Banner

Banner

FOLLOW US FACEBOOK

propertyfinder.co.tz

Wednesday, August 21, 2013

POLISI "CHANZO CHA MAUAJI YA BILIONEA ERASTO MSUYA NI KULIPIZANA KISASI"

Kamanda wa polisi mkoa wa kilimanjaro Robert Boaz
 
Wakati polisi mkoani Kilimanjaro wakitangaza kuwashikilia watu watatu kwa tuhuma za mauaji ya bilionea wa madini ya Tanzanite, Erasto Msuya (43), pia wamesema mauaji hayo ni ya kulipiza kisasi katika biashara ya madini.
Kauli hiyo ilitolewa mjini hapa jana na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Robert Boaz, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari juu ya hatua waliyofikia katika kusaka waliohusika na mauaji hayo ambayo yalitetemesha miji ya Arusha na Moshi.
Msuya aliuawa saa 6:30 mchana kwa kupigwa risasi kando ya barabara kuu ya Arusha – Moshi eneo la Mijohoroni, wilayani Hai karibu na Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA), Agosti 07, mwaka huu na kufa papo hapo.
Alifika eneo hilo akiwa peke yake baada ya kupigiwa simu na watu anaowafahamu kwenda kufanya nao biashara inayohisiwa kuwa ni ya madini ya Tanzanite.
Jana Kamanda Boaz alisema kwamba watuhumiwa hao ambao ni wakazi wa mikoa ya Arusha na Manyara, walikamatwa juzi na kufanya mahojiano na makachero wa Polisi na watafikishwa mahakamani kujibu tuhuma zinazowakabili.
Aliwataja waliokamatwa kuwa ni Sharifu Mohamed Athuman ambaye ni mchimbaji mdogo wa madini, Musa Juma Mangu ambaye ni dereva wa magari ya Shangarai mkoani Arusha na Shwaibu Jumanne Saidi, mkazi wa Mererani mkoani Manyara.
“Hawa tuliowatia mbaroni walikodishwa na wafanyabiashara waliokula njama za mauaji haya (hakuwataja wafanyabiashara hao), lakini tumefanya nao mahojiano na wakati wowote tutawaburuza kortini,” alisema Kamanda Boaz.
Kwa mujibu wa Kamanda Boaz, mauaji ya kikatili ya mfanyabiashara huyo yalisababishwa na kulipizana kisasi katika biashara ya madini.
“Inavyoonekana marehemu aliwekewa mtego na wauaji hao kwa kudai kwamba wana kiasi kikubwa cha madini na iko kama ni kulipizana kisasi kati yao ingawa tumewakamata watuhumiwa watatu,” alifafanua Kamanda huyo
Boaz alisema katika uchunguzi huo, wamefanikiwa kukamata pikipiki aina Toyo yenye namba za usajili T 316 CLV, ambayo ilitumika katika mauaji hayo ya kinyama.
Alisema uchunguzi zaidi juu ya mauaji hayo unafanyika na wahusika watafikishwa mahakamani taratibu za kuandaa mashtaka zitakapokamilika.
NIPASHE lilikuwa gazeti la kwanza kuelezea chanzo cha mauaji hayo ikiyafananisha na uhalifu unaofanywa na wahalifu wa kikundi cha mafia ambao huuana katika ama kudhumiana fedha au kulipizana kisasi katika biashara zao chafu.
Katika habari ambayo NIPASHE iliandika Agosti 9, mwaka huu yenye kichwa cha habari ‘Mauaji Bilionea Arusha ni biashara ya kimafia’ iliwanukuu baadhi ya wakazi wa jijini Arusha wakisema kuwa kuna kila dalili kuwa mauaji hayo ni matokeo ya kuzidiana kete katika biashara zisizo rasmi.
Habari hiyo pia iliongezewa nguvu na hoja ya watu wengi kwamba katika biashara ya madini ya Tanzanite usiri na kudhulumiana vimekuwa ni sehemu ya shughuli hiyo kiasi cha kusababisha visasi na hata mauaji.
“Wewe fikiria inakuwaje mtu abebe Sh. milioni 100 peke yake aende porini kote kule kufanya biashara.
Yaani anakwenda kununua madini porini, hana ulinzi, hana risiti hana nini… hapa aliitwa kuwa kuna mzigo kumbe wamemlengesha,” alisema mkazi mmoja wa Arusha ambaye aliomba kusitiriwa jina lake.
Aliongeza kuwa: “Unajua hawa wafanyabiashara bwana wana mambo yao mengi. Kwa sasa ni vigumu kusema hasa nini kimemtokea, lakini najua kwa miaka mingi mambo yao mengi ni deal (magendo) tu. Hata hapa unaona wazi kuwa maswali ni mengi kuliko majibu.”
Katika habari hiyo pia NIPASHE ilimnukuu mkazi wa Kaloleni Arusha anayejishughulisha na biashara ya utalii alisema kuwa ukiwaita wafanyabiashara wa madini wote hasa wenye vitega uchumi vikubwa jijini humo na kuwauliza nyaraka za shughuli za madini utashangaa kwa kuwa kila kitu kinafanyika kama watu wanaohama kesho.
“Si unajua bwana hata Benki Kuu ilikwisha kutoa maagizo kuwa hakuna malipo yanaozidi Sh. milioni 10 yanalipwa kwa cash (taslimu)? Sasa kama marehemu alikuwa na Sh. milioni 100 kama inavyoelezwa ina maana alikuwa anavunja sheria na pia anajihatarishia usalama wake mwenyewe,” alisema mkazi huyo huku akiomba jina lake lisitajwe kwa kuwa biashara za Arusha zina siasa zake.
Habari hiyo pia ilizungumza na kijana mmoja mkazi wa Usa River, Uria Nnko, ambaye amekuwa kwenye shughuli ya madini kwa kitambo sasa, ambaye alisema kuwa kwa muda mrefu sasa biashara ya Tanzanite jijini Arusha inategemea sana vijana aliosema “wanapiga mzigo” kutoka mgodi wa Tanzania One.
nko alisema kwa hali inavyoonyesha marehemu aliitwa kwenda kununua mzigo wa namna hiyo na kwa kuwa anajua hizo shughuli zipo aliingia kichwa kichwa kumbe safari hii alikuwa amewekewa mtego na waliomuua na kumpora.
Biashara hiyo imeelezwa kufanywa kwa mfumo wa uuzaji dawa za kulevya kama ambazo hufanywa duniani na makundi hatari ya uhalifu kama Mafioso (mafia) ambayo kila kitu humalizwa papo kwa papo bila nyaraka za kiserikali wala kibenki.
Kauli ya Kamanda Boaz sasa inathibitisha uvumi huu kwamba mauaji ya Msuya ni ya kulipizana kisasi katika biashara ya Tanzanite.
Msuya alifikwa na maafa hayo baada ya kudaiwa kupigiwa simu na watu waliotaka kumuuzia madini na kukubaliana wakutane eneo hilo.
Erasto alikuwa anamiliki mgodi wa Kalo uliopo Mererani na pia migodi mingine miwili ya baba yake Kikaango Msuya iliopo block B Mererani.
Mbali na migodi hiyo, Erasto alikuwa anamiliki vitegauchumi kadhaa ikiwamo hoteli moja kubwa inayojulikana kwa jina la SG Resort, iliyopo Sakina, Arusha.
 
Source: Nipashe

No comments:

Post a Comment