Banner

Banner

FOLLOW US FACEBOOK

propertyfinder.co.tz

Monday, August 27, 2012

Ng’ombe 72 Wakamatwa Katika Hifadhi ya Kilimanjaro...!



Baadhi ya Ng'ombe waliokamatwa katika hifadhi ya Kilimanjaro.

HIFADHI ya Taifa ya Mlima Kilimanjaro (Kinapa) imekamata ng’ombe 72 ndani ya msitu unaozunguka mlima huo wakiwa wanachungwa kinyume cha sheria na kuharibu mazingira.

Kukamatwa kwa ng’ombe hao kumefanya idadi ya mifugo ambayo imekamatwa ndani ya msitu huo kufikia 150 kati ya Februari na Agosti mwaka huu.

Akisoma taarifa ya tatizo la mifugo inayoingizwa kiholela katika Hifadhi ya Mlima huo mbele ya Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Leonidas Gama, Mhifadhi Mkuu wa hifadhi hiyo, Erastus Lufungulo alisema tatizo la wananchi wanaozunguka hifadhi hiyo kuingiza mifugo limekuwa sugu na linaharibu mazingira kwa kiasi kikubwa.

Alitaja maeneo korofi ambayo yamekuwa yakiingiza mifugo msituni kuwa ni Mbahe, Kitowo, Mweka, Mandara, Komela na Kilema.

Hata hivyo, alisema kuna changamoto kubwa katika kukamata mifugo hiyo, kwa kuwa  eneo la msitu ni kubwa na inakuwa vigumu kwa askari wao kutembelea maeneo yote kwa siku moja.

“Mkuu kutokana na ukubwa wa hifadhi, inakuwa vigumu maeneo yote kuwa na askari kwa wakati wote na kwa siku zote, na wananchi wamekuwa wakitumia mwanya huo kuharibu mazingira,” alisema.

Lufungulo alisema tatizo la mifugo ni changamoto kubwa kwao kwani wanalazimika kutumia gharama kubwa za kuwatunza pindi wakisubiri hukumu za mahakama na pia wanalazimika kulipa wachungaji, gharama za kuwasafirisha kwenda mahakamani na kuwatibu pale wanapougua.

Mkuu wa Mkoa Gama alisikitishwa na kitendo cha wananchi kuendelea kulisha mifugo ndani ya hifadhi licha ya elimu na onyo linalotolewa na Serikali.

Alisema Serikali haitasita kuchukua hatua kali kwa wote watakaokamatwa wakilisha mifugo ndani ya hifadhi hiyo, na akaitaka Kinapa kupeleka ombi mahakamani ili waruhusiwe kupiga mnada mifugo hiyo, ili kuondokana na gharama za kulisha na kuilinda mifugo iliyokamatwa.
 
Chanzo: Rehema Matowo, Marangu


No comments:

Post a Comment