Banner

Banner

FOLLOW US FACEBOOK

propertyfinder.co.tz

Tuesday, July 31, 2012

CCM NA CHADEMA WAWATANGAZIA KIAMA WABUNGE MAFISADI...!


DK SLAA AONYA HAKUNA HURUMA, MSEKWA ASEMA RUSHWA  ADUI WA HAKI, MBATIA ATOA WIKI MOJA SPIKA AWATAJE WOTE   
Kizitto Noya, Dodoma na Leon Bahati, Dar
VYAMA vya CCM na Chadema vimetoa onyo kali kwa wabunge wanaotuhumiwa kwa kashfa ya kuhongwa na baadhi ya kampuni za mafuta na kulihujumu Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco), vikisema havitasita kuwawajibisha pindi tuhuma hizo zitakapothibitika.
Kauli ya vyama hivyo imekuja siku moja baada ya wabunge watano, watatu wa CCM na wawili wa upinzani kudaiwa kuhusika na vitendo hivyo vya rushwa, ambavyo vimesababisha Spika wa Bunge, Anne Makinda kuivunja Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini na kuagiza uchunguzi wa kina ufanyike ili majina ya wahusika yawekwe hadharani.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti jana, viongozi wa juu wa vyama hivyo walisema wanasubiri kwa hamu taarifa rasmi kutoka bungeni.
CCM: Rushwa adui wa haki
Makamu Mwenyekiti wa CCM Bara, Pius Msekwa alisema chama hicho kimewaapiza wanachama wake wote kutotoa wala kupokea rushwa.
Alisema rushwa ni kosa la jinai hivyo anaamini vyombo husika vya dola vitachukua hatua zinazofaa kwa mujibu wa sheria za nchi.
Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye alikazia kauli hiyo akisema rushwa inaelezwa katika katiba ya chama hicho kwamba ni, ‘adui wa haki’ na wanachama wote waliapishwa kuwa hawatapokea wala kutoa rushwa.
Alisema yeyote anayekwenda kinyume na kanuni za CCM, anajiweka katika kundi la wasaliti wa chama.
Alisema wabunge ni kundi maalumu nchini ambalo linalipwa vizuri ili lisimamie vyema misingi ya maendeleo ya nchi pasipo tamaa wala vishawishi hivyo wanapotajwa miongoni mwa kundi la wala rushwa, CCM kinalaani vikali tukio hilo.
Kuhusu tuhuma hizo kutajwa kuwahusisha wabunge watatu wa chama hicho, Nape aligoma akisema habari hizo siyo rasmi, hivyo hawezi kuzizungumzia.
Hata hivyo, alisema CCM kinasubiri uchunguzi ufanyike ambao  ndiyo utakaoweka bayana wahusika wa tuhuma... “Tusubiri uchunguzi ukamilike.  Idadi inawezekana ikawa hiyo au ikapungua au kuongezeka.”

Dk Slaa: Hatufumbii macho ufisadi
Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa alisema: “Nalaani kitendo cha wabunge kuhusishwa na ufisadi hasa ikizingatiwa kwamba Chadema tumekuwa tukiupinga vikali. Tumekuwa tukipinga rushwa kwa sababu ndiyo inayoielekeza nchi pabaya… Chadema hatufumbii macho rushwa.”
Alisema tangu kuanza Bunge la 10, Chadema kimekuwa kikiona baadhi ya mambo yanayoendelea katika mhimili huo muhimu wa dola yamejaa walakini... “Ndiyo maana sisi Chadema tumekuwa tukisema Bunge limepoteza mwelekeo.”
Alisema akiwa mtendaji mkuu wa chama, anasubiri taarifa kamili kutoka katika kikao cha wabunge wa chama hicho ili kuweka wazi majina ya wahusika na kisha kufuatiwa na kikao cha Kamati Kuu (CC) ambacho kitakaa na kuchukua hatua kali.
“Tunahitaji tupate maelezo ya kina... chama chetu hakikurupuki… Nasubiri taarifa ya kokasi ya chama. Katiba ya Chadema inatambua uwapo wa kikao cha wabunge wetu na kwa bahati nzuri, kiongozi wake mkuu ni Mwenyekiti wa Chadema (Freeman Mbowe) na katibu (David) Silinde ni mbunge wetu. Tunasubiri taarifa yao.”
Alisema Chadema kina kanuni ya kudhibiti rushwa hivyo, mbunge wake akitajwa miongoni mwa wanaohusishwa na rushwa, atawajibishwa kupitia kikao cha CC ya chama hicho.
NCCR-Mageuzi  yakoleza moto

Katika hatua nyingine, Chama cha NCCR- Mageuzi jana kilikoleza moto baada ya kumtaka Spika Anne Makinda awataje wabunge hao bungeni ili wafukuzwe na kufungwa kama Sheria ya Haki, Kinga na Madaraka ya Bunge inavyotaka.
Chama hicho kimetoa wiki moja kwa Spika Makinda kufanya hivyo, kikionya kuwa vinginevyo, chenyewe kitawasilisha hoja mahususi kutaka Bunge lichukue hatua hiyo.
Mwenyekiti wa chama hicho, James Mbatia alitoa tamko hilo mjini Dodoma, akisema  Sheria Namba 3 ya Haki, Kinga na Madaraka ya Bunge ya mwaka 1988, inataka wabunge wanaothibitika kujihusisha na rushwa wafukuzwe na kufungiwa kwa kipindi cha miaka mitano.
“Ni aibu kwa Bunge, taasisi inayoitwa tukufu kuwa na mafisadi. Kitendo cha Spika kukubali kuivunja Kamati ya Nishati na Madini na kuahidi kuzivunja nyingine, maana yake anakubali kuna mafisadi. Sisi tunamtaka atutajie wabunge hao bungeni ndani ya juma moja,” alisema Mbatia.
Mbatia aliyeongozana kwenye mkutano huo na wabunge Moses Machali wa Kasulu Mjini na Agripina Buyogela (Kasulu Vijijini), alisema pamoja na Bunge kuendeshwa kwa kanuni zake, kwa Tanzania kuwa mwanachama wa Jumuiya ya Madola inaweza pia kuiga yaliyofanywa katika nchi nyingine za jumuiya hiyo, zikiwamo India na  Uingereza.
Kwa mujibu wa Sheria zinazotumika katika nchi hizo, mbunge yeyote anayethibitika kutumwa na mtu nje ya Bunge, kuongea au kuandika bungeni kwa masilahi ya mtu huyo, anapaswa kufukuzwa ubunge na kufungwa.
“Kati ya mwaka 1924 na 1956, Uingereza ilifukuza wabunge 59 na kati ya mwaka 2005 hadi sasa, Bunge la India liliwafukuza wabunge 11 baada ya kuthibitika walihongwa na wafanyabiashara kuuliza maswali binafsi,” alisema.
Mbatia aliendelea kueleza kuwa katika Bunge la Nane nchini, wabunge wanne walikamatwa na kushtakiwa, kisha chama chao CUF, kiliwazuia kujihusisha tena na siasa baada ya kubainika kuwa walifunga ndoa batili na Wasomali ili wapate hati ya kuishi nchini.
“Sasa suala hili, wabunge wote wanaohisi wamo kwenye orodha hii ya ufisadi waachie ngazi. Mbunge yeyote na wa chama chochote anayeona ameshiriki uchafu huu, kwa utashi wake aachie ngazi,” alisema na kuongeza:
“Kwa vile vyama viadilifu, waige mfano wa CUF. Bunge lichukue nafasi yake kabla hatujafunga Bunge Agosti 18 tuwe tumefanya uamuzi wa kuwafukuza.”
Mbatia alisema ili Bunge lilirudi kwenye heshima yake, Spika Makinda pia anapaswa kuzitaja kamati nyingine alizosema zinachunguzwa na ikiwezekana nazo zivunjwe ili haki itendeke.
“Sisi (NCCR-Mageuzi) tunataka pia Spika azitaje kamati hizo, ziko sita na tuseme pia kwamba hatuna imani na Kamati ya Haki, Kinga na Madaraka ya Bunge. Tunataka nayo ijisafishe kwanza kwa kuwa nako kuna watuhumiwa.”
“Katika hili niombe kiti cha Spika kitende haki, hata kama kuna mbunge wa NCCR-Mageuzi anahisi alishiriki ufisadi huu, awahi mapema kuondoka, hii isiwe kwa vyama vingine tu,” alisema.
Mbatia alisema suala la Tanesco ni tone tu, akisema ufisadi kwa wabunge ulianza siku nyingi na kuongeza... “Mheshimiwa Kafulila (David) aliwataja wajumbe wa Kamati ya LAAC lakini, mpaka leo hakuna kinachoendelea.”
Alisema tatizo la ufisadi kuhusisha wabunge lilianza Juni 23, 2006 siku ambayo nchi iliingia mkataba na Kampuni ya Richmond... “Kuanzia hapo kumeendelea kuwa na sintofahamu katika Wizara ya Nishati na Madini. Dawa yake ni kuweka mikakati ya Bunge kujitakasa.”

Sakata lenyewe

Wabunge hao watano (majina tunayahifadhi kwa sasa) wanatuhumiwa kutumia nafasi zao za uwakilishi bungeni au ujumbe ndani ya kamati husika, kufanya biashara na Tanesco na kutetea mafisadi wanaolihujumu shirika hilo kutoka ndani na nje.
Hata hivyo, baadhi ya wabunge waliochangia hoja hiyo bungeni walisema wanawafahamu wabunge hao kwa majina, lakini wasingependa kuwataja kwa kuwa siyo wakati mwafaka.
Moto wa kutaka kutajwa kwa majina ya wabunge hao ulikolezwa na Mbunge wa Namtumbo (CCM),
Vita Kawawa  ambaye aliomba Spika avunje Kamati ya Nishati na kutaka pia Bunge lijadili kashfa hiyo.
“Waheshimiwa wabunge wamejadili suala hili kwenye wizara, lakini kwa mujibu wa Kifungu cha 55 (3) f, Mbunge au Waziri anaweza kutoa hoja ili jambo fulani lijadiliwe.
Sasa mimi naomba kutoa hoja ya kujadili suala hilo.”Baada ya hoja hiyo kuungwa mkono na idadi kubwa ya wabunge , ndipo Spika Makinda aliposimama na kukubali hoja hiyo ya Mbunge Vita Kawawa na kutangaza kuivunja kamati hiyo.
Spika Makinda alisema tayari pia, ameagiza Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge kutengeneza kanuni za kuwadhibiti wabunge wenye tabia hiyo ya kupokea rushwa kutoka kwa watu mbalimbali ili kutimiza matakwa yao binafsi.
“Nasema kwa dhati kabisa kitendo hiki hakikubaliki ndani ya Bunge. Wabunge mkae vizuri, kama kuna baadhi yetu wanakwenda huku na huku kujitafutia masilahi binafsi mnawezaje kuisimamia Serikali?”

Aliyekuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Nishati na Madini, Seleman Zedi alisema ameshtushwa na uamuzi huo wa Spika na kwamba anasubiri uamuzi wa Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge.
Akihitimisha hoja ya wizara yake bungeni, Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo alisema baadhi ya wabunge ambao wanashiriki kwenye vikao vya uamuzi vya Tanesco kama wajumbe wamekuwa wakilihujumu shirika hilo kwa njia mbalimbali ikiwamo kufanya nalo biashara.
“Shirika liliwahi kulipa Paundi 50,000 za Uingereza kwa ajili ya ununuzi wa vipuri, lakini kilicholetwa nchini ni masanduku ya misumari. Nguzo hizo za umeme kuna biashara inaendelea. Tunajua kwamba nguzo hizo zinazalishwa Iringa na kupelekwa Mombasa kisha kurudishwa nchini kwa maelezo kwamba zimetoka Afrika Kusini,” alisema Profesa Muhongo.

No comments:

Post a Comment