Serikali
 inatarajia kuwanyang’anya wawekezaji waliopewa vibali vya kujenga 
hoteli za kimataifa kwenye hifadhi, kutokana na kushindwa kuendeleza 
maeneo hayo.
Hayo yalisemwa jana na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro 
Nyarandu, wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari, kuhusiana
 na kongamano la kwanza la Afrika, kuhusu usimamizi wa utalii endelevu 
katika hifadhi za taifa, litakaloanza Oktoba 15 na kushrikisha washiriki
 412 toka nchi 40 za Afrika.
Alisema kuwa maeneo hayo walipewa kwa lengo la kuyaendeleza na 
kupunguza uhaba wa maeneo ya kufikia watalii, lakini wameyahodhi na 
kushindwa kuendeleza, jambo linalokera na kulazimisha serikali kuchukua 
hatua zingine.
“Tutayachukua maeneo haya na yatakuwa chini ya hifadhi husika, kisha 
tutawapatia wawekezaji  wengine kuwekeza katika maeneo haya, na tutatoa 
kipaumbele kwa wazawa,” alisema Nyarandu.
Alisema kuwa Tanzania inahitaji hoteli za kutosha, sababu inakabiliwa
 na uhaba mkubwa wa vitanda vya kulaza wageni na kutoa mfano wa Mkoa wa 
Arusha ambako kuna vitanda 2,800, Dar es Salaam 3,700, Mwanza 914 na 
Kilimanjaro 414, wakati mji wa Nairobi nchni Kenya una vitanda 15,000 na
 Mombasa na Malindi 28,000, idadi ambayo inavimeza vitanda vya hapa 
nchini.
Alisema ili kukidhi mahitaji yaliopo kwa sasa ambayo ni makubwa sana,
 kutokana na kupokea idadi kubwa ya watalii na hasa wakati wa Msimu wa 
Utalii, kunahitajilka jitihada za haraka kukidhi hilo.
Aidha, serikali inatarajia kufungua Uwanja wa Ndege wa Arusha Mjini, ili uweze kutumika kwa kuruka na kutua ndege za kutoka
Nairobi moja kwa moja bila kupitia KIA.
Nairobi moja kwa moja bila kupitia KIA.
“Tukifungua Uwanja huu tutaweza kuongeza utalii kwa zaidi ya asilimia
 kumi, tena kwa haraka sana, hivyo tupo mbioni kuanza hili kwa ajili ya 
kupunguza pia muda mrefu wa kukaa watalii uwanja wa KIA kusubiri usafiri
 wa Nairobi,”alisema.
Kuhusu usalama wa watalii kutokana na mauaji ya watalii yaliyotokea 
siku za karibuni, alisema serikali wameongeza ulinzi wa kutosha maeneo 
ya hifadhi na kudhibiti wanaoingia bila sababu.
 
 
 
No comments:
Post a Comment