Banner

Banner

FOLLOW US FACEBOOK

propertyfinder.co.tz

Monday, September 16, 2013

FAHAMU KIWANDA CHA KUTENGENEZA BUNDUKI KILICHO GUNDULIWA MKOANI MOROGORO.


Kamanda wa Polisi, Mkoa wa Morogoro, Faustine Shilogile akizungumzia juu ya tukio hilo.


Mhifadhi wa Hifadhi ya Taifa ya Selous, Kisiro Nsabo, akizungumzia juu ya tatizo hilo katika Hifadhi hiyo.


Baadhi ya Siraha hizo zikiwa zimekamatwa


KIKOSI cha Kuzuia Ujangili cha jijini Dar es Salaam (KDU), kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi mkoani hapa, wamegundua mahali kilipo kiwanda cha kutengeneza bunduki na kuzikarabati kinyume cha sheria. Kiwanda hicho kiligunduliwa juzi katika Mtaa wa Kingo, Manispaa ya Morogoro, kutokana na msako uliofanywa na kikosi hicho.

Akizungumzia tukio hilo, Kamanda wa Polisi, Mkoa wa Morogoro, Faustine Shilogile, alisema kiwanda hicho kiligundulika Septemba 14, mwaka huu, saa sita mchana.

Pamoja na kugundua kiwanda hicho, alisema watu sita walikamatwa na watano wanaendelea kutafutwa kutokana na kujihusisha na utengenezaji wa silaha hizo.

Alisema kiwanda hicho bubu kilikuwa kwenye nyumba ya Ally Mavumila, ambaye ni marehemu.

Alisema kwamba wakati wa upekuzi katika nyumba hiyo, walikamata vitu mbalimbali na bunduki 11, zikiwamo aina ya rifle saba, shotgun mbili, magobole mawili na risasi 22 za rifle.

Alivitaja vitu vingine vilivyokamatwa kuwa ni maganda 13 ya risasi, mitutu 23, ikiwamo ya magobole miwili, shotgun miwili na rifle 458 pamoja na vifaa vingine vya bunduki.

Kwa mujibu wa Kamanda Shilogile, wakati wa upekuzi huo pia walikamata, mifuko ya kubebea silaha, mkanda wa kubebea bunduki, vyuma vya kushindilia baruti kwenye magobole, baruti robo kilo pamoja na mitambo ya kutengenezea bunduki.

Alisema licha ya watu hao kujishughulisha na utengenezaji wa silaha, pia watuhumiwa hao walikuwa wakichonga funguo za aina mbalimbali, zikiwamo za magari, pikipiki na za majumbani.

Hata hivyo, hakuwataja majina, kwa kile alichosema kuwa, uchunguzi bado unaendelea, japokuwa watafikishwa mahakamani wakati wowote baada ya upelelezi kukamilika.


Pia, kamanda huyo wa polisi aliwashukuru wananchi kwa ushirikiano walioutoa na kufanikisha kukamata wahusika wa kiwanda hicho.

Kwa upande wake, Mhifadhi wa Hifadhi ya Taifa ya Selous, Kisiro Nsabo, alisema wamekuwa wakikabiliwa na changamoto ya majangili ambao wana kawaida ya kuua wanyama bila vibali.

“Tuna changamoto kubwa ya kukabiliana na hawa majangili, kwani tukiwakamata wanasema wametumwa na matajiri wakubwa, hawa matajiri ndio wanasababisha huu ujangili uendelee kuwapo, ingawa tunajitahidi kukabiliana nao.

“Kuhusu msako tulionao, huu ni endelevu na ni maalumu, kwani umeshirikisha Hifadhi za Mikumi, Milima ya Udzungwa, Selous na Kikosi cha Kuzuia Ujangili kutoka Dar es Salaam.

Chanzo: Mtanzania
Picha na Morogoro Yetu

No comments:

Post a Comment