Banner

Banner

FOLLOW US FACEBOOK

propertyfinder.co.tz

Wednesday, May 1, 2013

HADITHI:: MWANDISHI AMERUDI (A Journalist is Back)


    
                                                MWANDISHI: NYEMO CHILONGANI.
SIMU: 0718 069 269
              MAHALI: DAR ES SALAAM. 
Sehemu ya kwanza ..

   Mambo mengine yakaonekana kufumuka. Watu wakaanza kulitolea macho gazeti la Pamoja ambalo lilikwa na kichwa cha habari kikubwa  kilichoonekana kumvutia kila mtu ambaye alikuwa akiliangalia. Habari ile ikaonekana kumshtua kila mtu, hakukuwa na mtu aliyeamini kwamba mambo kama yale yangeweza kutokea kwa mara nyingine.

   Gazeti hilo likanunuliwa mtaani kupita kiasi, kila mtu alikuwa akiligombania. Kila mtu alitaka kujua hasa chanzo cha habari ile ambayo ilikuwa ikimvutia kila mtu. Mpaka inafika saa sita mchana, gazeti lile halikuwa likionekana mitaani.

   ‘VIONGOZI HAWA WATAFUNA MABILIONI YA WATANZANIA’ Kichwa cha habari kilikuwa kinasomeka vizuri mbele kabisa ya gazeti hilo tena huku kikiwa kimeandikwa kwa mwandiko mkubwa ambao hata kwa aliyekuwa na matatizo ya macho angeweza kuusoma.

   Shauku ya kutaka kufahamu kwa kina juu ya habari ile ndio ambayo iliwafanya watu kulinunua zaidi gazeti lile. Idadi kubwa ya wananchi ndani ya jiji la Dar es Salaam walikuwa na nakala ya gazeti lile ambalo mara kwa mara lilikuwa likizungumzia mambo yanayofanywa na viongozi wa Serikali

   Ununuzi mkubwa wa gazeti hilo haikuwa Dar es Salaam tu, bali hadi katika mikoa ya jirani, gazeti hilo lilikuwa likigombaniwa kupita kiasi. Habari ile ilimsisimua kila aliyekuwa akiiangalia. Hawakuamini kama viongozi ambao walikuwa wakiwaamini ndio ambao walikuwa wamefanya wizi mkubwa wa mabilioni.

   Watu hawakutaka kuishia kuisoma habari ile tu, kuna kitu ambacho walitamani kukifahamu zaidi, jina la mwandishi ambaye alijitolea kuandika habari ile. Jina la Dominick Hyera lilikuwa likionekana vizuri, mwandishi huyu ambaye mara kwa mara alikuwa akiyaandika maovu mengi yaliyokuwa yakifanywa na viongozi wengi alionekana kuyatoa sadaka maisha yake.

   Kila Mtanzania alimuona mwandishi Dominick kuwa shujaa, shujaa ambaye hakutaka kuona Watanzania wakiibiwa fedha zao ambazo walikuwa wakiziangaikia katika kuzilipia kodi. Dominick alionekana kuwa radhi kupata tatizo lolote lile ili mladi tu Watanzania wafahamu ni watu gani ambao walikuwa wakichukua fedha ambazo walikuwa wakiziangaikia.

   “Nitaendelea kuandika mambo haya hadi mwisho. Nitataka watu wote wabaya wajulikane” Hayo yalikuwa maneno ambayo mara kwa mara Dominick alikuwa akimwambia bosi wake.

   Dominick hakuonekana kuogopa kitu chochote kile. Maisha ya dhiki ambayo alipita katika kipindi cha nyuma ndio ambayo yalikuwa yakimfanya kuandika mambo hayo. Dominick aliwachukia viongozi wezi kuliko kitu chochote katika maisha yake.

   Aliandika mambo mengi kipindi cha nyuma, wizi ambao ulitendeka katika kila sekta nchini. Aliandika mambo mengi kuhusu EPA, Dominick hakufumbia macho, aliandika mambo mengi kuhusu BoT. Dominick hakuishia hapo, kila wizi ambao ulifanyika, aliuandika gazetini pasipo kujali kitu chochote kile.

   Jina lake liliendelea kuwa maarufu, kila mtu alitamani kumuona Dominick. Siku ambayo Dominick alionekana akihojiwa katika runinga, hakukuwa na mtu ambaye aliamini kuwa ni yeye. Alikuwa kijana mdogo sana ambaye kwa mtazamo wa haraka haraka alikuwa na miaka ishirini na tano.

   Kila siku maisha yake yalikuwa ni kuwaweka wazi watu wote ambao walikuwa wakitumia nyadhifa zao katika kuiba mamilioni ya Watanzania, ambao asilimia zaidi ya tisini na tano walikuwa wakiishi maisha ya kimasikini.

   Mtu pekee ambaye alikuwa akimtia moyo katika kazi yake alikuwa mke wake mpendwa, Christina pamoja na mtoto wake, Ibrahim aliyekuwa na miaka mitatu. Kila alipokuwa akiwaangalia watu hao, alijiona kupata nguvu ya kuandika mambo mengi zaidi.

   Hakutaka mtoto wake, Ibrahim apate matatizo kama yeye alivyopata matatizo kipindi cha nyuma kwa viongozi kula fedha ambazo zilitolewa kwa ajili ya kuendeleza elimu nchini Tanzania. Alijiona kuwa na jukumu kubwa kuhakikisha wezi anawaweka wazi ili hata nafasi ya kuiba mamilioni ya Elimu isiwepo tena.

   Kila kiongozi alikuwa akimuogopa Dominick, alionekana kuwa adui namba moja kwa viongozi ambao kazi yao kubwa ilikuwa ni kuiba mabilioni ya fedha ambazo zilikuwa zikilipiwa kodi kutoka kwa Watanzania.

   Siku za Jumanne na Ijumaa hazikuwa zikikalika ofisini, watu walikuwa mitaani kununua gazeti la Pamoja kujua ni mambo gani ambayo yalikuwa yametokea kwa viongozi kwa wakati huo. Kila siku Watanzania walikuwa wakiumia, hawakuamini kama fedha ambazo walikuwa wakizitoa kama kodi zilikuwa zikiliwa kirahisi namna ile.

   “Unajua kama leo ni sikukuu ya kuzaliwa ya Ibrahim?” Sauti ya Chrstina ilisikika ikiuliza swali kupitia simu.

   “Mungu wangu! Kumbe ni leo! Nilikuwa nimesahau kabisa mpenzi, mambo mengi” Dominick alisema huku mkono wake mmoja akiutumia kushikilia usukani.

   “Basi fanya haraka mpenzi. Fanya haraka kwa sababu wote hapa nyumbani tumekumisi, njoo tusherehekee pamoja” Christina alimwambia mumewe, Dominick.

   “Usijali. Ngoja nipitie madukani nikanunue zawadi” Dominick alimwambia mkewe.

   “Usichelewe....”

   “Usijali, nitawahi mpenzi”

   “Nakupenda”

   “Nakupenda pia” Dominick alijibu na kukata simu.

   Ingawa alikuwa safarini kurudi nyumbani, akakata kona na kuanza kuelekea katika maduka ambayo yalikuwa yakiuza vitu mbalimbali ambavyo vilikuwa vikitumika kama zawadi katika sherehe mbalimbali. Mara baada ya kufika katika eneo la maduka hayo, akasimamisha gari na kuteremka.

   “Nahitaji midoli kwa ajili ya mtoto wangu, na ni vizuri kama itakuwa na ujumbe wa siku ya kuzaliwa” Dominick alimwambia muuza duka.

   “Midoli ipo. Ipo ya aina mbalimbali na yenye jumbe tofauti tofauti” Muuza duka alimwambia Dominick huku akichukua baadhi ya midoli na kumkabidhi.

   Dominick akaanza kuiangalia baadhi ya midoli ile, aliyoiona inafaa, akaichukua na kuondoka dukani hapo huku ikiwa imetimia saa kumi na mbili na nusu jioni.

   Foleni ya magari kuanzia Ubungo ilikuwa kubwa mpaka Manzese Tip Top. Dominick alionekana kuchoka, tayari alijiona akichelewa kufika nyumbani. Kila wakati alikuwa akilalamika peke yake, foleni ilionekana kumchosha kupita kiasi.

   Muda ulizidi kwenda mbele lakini hakukuwa na dalili ya foleni kusogea mbele kutokana na magari ambayo mara kwa mara yalikuwa yakijiingiza. Foleni ilidumu kwa dakika arobaini, magari yakaanza kusogea kwa mwendo wa taratibu.

   Magari yalitembea kwa mwendo wa taratibu kwa dakika moja lakini yalikuwa yakisimama kwa dakika ishirini. Mpaka wanafika Ubungo na kupavuka tayari ilikuwa imetimia saa mbili kasoro. Dominick akaonekana kukasirika kupita kiasi.

   Kutoka Ubungo mpaka Kimara mwisho wala hakuchukua muda mrefu, ni ndani ya dakika nne tu akawa amekwishafika. Akakata kona na kuanza kuingia barabara ya vumbi na kuendelea na safari ya kuelekea nyumbani.

   Huku akiwa njiani, ghafla akasikia king’ora kikilia. Kwa haraka sana akaliegesha gari lake pembeni na gari lile la kitengo cha zima moto kupita.

   “Wanajifanya wana haraka sana na wakati utakuta nyumba yenyewe imekwishateketea” Dominick alisema huku akiachia tabasamu la chini.

   Akaendelea na safari yake ya kwenda nyumbani. Kila wakati alikuwa akiiangalia midoli aliyoiweka katika kiti cha pembeni. Furaha kubwa ilikuwa moyoni mwake, alimini mkewe, Christina angezifurahia zawadi zile kwa ajili ya mtoto wake, Ibrahim ambaye alikuwa akifikisha umri wa miaka mitatu.

   Dominick aliendelea na safari, moshi mkubwa ukaanza kuonekana mbele yake huku mwanga wa moto uliokuwa ukiendelea kuwaka ukizidi kuongezeka. Dominick akaonekana kuwa na wasiwasi, akaongeza kasi ya gari lake.

   Akakata kona ya njia ya kuelekea nyumbani kwake. Watu walikuwa wengi wakikimbilia katika njia ambayo alikuwa akiitumia kufika nyumbani kwake. Dominick akapigwa na mshtuko mara baada ya macho yake kutua katika nyumba ambayo ilikuwa ikiteketezwa kwa moto, ilikuwa nyumba yake.

   “Christina.....” Dominick akajikuta akiita.

   Hakuamini macho yake kama nyumba yake ndio ambayo ilikuwa ikiendelea kuteketea kwa moto. Kwa kasi ya ajabu akateremka kutoka garini na kuanza kupiga hatua kuelekea kule ilipokuwa nyumba yake huku akionekana kuchanganyikiwa.

   Majirani zake ambao walikuwa wakiiangalia nyumba ile, walipomuona, wakamzuia. Dominick akaanza kupiga kelele huku akionekana kuchanganyikiwa zaidi. Majirani ambao walikuwa wamemshika upande wa kulia na kushoto wakamshika zaidi.

   “Christinaaaaaaa..... Christinaaaaa... Ibrahimmmmm...” Dominick aliita huku akiwa amechanganyikiwa.

   Watu kutoka katika kitengo cha Zima moto bado walikuwa wakiendelea na kazi ya kuuzima moto ambao ulikuwa umeiteketeza nyumba ile. Kila mtu akaonekana kuchanganyikiwa, hawakuelewa sababu iliyosababisha moto ule.

   “Au shoti ya umeme ilipiga?” Kijana mmoja alimuuliza mwenzake.

   “Mmmh! Sidhani. Nafikiri kuna mtu atakuwa ameichoma moto” Kijana mwingine alijibu.

   “Kwa nini unasema hivyo?”

   “Hauisikii harufu ya petroli?”

   “Mhhhh! Inawezekana”

   Zoezi la kuzima moto liliendelea zaidi na zaidi. Dominick alikuwa akilia kama mtoto, alitamani achoropoke kutoka katika mikono ya watu waliokuwa wamemshika lakini watu wale walikuwa wamemshika vilivyo.

   Moto ulizimwa, hakukuwa na kitu chochote ambacho kilikuwa kimesalia, kila kitu kilikuwa kimeteketezwa kwa moto. Watu wakasubiri joto lipungue na ndipo waingie ndani. Walikaa kwa takribani dakika ishirini baada ya moto kuzimwa na ndipo wakaingia ndani ya nyumba ile ambayo tayari ilikuwa gofu.

   Dominick akatamani aingie pamoja nao lakini watu wale waliomshika hawakutaka kumuachia. Baada ya dakika fulani maiti ya Christina na Ibrahim zikatolewa huku zikiwa zimefunikwa kwa kanga. Dominick akajikuta akipata nguvu za ziada, akajitoa mikononi mwa watu wale na kuanza kuwafuata watu wale waliobeba maiti ya mkewe, Christina na mtoto wake, Ibrahim.

   “Christina.... Christina mke wangu...” Dominick aliita mara baada ya kuwafikia watu wale waliobeba maiti.

   “Christina...Christina...” Dominick aliita huku akiwa haamini kile ambacho kilikuwa kimetokea.

   “Ebu angalieni yale maneno pale” Jirani mmoja alisikika akiwaambia wenzake waangalie maneno ambayo yalikuwa yameandikwa getini.

   ‘BoT’ Maneno yale yalisikika.

   Dominick akageuka na kuangalia kule getini, maneno yale yalikuwa yakisomeka vizuri machoni mwake. Akaonekana kugundua ni kitu gani ambacho kilikuwa kinaendelea kwa wakati huo.

                                                                        *********

   Mara baada ya kukata simu, Christina akaanza kufanya maandalizi kwa ajili ya kusherehekea siku ya kuzaliwa ya mtoto wake, Ibrahim. Kwanza akampeleka kumuogesha na kisha kumvalisha nguo nzuri ambazo zilionekana kumvutia hata yeye mwenyewe.

   Christina akaingia jikoni ambako akaandaa chakula kizuri ambacho aliamini kingemfurahisha mumewe. Mara baada ya kumaliza kupika, akakipeleka chakula mezani.

   Muda ulizidi kwenda mbele lakini bado Dominick hakuweza kuwasili. Christina aliendelea kusubiri zaidi na zaidi, wakati mwingine alitamani kumpigia simu kujua ni mahali gani alipokuwa na kama zawadi alikwishanunua, lakini kila alipotaka kufanya hivyo, alisita.

   Muda ulizidi kusogea, mara kwa mara alikuwa akiangalia mishale ya saa kubwa ya ukutani, hasa mshale wa dakika, aliona muda ukizidi kusogea lakini wala mumewe hakuwa amefika nyumbani.

   “Fanya haraka mpenzi...” Christina alijikuta akiongea peke yake.

   Wala hazikupita dakika nyingi, akashtukia mlango ukigongwa. Christina akashtuka, hakuelewa ni nani ambaye alikuwa akigonga mlango wakati huo. Wazo la mumewe likamjia kichwani, lakini likapotea ghafla mara baada ya kugundua kuwa hakuwa amesikia muungurumo wa gari wala geti kufunguliwa.

   Swali juu ya mtu ambaye alikuwa akigonga mlango lilikuwa likijirudiarudia kichwani mwake kila nukta ambayo ilisogea. Akainuka kutoka katika kiti alichokuwa amekaa na kuufuata mlango.

   Christina akapigwa na mshtuko mara baada ya kuufungua mlango na macho yake kutua katika uso ambao ulikuwa umefunikwa kwa kutumia kinyago. Hata kabla Christina hakuchukua uamuzi wa kupiga kelele, akajikuta akizibwa mdomo.

   Vijana wengine ambao nao nyuso zao zilikuwa zimefunikwa na vinywago wakaingia ndani. Christina akawekwa kochini na kuamriwa kutokupiga kelele zozote zile. Akabaki akitetemeka kama mtu ambaye alikuwa akisikia baridi kali.

   Muda wote Christina alikuwa akilia, hakuelewa ni kitu gani ambacho kilikuwa kinaendelea mahali hapo. Kijana mmoja akamfuata Ibrahim ambaye alikuwa amewekwa katika kochi la pembeni, alipomfikia, akambeba na kumpelekea Christina.
***************************************************
USIKOSE KUANGALIA MUENDELEZO WA HADITHI HII..

No comments:

Post a Comment