Banner

Banner

FOLLOW US FACEBOOK

propertyfinder.co.tz

Friday, February 8, 2013

MAREHEMU ASKOFU THOMAS LAIZER KUZIKWA IJUMAA IJAYO JIJINI ARUSHA...!


ALIYEKUWA Askofu wa Kanisa la Kilutheri Tanzania (KKKT) Dayosisi ya Kaskazini Kati,Marehemu Askofu Dk. Thomas Laizer anatarajiwa kuzikwa Ijumaa Februari 15, 2013.

Kwa Mujibu wa Taarifa maalum iliyotolewa na Kamati ya Mazishi ya KKKT na Familia ya Marehemu, inasema kuwa Marehemu atazikwa katika eneo la Kanisa Kuu mjini Kati Arusha. 


Aidha taarifa hiyo ambayo Father Kidevu Blog imeipata inasema kuwa waumini na Washirika wa Kanisa Kuu na makanisa yote ya KKKT nchini, Wananchi, ndugu jamaa na marafiki watapata fursa ya kutoa heshima za mwisho kwa Mwili wa marehemu kuanzia Alhamisi Alasiri ya Februari 14, 2013.
Taarifa hiyo iliongeza kuwa Mwili wa Askofu Laizer utalala Kanisani hapo hadi Ijumaa ya Mazishi.
Marehemu Askofu Thomas Laizer aliyezaliwa Machi 10, 1945 katika Kijiji cha Kitumbeni Arusha na baade kupata elimu yake ya msingi hadi darasa la nane Longido na kumaliza mwaka 1965.

Askofu Laizer, aliendelea na masomo yake ya juu ndani na baade kujiunga na masomo ya Theolojia katika chuo cha Makumira na baade kuongeza masomo nchini Marekani.
Marehemu wakati wa uhai wake alikuwa Mwinjilisti, Mchungaji katika makinisa mbalimbali nchini na baade kuwa Mkuu wa Jimbo na Mkuu wa Sinodi na baade kuwa Rais wa sinodi kabla ya kusimikwa rasmi kuwa Askofu wa Kwanza wa Dayosisi ya Arusha ambayo kwa sasa ni Dayosisi ya Kaskazini Kati.

Marehemu Baba Askofu Thomas Laizer ameacha mjane watoto wanne na mjukuu mmoja.
Nae Waziri Mkuu Mstaafu Edward Ngoyai Lowasa amesema kuwa Kanisa na jamii limempoteza kiongozi na mpigania maendeleo ya jamii kiroho na kimwili. 


“Tumepoteza kiongozi wa kiroho na kijamii,amehusika katika kuelimisha jamii kwa kuanzisha shule nyingi za Sekondari,amehusika pia ujenzi wa hospitali ya rufaa ya Arusha Lutheran Medical Center,zahanti na vituo vya afya katika vijiji kadhaa Mkoani Arusha pamoja na hoteli ya Corridor springs”alisema Lowasa. 


Aliwataka waumini wa kanisa la KKKT kuwa watulivu katika kipindi hiki kigumu baada ya kuondokewa na kiongozi wao.

"Natoa pole nyingi kwa familia ya marehemu Baba Askofu Laizer na kanisa la KKKT kwa ujumla wake,lakini askofu Laizer atakumbukwa kwa utumishi uliotukuka katika siku za uhai wake"alisema Lowasa akihojiwa na kituo cha radio cha kitaifa cha Radio one asubuhi ya leo.

No comments:

Post a Comment