Banner

Banner

FOLLOW US FACEBOOK

propertyfinder.co.tz

Tuesday, July 31, 2012

ZITTO KABWE AHOJIWA KWA MASAAA MATATU KUHUSU TUHUMA YA RUSHWA INAYO MKABILI...!


Waandishi Wetu, Dar na Dodoma
SAKATA la wabunge kuhusishwa na rushwa limeingia sura mpya, baada ya Naibu Kiongozi wa Upinzani Bungeni, Zitto Kabwe kuhojiwa na chama chake cha Chadema kwa saa tatu jana.
Wakati Zitto akihojiwa, kambi rasmi ya upinzani bungeni, iliwataja wabunge saba wa CCM na kueleza kuwa ndiyo wanaolichafua Bunge kwa kujihusisha na mambo yenye maslahi binafsi wakiwa watumishi wa umma.

Kadhalika, Naibu Spika wa Bunge, Job Ndugai alisema kwamba Taasisi ya Kuzuia na Kupamba na Rushwa (Takukuru) ilikuwa ikiendelea kuwahoji baadhi ya wabunge kuhusu tuhuma za rushwa na kwamba uchunguzi ukikamilika taarifa zitawekwa wazi.

Zitto ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC) na Naibu Katibu Mkuu wa Chadema, jana aliandika katika ukurasa wake wa mtandao wa Tweeter kwamba alihojiwa na Sekretarieti ya chama chake kutokana na tuhuma za rushwa zinazowagusa badhi ya wabunge.
Katika maelezo yake, Zitto alisema aliiambia sekretarieti ya chama hicho kwamba Chadema kifanye uchunguzi ili kubaini ukweli wa suala hilo na kwamba yuko tayari kuwajibika ikiwa itathibitika kwamba alihusika kula rushwa.

“Kwa saa tatu nimejieleza mbele ya sekretariati ya chama kuhusu tuhuma za rushwa dhidi yangu. Niliomba kutaka kutoa maelezo kwa Katibu Mkuu, nimekiomba chama kufanya uchunguzi na ikibainika hatua zichukuliwe,” inasomeka sehemu ya taarifa hiyo kwenye Tweeter.

Lissu ataja wengine
Kwa upande wake, Mnadhimu Mkuu wa kambi hiyo, Tundu Lissu aliwataja wabunge wa CCM ambao wanatuhumiwa kuwa ni Nasir Abdallah (Korogwe Mjini), Mariam Kisangi (Viti Maalumu), Vicky Kamata (Viti Maalumu) na Charles Mwijage (Muleba Kaskazini) ambao hata hivyo, wote wamekanusha madai hayo.

Wabunge wengine watatu tumeshindwa kuwataja kwa kuwa hawakupatikana kuzungumzia tuhuma dhidi yao.

Katika orodha hiyo wamo wawili wa Viti Maalumu na mmoja wa jimbo na Lissu alidai kwamba wamekuwa wakishiriki vikao vya Kamati ya Nishati na Madini huku wakijua kuwa wana maslahi binafsi na wengine kutumia fursa hiyo kujinufaisha.
“Kwa takriban juma moja sasa kumekuwa na mjadala mzito wa ufisadi hapa bungeni, sasa Kambi Rasmi ya Upinzani imejitathmini na kuona kwamba wabunge wake hasa walioko kwenye Kamati ya Nishati na Madini iliyovunjwa, John Mnyika, David Silinde na Mwanamrisho Abama hawahusiki,” alisema Lissu na kuendelea:

“Ila uchunguzi wetu umefanikiwa kupata majina ya wabunge wanaohusika moja kwa moja na mgongano wa kimaslahi ambao tunaona tuwataje kwa maslahi ya umma.”
Lissu alikwenda mbali zaidi na kutaja tuhuma zinazowahusu wabunge hao akisema wawili ambao gazeti hili halikuwaja, wamejihusisha kufanya biashara na Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) hivyo wana mgongano wa kimaslahi.

Alisema Mwijage ana mgongano wa kimaslahi katika mchakato mzima wa kuipa zabuni ya kusambaza mafuta kampuni ya Puma Energy kwa kuwa yeye ni mtalaamu mwelekezi wa kampuni hiyo inayomilikiwa na Serikali kwa asilimia 50.
“Nasir Abdalah na Mariam Kisangi; Hawa wanamiliki vituo vya mafuta. Sasa kwa namna yeyote ile kuwa wajumbe wa Kamati ya Nishati na Madini hawawezi kutenda haki katika mchakato wowote unaohusu suala la mafuta,” alisema na kuendelea;

"....(jina limehifadhiwa) hana mgongano wa moja kwa moja wa maslahi, lakini kwa kadri tunavyofahamu, yeye ndiye aliyekuwa akiyafanyia kampeni ya kupata zabuni makampuni ya mafuta ya Oryx na Camel na ....(jina limehifadhiwa), suala lake ni complicated kidogo. Maslahi aliyonayo katika suala hilo ni kuwa ana uhusiano wa Kimapenzi na kigogo mmoja katika Wizara ya Nishati na Madini.”

“Hawa ndiyo wajumbe wa Kamati ya Nishati na Madini ambao sisi Kambi ya Upinzani tunawafahamu kuwa ndiyo waliojihusisha na mgongano wa kimaslahi. Tumewaangalia wabunge wetu wote watatu hawamo ila kama kuna mtu ana taarifa zinazowahusu, aseme na tutazifanyia kazi.”

Lissu alisema kitendo cha wabunge kujihusisha na mgongano wa kimaslahi na taasisi za umma ni kinyume na Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma ya mwaka 1995 na ni kinyume na maadili ya kibunge.
Katika hatua nyingine Lissu amemshauri Spika wa Bunge Anne Makinda kuzivunja pia kamati za Bunge za Serikali za Mitaa (LAAC) na Kamati ya Mashirika ya Umma (POAC) akisema nazo zina madudu mengi.

“Hili lisiishie tu kwa kuvunja Kamati ya Nishati na Madini, tunataka pia kamati za POAC na LAAC zivunjwe, uchunguzi ufanyike na wahusika waitwe kujitetea na hatimaye wenye hatia watajwe hadharani bungeni na majina yao yachapishwe kwenye magazeti ili haki itendeke,” alisema.

Alipoulizwa Chadema imefanya nini dhidi ya Mbunge wake, Zitto Kabwe kutajwa katika orodha hiyo, alijibu: “Nikiri kwamba sisi taarifa tunazo ila hatujamwita kumwuliza. Naomba ieleweke kwamba kama chama au Kambi Rasmi ya Upinzani hatuna maslahi na mbunge yeyote anayeonekana kujihusisha na masuala hayo.”
“Katika hili tunaomba uchunguzi ufanyike na matokeo yake yatangazwe ili tupate msingi wa tuhuma hizo na ninaahidi kwamba tutazifanyia kazi ipasavyo.”

Majibu ya tuhuma
Alipotakiwa kuzungumzia tuhuma hizo, Kisangi alikiri kumiliki kituo cha mafuta lakini akasema sheria haimzuii mtu kama mambo yake anayafanya kwa uwazi.

“Nimekuja bungeni nikitokea kwenye ualimu, nilikuwa nafundisha Shule ya Msingi ya Mianzini na biashara hii ni ya familia. Inaendeshwa kwa uwazi na mwanangu wa kwanza ndiye anayeisimamia. Kutokana na uwazi katika shughuli zangu, mwaka jana Tume ya Maadili ya Viongozi wa Umma ilinipongeza. Mimi ni msafi na siko huko wanakofikiri wao (Chadema).”

Kwa upande wake, Mwijage alikanusha kuwa mtaalamu mwelekezi wa Kampuni ya Puma, badala yake akasema ni mtaalamu wa petroli anayefanya kazi ya kuishauri Serikali kuhusu mambo mbalimbali yanayohusu nishati hiyo.

"Siyo kweli, hawa wanadandia hoja. Mimi ni mtaalamu wa petroli ambaye mchango wangu kimsingi una faida kubwa bungeni na hata kwa jamii kwa ujumla. Sijafanya maamuzi yeyote ya kulihujumu taifa hili na hata kwenye Bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini pekee, nilitoa mchango wa kurasa 10 kuhusu masuala hayo ya petroli,” alisema

Aliishauri kambi hiyo ya upinzani kuvuta subira, akieleza kuwa jambo lililoko bungeni linahusu ufisadi na uhujumu uchumi hivyo kauli zinazotolewa bila utafiti zinaweza kuvuruga mchakato mzima uliokwishaanzwa na Kamati ya Maadili ya Bunge.

Awali, Abdallah alipoulizwa kuhusu tuhuma za kumiliki vituo vya mafuta hivyo kuwa na maslahi binafsi, alicheka na kuahidi kwamba angepiga simu baadaye, lakini hakufanya hivyo na alipopigiwa baadaye alikata simu. Hata hivyo, alizungumza na waandishi wa habari na kukanusha kumiliki vituo vya mafuta.

Kamata kwa upande wake alisema: “Kuna kamati maalumu imepewa kazi ya kuchunguza mambo hayo, hivyo yote yanayoulizwa yatakuwa wazi na ukweli utajulikana tu. Nina maslahi au sina ukweli mtaujua, haraka ya nini?.

Mjadala Bungeni
Mjadala huo wa wabunge kuhusishwa na mgongano wa kimaslahi ulianza kulipuka bungeni jana asubuhi baada ya wabunge watatu; Joshua Nassari (Arumeru Mashariki), Salum Barwany (Lindi Mjini) na Mbunge wa Nkasi Kaskazni, Ali Kessy kutaka wabunge wanaotuhumiwa kwa ufisadi watajwe bungeni ili kuisafisha taasisi hiyo ya kutunga sheria.

"Mheshimiwa Naibu Spika juma lililopita Mheshimwa (Vita) Kawawa alitoa hoja kutaka suala la ufisadi lishughulikiwe kwa kuvunjwa Kamati ya Madini na Spika akaridhia na kulipeleka suala hilo kwenye Kamati ya Maadili. Kwa nini Kamati nyingine zilizohusishwa na ufisadi huo nazo zisivunjwe?” alihoji Nassari na kuendelea:

“Kuna Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) inayoongozwa na Mheshimiwa Mrema na Kamati ya Mashirika ya Umma (POAC) inayoongozwa na Zitto. Kuna tabia ya wabunge kuzikimbia kamati zisizokuwa na mikataba kama Kamati ya Huduma za Jamii na wanazikimbilia kamati zenye mikataba.”

Barwany alitaka Bunge litajiwe majina ya wabunge waliotuhumiwa kwenye kashfa hiyo mpaka wakapelekwa kwenye Kamati ya Maadili, akieleza kuwa hili litasaidia kulisafisha... “Tumeambiwa Kamati ya Maadili inajadili suala hilo, lakini hatujatajiwa ni wabunge gani waliopelekwa huko, tunaomba mtutajie ili Bunge lijisafishe.”

“Mimi naungana na wazo la Barwany na Nassari. Majina yatajwe wabunge tunadhalilishwa na wananchi huko mitaani. tuwataje hadharani,’ alisema Kessy.

Akitoa mwongozo wa hoja hiyo, Ndugai aliiagiza Kamati ya Uongozi ya Bunge kutoka kwenye ukumbi wa Bunge ili wakajadili suala hilo na baadaye apelekewe taarifa.
“Naamini wenyeviti wote wa kamati mmo humu ndani, naomba sasa hivi mwende kwenye Ukumbi wa Spika mkajadili suala hilo halafu nipate majibu sasa hivi,” alisema.

Baadaye jioni, Ndugai alisema kuwa Spika hawezi kuwataja kwa majina wabunge ambao wanajihusisha na rushwa kwa kuwa hawajui.

Alisema Kamati ya Uongozi iliyokutana jana mchana ilikubaliana kuwa ufanyike uchunguzi wa kina kwa ajili ya kuwabaini wale wanaoshukiwa na kwamba ikibainika Bunge litawaanika hadharani.

“Kamati imerejea kumbukumbu za hansard ya Jumamosi kuwa ufanyike uchunguzi wa kina juu ya jambo hilo na wabunge mtaitwa kwa ajili ya kutoa ushirikiano, ikumbukwe kuwa mbunge akiitwa siyo kwamba ndiyo amekuwa mtuhumiwa, bali pale itakapothibitika majina yatawekwa hadharani,’’ alisema Ndugai.
Naibu Spika alitahadharisha kuwa ndani ya Kamati hiyo utafanyika uchunguzi wa kutosha kubaini kama kuna mjumbe mwenye maslahi kwa wale wahusika basi ataondolewa ili kutoa nafasi kwa kamati kufanya kazi yake ipasavyo.

Aliwatahadharisha wabunge kuwa Kamati hiyo haitaingilia utaratibu wa vyombo vya dola ambao wamekuwa wakiufanya ikiwemo wa Takukuru wa kuwahoji baadhi ya wabunge.

No comments:

Post a Comment