Banner

Banner

FOLLOW US FACEBOOK

propertyfinder.co.tz

Friday, September 4, 2015

BENKI YA DUNIA YAIDHINISHA DOLA MILIONI 80 KUJENGA AJIRA TANZANIA




Bodi ya Wakurugenzi Watendaji wa Benki ya Dunia leo wameidhinisha  mkopo wa maendeleo wa Dola za Marekani milioni 80 zinazolenga kuboresha utendaji katika sekta binafsi ya Tanzania, ili kukuza wajibu wake katika kujenga ajira nchini.
 
Kwa zaidi ya miaka kumi iliyopita, uwekezaji wa sekta binafsi ulikuwa umejikita  zaidi katika sekta chache zinazokua kwa kasi, kama vile sekta za madini, fedha, mawasiliano na uchukuzi, wakati sekta zinazohitaji nguvu kazi nyingi kama vile kilimo na uzalishaji viwandani zilikua kwa kiwango chini ya wastani wa uchumi  (takribani asilimia 7 mwaka 2014/15). Matokeo yake ni kwamba ajira hazikuongezeka kwa kasi inayolingana na kukua kwa idadi ya watu wanaoweza kufanya kazi.

“Maelfu ya vijana wanaingia katika soko la ajira kila mwaka na wanakuwa na ari na matumaini makubwa,” anasema Bi. Bella Bird, Mkurugenzi wa Benki ya Dunia nchini. “Kujenga ajira zenye tija ni kipaumbele kwa Tanzania, na ni sekta binafsi pekee ndiyo inayoweza kuzalisha idadi ya ajira zinazotakiwa. Mageuzi ya sera yanayofadhiliwa na mradi huu yatasaidia kupunguza vikwazo vya kufanya biashara nchini, kuruhusu sekta binafsi na ukuaji wa ajira.”

Kila mwaka, takribani vijana 800,000 wanaingia katika soko la ajira, ambalo linatarajiwa kukua kutoka watu milioni 20 leo hadi watu milioni 40 ifikapo mwaka 2030. Fursa za kazi zenye tija kwa vijana hawa bado ni finyu, nyingi zikiwa katika sekta isiyo rasmi.

Mazingira ya Kazi kwa ajili ya Shughuli za Sera ya Kuendeleza Ajira ni programu ya kwanza katika mfulululizo wa programu tatu za shughuli za msaada wa bajeti kwa Tanzania. Shughuli hii inajenga juu ya programu inayoongozwa na serikali ya ‘Matokeo Makubwa Sasa’ (BRN), na inasaidia programu kadhaa za sera zinazolenga katika kuboresha kwa ujumla ‘urahisi wa kufanya biashara’ na kuimarisha masoko ya vipengele vikuu (nguvu kazi, ardhi na mtaji). Aidha, shughuli hii inasaidia maboresho yanayolenga kuinua mazingira ya biashara katika biashara ya kilimo na utalii, sekta mbili zinazotoa ajira nyingi ambazo ni muhimu kwa Tanzania.

“Tunaunga mkono hatua madhubuti za kurahisisha maisha ya biashara,” anasema Andrea Dall’Olio, Kiongozi wa Kikosi Kazi cha Benki ya Dunia. “Kwa mfano, tuliainisha ada, ushuru na kodi zaidi ya 59 zinazotozwa kwenye sekta ya utalii na wakala mbalimbali wa serikali. Orodha kamili inaweza kupatikana katika tovuti ya Wizara ya Maliasili na Utalii, na tunaendelea kufanya kazi na serikali kupunguza kwa kiasi kikubwa idadi yao na athari zake kwenye biashara.”

Shughuli hii ya Kuendeleza Sera ya Ajira imetayarishwa kwa pamoja na Shirika la JICA (Japan International Cooperation Agency), ambalo limepanga kutoa fedha sambamba na Benki ya Dunia.

Na Mroki Mroki

No comments:

Post a Comment