Banner

Banner

FOLLOW US FACEBOOK

propertyfinder.co.tz

Saturday, September 15, 2012

RAISI KIKWETE AZINDUA MAKAZI...!

Rais Jakaya Mrisho Kikwete



Rais Jakaya Kikwete,  amezindua mradi wa uwekaji wa anuani za makazi na postikodi mkoa wa Dar es Salaam na  kuwaagiza viongozi na watendaji wa Jiji,  kuipa majina  mitaa  ambayo haina majina.

Aidha alisisitiza kuwa  zoezi hilo lifanywe bila kisingizio cha  fedha kwani  kazi hiyo haihitaji pesa na kuwaonya wasije wakaikuza kuwa kazi ngumu inayohitaji kuandaliwa bajeti maalumu.

Aliwaambia  mameya, madiwani, maofisa wa mipango miji, ardhi, mabaraza  na viongozi wa mitaa kuanza zoezi  hilo kwa kutoa majina kwa mitaa ambayo haina.

Anuani za makazi zinamaanisha kuipa mitaa majina na kuweka vibao vya kuitambulisha barabarani, kutoa namba za utambuzi kwa majengo na kuyapa majina  majengo marefu.

Akizungumza katika uzinduzi huo uliofanyika jana, Rais alisema  mitaa mingi ya jiji haina majina kutokana na watendaji kutokutimiza wajibu ipasavyo.

 Rais alikumbusha kuwa  baada ya Uhuru mitaa ilipewa majina mfano Ilala  majina ya mikoa yalitumika mathalani Mtaa wa Arusha, Lindi  wakati  majina ya wanasiasa maarufu kama Samora,  Toure, Luthuli, Nkurumah, Indira Ghadhi  yanatumiwa katikati ya jiji.

Alishangazwa na watendaji wa sasa  kushindwa kuipa  mitaa majina na kuhoji inakuwaje maofisa wa mipango miji na wa ardhi  wapime viwanja, waweke miundo mbinu  lakini wasiipe  mitaa majina?

Alisema maeneo ya Mbezi Beach na  Tegeta yamepimwa lakini mitaa yake haina majina.

Katika hotuba  yake aliagiza watendaji kuachana na majina ya kizamani mfano  Mburahati Barafu na kubuni mapya yenye maana na kuongeza; “ondoeni majina ya kienyeji kama Kwa Dikwazu  ambayo maana yake ni kwenye  mti wa mkwaju”.

Rais aliwapa viongozi hao jukumu jingine la kutunga sheria  za kulinda miundombinu  yote inayotumika kwenye anuani za makazi mfano vibao vya majina ya mitaa na masanduku ya posta yatakayowekwa maeneo ya makazi.

“Usalama wa mali za watu  ni lazima katika masanduku yenu ya  posta,” alisema na kuwaagiza wadau wa mradi huo kutengeneza masanduku imara kuzuia mali za wateja kuibwa.

Aliwataka wadau hao kutoa elimu kwa wananchi ili wajue masuala ya anuani za makazi na wawe sehemu ya mradi huo.

Awali Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano (TCRA),  Profesa John Mkoma, alisema zoezi la kutoa anuani za makazi ambazo zitahusisha pia postikodi ambazo ni namba zinazotambulisha na kutofautisha eneo moja na jingine lilianza tangu mwaka jana.

Postikodi hizo zimegawanywa  hadi ngazi za kata  na kuongeza kuwa zoezi la kugawa posti kodi hizo kwa nchi nzima  limekamilika .

Profesa  Mkoma alieleza faida za anuani za makazi kuwa ni pamoja na kurahisisha usambazaji huduma, ufanyaji biashara, maeneo kufikika kwa urahisi,  kuimarisha ulinzi na usalama  pia inaweza kusaidia kujua idadi kamili ya wakazi wa eneo husika.

Dar es Salaam ni  mkoa wa tatu kutekeleza  zoezi hilo  baada ya Dodoma na Arusha.

 

CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment