Banner

Banner

FOLLOW US FACEBOOK

propertyfinder.co.tz

Wednesday, March 4, 2015

MCT yaahidi ushirikiano na bloggers, ubalozi wa Marekani waunga mkono

Kulia ni Kajo akiwa na King Jofa wa Kilimanjaro Official Blog.

Baadhi ya bloggers waliohudhouria katika hafla ya kihistoria ya TBN iliyokutanisha bloggers kutoka mikoa mbalimbali ya Tanzania wakifurahia sherehe yao.

Baadhi ya bloggers na wageni waalikwa walioshiriki katika hafla ya kihistoria ya TBN iliyokutanisha bloggers kutoka mikoa mbalimbali ya Tanzania bara na Visiwani.

      Baraza la Habari Tanzania (MCT) limekubali kuanza ushirikiano na uhusiano mzuri na Chama cha Bloggers Tanzania (TBN) mara kitakapo maliza mchakato wa usajili wake na kutambulika rasmi kisheria. MCT imesema kwa hatua ya kwanza itafanya mazungumzo na viongozi wa TBN na kujadiliana namna gani ya kuisaidia TBN.
Kauli hiyo imetolewa juzi jijini Dar es Salaam na Katibu Mtendaji wa MCT, Kajubi Mkajanga alipokuwa akizindiwa hafla ya kwanza ya mwaka 2015 ya wamiliki na waendeshaji wa blogu na mitandao mingine ya kijamii iliyofanyika katika Hoteli ya Serena.
Katibu huyo Mtendaji wa MCT alisema kwa maendeleo ya sasa ya teknolijia ya habari na mawasiliano ni vigumu kuzitenga blogu kama vyombo vya habari, hivyo kuahidi kushirikiana na TBN kuhakikisha inafikia malengo yake ya kuwaunganisha bloggers na kufanya kazi zao kwa kuzingatia maadili.
Alisema MCT inasubiri TBN ipate usajili kisheria toka mamlaka husika serikalini na baada ya zoezi hilo itaanza kushirikiana maramoja na chombo hicho kilichoanzishwa kuwaunganisha wamiliki na waendeshaji wa mitandao ya kijamii nchini na wale wanaofanya shughuli za nje ya nchi.
“…MCT ipo tayari wakati wowote kuanza kushirikiana nanyi kikazi, tunachosubiri ni TBN kusajiliwa rasmi…mtakapo maliza usajili tu njooni ofisi, tutazungumza na viongozi wenu ili kujua nini cha kuwasaidia. Naombeni msichelewe tuanze hili mara moja,” alisema Kajubi Mkajanga akizungumza na wana-TBN kabla ya kuzinduwa sherehe hiyo.
Awali akizungumza katika hafla hiyo Mwenyekiti wa TBN, Joachim Mushi alisema kwa sasa mitandao ya kijamii imekuwa ikitekemewa na kundi kubwa la jamii katika kusambaza taarifa kwa haraka licha ya uwepo wa changamoto kadhaa ndani ya tasnia hiyo.
Alisema pamoja na mambo mengine, TBN imeanzishwa kwa lengo la kuwaunganisha waendeshaji na wamiliki wa blogu pamoja na mitandao mingine ya kijamii, na pia kuhakikisha wana-TBN wanapata fursa ya kujifunza zaidi maadili ya tasnia ya habari na mawasiliano ili kufanya kazi zao kiufanisi zaidi.
Aidha aliishukuru Kampuni ya Simu ya Vodacom Tanzania kwa kusaidia kufanikisha tukio la kukutana ‘bloggers’, pamoja na Benki ya NMB na makampuni mengine ya Coca Cola, AIM Group na kampuni ya huduma za intanenti ya Raha kufanikisha tukio hilo la kuwaleta pamoja bloggers wa Tanzania.
Akisoma risala ya wana-TBN kwa mgeni rasmi, Mjumbe wa TBN, Henry Mdimu alisema licha ya blogu kuwa chanzo kikubwa cha habari na mstari wa mbele kuwafikishia wananchi habari kwa haraka zaidi lakini bado zimekuwa hazitambuliwi na mamlaka zinazosimamia na kutetea tasnia nzima ya habari.
“…Pamoja na kazi kubwa na nzuri inayofanywa na ‘bloggers’ na waendeshaji wa mitandao ya kijamii, bado hawatambuliki rasmi na mamlaka husika pamoja na taasisi zinazohusika na usimamizi wa tasnia hii likiwemo Baraza la Habari Tanzania (MCT), Idara ya Habari (Maelezo), MISA-Tan na hata Mfuko wa Ruzuku kwa Vyombo vya Habari nchini (TMF).
“..Tunasema hivi maana tunaona kwa namna moja ama ingine wadau hawa muhimu hawajumuishwi katika harakati au michakato yoyote ile mnayoifanya kwenye tasnia hii. Mfano kupata semina za MCT, kupewa vitambulisho (Press card), kushiriki katika mafunzo na hata mashindano ya kila mwaka ya wanahabari yanayoandaliwa na MCT,” alisema Mdimu akisoma risala ya TBN mbele ya mgeni rasmi Bw. Mkajanga.
Kwa upande wa waalikwa rasmi kutoka ubalozi wa Marekani wakizungumza katika hafla hiyo kupitia kwa mwakilishi wao ameahidi kuisaidia TBN katika programu mbalimbali ili kuchochea uhuru wa habari nchini Tanzania.
Credit: Joachim Mushi

No comments:

Post a Comment