Banner

Banner

FOLLOW US FACEBOOK

propertyfinder.co.tz

Thursday, June 27, 2013

Ulimi wamponza Pinda..!

 
NI wazi sasa, inaonekana ulimi umemponza Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, baada ya Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), kuendesha kazi ya kukusanya saini za watu mbalimbali ili kumwajibisha. Kituo hicho kimesema hadi jana, kilikuwa kimekusanya saini 1,000 za watu mbalimbali ambazo zinamtaka Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, kufuta kauli yake aliyoitoa bungeni wiki iliyopita.  Wiki iliyopita, Pinda alitoa baraka zote kwa Jeshi la Polisi nchini kutumia nguvu dhidi ya watu wote wanaovunja amani na utulivu, wakati akijibu maswali ya papo kwa papo mjini Dodoma. 


Katika kauli yake, alivitaka vyombo vya ulinzi, hasa Jeshi la Polisi kuwapiga watu watakaokaidi au kupinga amri halali zinazotolewa na vyombo hivyo.

Akizungumza na waandishi wa habari mjini Dar es Salaam jana, Mkurugenzi wa LHRC, Dk. Helen Kijo Bisimba, alisema kamwe hawakubaliani na kauli ya Pinda, kwa sababu haifuati haki za binadamu.

Alisema ni aibu kauli hiyo kutolewa na kiongozi wa juu serikalini, kwani inaonyesha wazi imevunja Katiba, sheria na misingi ya haki za binadamu.

Alisema Pinda, hatafuta kauli yake au kuomba radhi Watanzania, wao kama kituo watajua njia gani ya kufanya ili kulinda maisha ya Watanzania.

Alisema katika saini hizo, kituo chake kimezipokea kutoka maeneo mbalimbali, yakiwamo ya Kinondoni (Dar es Salaam), Chato, Biharamulo (Kagera), Temeke (Dar es Salaam).

Alisema mpaka jana, wananchi wengi wanaendelea kutuma saini zao kwa njia ya mtandao.

“Tunamtaka Waziri Mkuu Pinda, afute kauli yake aliyoitoa bungeni kubariki polisi kupiga raia katika mkutano huu wa Bunge la Bajeti au aombe radhi kwa Watanzania kwa kile alichokisema bungeni.

“Tunapenda kumkumbusha, utawala wa sheria unajumuisha serikali, vyombo vya utekelezaji na ulinzi pamoja na wananchi kuheshimu sheria na si kuvunja sheria…tamko hili limetoa mwanya mkubwa wa nguvu kwa vyombo vya usimamizi wa sheria kuvunja haki za raia.

“Hali hii ni ya kushtusha kwenye nchi yenye utulivu na amani na kama tunavyopenda kusema kisiwa cha amani, kiongozi huyu wa ngazi za juu anatoa tamko linaloashiria kutoa ruksa kwa Jeshi la Polisi kuvunja tena sheria, tunasema hatukubaliani nalo kamwe,” alisema Dk Bisimba.

Alisema katika miaka ya hivi karibuni, kumekuwa na matukio mengi ya ukiukwaji wa haki za binadamu, hasa yale yanayotokana na vyombo vya dola na Jeshi la Polisi, kwa kupiga na kuua watu kwa risasi za moto.

Waziri Pinda alitoa kauli hiyo bungeni, alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Kilwa Kaskazini, Murtaza Mangungu (CCM), aliyetaka kujua hatua zinazochukuliwa na serikali kutokana na matukio ya vurugu mara kwa mara nchini, hususani katika mikoa ya Mtwara na Arusha.

Katika swali hilo, Pinda alijibu: “Na mimi nasema wanaokaidi amri halali ya Jeshi la Polisi muwapige tu, kwa sababu hakuna namna nyingine ya kupambana na wakaidi zaidi ya kuwapiga”.

Kauli hiyo, pia ilipingwa vikali na Jaji mstaafu, Mark Bomani, ambaye alisema kutumia vyombo vya dola kudhibiti au kupiga watu kama ilivyoamuliwa na Pinda, haikubaliki.


habari NA ADELINA RUTALE, DAR ES SALAAM
chanzo - mtanzania

No comments:

Post a Comment