Mulundi.


Kwa mujibu wa mtuhumiwa huyo, amepata kutoa malalamiko kwa Waziri wa Mambo ya Ndani, Dk. Emmanuel Nchimbi, Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Angela Kairuki na Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP), akiiomba serikali imlete mbele yake, Dk. Ulimboka ili amtambue na kuhakikisha upelelezi wa kesi hiyo unafikia tamati.

Mbali ya maombi hayo, mtuhumiwa huyo wa kesi inayovuta hisia za wengi ndani na nje ya nchi, pia alisema aliwaomba viongozi hao wamsaidie kupata dhamana kwani kesi inayomkabili inaruhusu dhamana na hana wakili wa kumtetea.

“Dk. Nchimbi alipokuja hapa gerezani nilimwambia, lakini aliniangalia tu bila kujibu kitu. Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Kairuki nimemwambia, DPP nimemwandikia barua na hata Balozi wa Kenya nchini Tanzania nimemwandikia, hajanijibu wala hakuna msaada ninaopata. Naomba serikali, jamii inisaidie kesi hii imalizeke haraka,” alisema mtuhumiwa huyo.

Hata hivyo mtuhumiwa huyo alitoa siri nzito ya kile alichokieleza kuwa, ukweli kuhusu Dk. Ulimboka, jinsi alivyokamatwa, kuhojiwa na kufikishwa mahakamani katika mazingira aliyodai tatanishi, ambayo gazeti hili kwa sasa haliwezi kuripoti kwani kufanya hivyo ni kuingilia mwenendo wa kesi iliyopo mahakamani.

Wakati Dk. Ulimboka alitekwa Juni 26 mwaka jana na watu wasiojulikana, mtuhumiwa huyo alikamatwa Julai 3 na kufikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kitusu, Dar es Salaam Julai 13.

Dk. Ulimboka ambaye alikuwa kinara wa mgomo wa madaktari uliotikisa nchini katika nyakati tofauti mwaka jana, alitekwa, kuteswa, kupigwa hadi kung’olewa meno na kucha na kisha kutupwa katika msitu wa Mabwepande, nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam.

Baada ya tukio hilo, Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova, alitangaza kuunda tume ya wataalam kutoka ndani ya jeshi hilo, iliyoongozwa na ACP Ahmed Msangi.

Hatua hiyo ilikuja baada ya Dk. Ulimboka mwenyewe kuwataja baadhi ya watu aliodai kuwa ndio walihusika kumteka na kumtesa, lakini hadi sasa Mulundi, ndiye mtuhumiwa pekee aliyekamatwa.

Hata hivyo, tume hiyo haijawahi kutoa ripoti yake kama Kova alivyoahidi pamoja na kwamba hata majeruhi mwenyewe, Dk. Ulimboka hajawahi kuhojiwa, huku vigogo wa jeshi hilo wakitupiana mpira kuhusiana na sakata hilo.

Katika hatua ya kushangaza, juzi jeshi hilo kupitia kwa msemaji wake, Advera Senso, limekanusha kuwepo kwa tume hiyo likisema kuwa walioteuliwa ni polisi ambao watafanya kazi za kiuchunguzi kwa taratibu za polisi.

Kauli ya Senso ilipingana na ile ya Kova, ambaye juzi alikiri kuwepo kwa tume hiyo, lakini akasema hawezi kulizungumzia suala hilo kwa vile taarifa zake alishazipeleka kwa wakubwa wake makao makuu baada ya kukamilisha wajibu wake.

“Hili suala lipo mahakamani kwanza, na kuhusu kuhojiwa au kutokuhojiwa kwa Dk. Ulimboka hilo lipo kwa mkubwa wangu, sasa unataka mimi niseme kama amehojiwa au la wakati sijui kinachoendelea huko?” alisema Kova.

Lakini Senso alisema kuwa, hakukuwepo na tume hiyo na kwamba walioteuliwa ni polisi ambao walifanya kazi za kiuchunguzi kwa taratibu za jeshi hilo.

Alisema Jeshi la Polisi lisingeweza kuunda tume katika suala la Dk. Ulimboka kwa kuwa kilichotokea ni uhalifu kama mwingine na litashughulikiwa kwa mujibu wa jeshi hilo.

“Kwanza hilo ni suala la mwaka jana na sisi ripoti za mwaka huo tumeshafunga, labda nianze kufuatilia sasa hivi kujua limefikia wapi,” alisema Senso.

Wakati vigogo hao wakisigana katika kulifafanua sakata hilo, Dk. Ulimboka mara kadhaa amekuwa akieleza kuwa yupo tayari kutoa maelezo yake kama kutakuwa na tume huru ambayo si hiyo iliyoundwa na polisi.

Katika tamko lake mwishoni mwa mwaka jana lililosomwa kwa niaba yake na wakili wa kujitegemea, Nanyoro Kicheere, akimwakilisha mwanasheria wake, Dk. Ulimboka alisema wapo watu ambao hawatapenda kusikia siri iliyojificha katika tukio zima la kutekwa kwake na kwamba hana jinsi zaidi ya kueleza ukweli.

Alisema kuwa tukio la kutekwa kwake, kusukumizwa kwenye gari, kupigwa, kufungwa mikono na miguu, kunyofolewa kucha na kutolewa meno, na hatimaye kutupwa katika msitu wa Mabwepande, lilitokea wakati akiwa kikao na ofisa aliyetambulishwa kwake ni ofisa wa Ikulu, Ramadhani Abeid Ighondu.

Chanzo:
Tanzania Daima

No comments:

Post a Comment