Banner

Banner

FOLLOW US FACEBOOK

propertyfinder.co.tz

Monday, August 20, 2012

MWANASHERIA MKUU APINGA SHERIA YA KUIKWAZA TAKUKURU KUWASHTAKI VIGOGO WA UFISADI...!


Jaji Werema.
MWANASHERIA Mkuu wa Serikali (AG), Jaji Frederick Werema amesema Sheria ya Taasisi ya Kuzuia na Kupamba na Rushwa (Takukuru), ni nzuri na kwamba haipaswi kufanyiwa mabadiliko kama ambavyo imekuwa ikidaiwa.

Jaji Werema aliliambia gazeti hili jana kuwa haoni haja ya sheria hiyo kufanyiwa mabadiliko sasa kwa kuwa haina tatizo na ipo kutekeleza misingi ya utawala wa Sheria.

"Mimi nakubaliana na Sheria hii ya (Takukuru) kwamba iendelee kuwapo. Hakuna haja ya kuifanyia mabadiliko sasa. Ni nzuri kwa kuwa inazingatia misingi ya utawala wa sheria," alisema Jaji Werema.

Kauli ya Jaji Werema inapingana na ile iliyotolewa na Mkurugenzi Mkuu wa Takukuru, Dk Edward Hoseah kwamba sheria hiyo imekuwa ikiwakwaza kuwashughulikia wala rushwa wakubwa, kwani majalada ya kesi zilizokwishafanyiwa uchunguzi yamekwama kwa Mkurugenzi Mkuu wa Mashtaka (DPP).

Wiki iliyopita Dk Hoseah alilalamikia sheria hiyo, hasa kifungu cha 37 na 57 akisisitiza kuwa ni mbovu kwa kuwa vinamzuia kuwafikisha watuhumiwa wa rushwa kubwa mahakamani. “Tusaidieni sheria hii ibadilishwe ili iweze kuturuhusu kufanikisha kupambana na rushwa nchini,” alisisitiza Dk Hoseah.

Hata hivyo, jana Werema alipinga dhana hiyo na kusema kwamba siyo sahihi kuipa Takukuru mamlaka yote; kutuhumu, kupeleleza na kushtaki kwa kuwa kufanya hivyo ni kinyume na demokrasia, Katiba na utawala wa sheria.

Kumrundikia mtu au taasisi moja mamlaka zote hizo, ni kinyume na misingi ya utawala bora, alisema.

"Haiwezekani mtu (Dk Hoseah) akawa na mamlaka ya kupeleleza na kushtaki, halafu Mahakama ikiwaachia huru watuhumiwa, atasema siyo mimi ni kosa la Mahakama, We can't do that! (hatuwezi kufanya hivyo)," alisema Werema na kuongeza:

"Mimi nakubaliana na kitu kimoja, kila mamlaka iwe na kigingi. Iwe Mamlaka ya Rais, Bunge au Mahakama, lazima kuwe na chombo cha ku-check and balance," alisema Jaji Werema.

Kauli hiyo ya Jaji Werema imekuja siku chache tangu Mkurugenzi wa Mashtaka, (DPP) Eliezer Felishi kukiri kwamba kazi ya kuwafikisha watuhumiwa hao mahakamani ni yake, lakini kesi nyingi zinakwama.

DPP Feleshi alisema ucheleweshaji wa kesi za rushwa kupelekwa mahakamani, unatokana na kukosekana kwa ushahidi wa kutosha. "Ikifikia hapo, nalazimika kuyarudisha mafaili hayo kwa Takukuru," alisema.

"Mimi nafanya kazi kwa kufuata sheria na taratibu zilizowekwa na Serikali. Siwezi kufanya kazi kwa sababu mtu fulani ametaka nifanye. Jambo hilo linaweza kuniletea matatizo baadaye," alisema na kuongeza:

"Kutokana na hali hiyo, siwezi kupeleka mahakamani jalada ambalo halijakamilika. Sheria inanipa siku 60 niwe nimepeleka kesi mahakamani, lakini kama ushahidi haupo cha kufanya ni kurudisha Takukuru faili.”

Madai ya Dk Hoseah
Awali Dk Hoseah alisema anajua matarajio ya wananchi ni makubwa kwa Takukuru, lakini sheria imewafunga mkono kwa kuwa hawawezi kuchukua uamuzi dhidi ya kesi kubwa za ufisadi bila ushauri wa DPP.

“Sina mamlaka ya kumpeleka mtuhumiwa wa rushwa kubwa mahakamani. Uwezo wangu ni kupeleka walarushwa ndogondogo tu na kwamba kazi yangu ni kuchunguza tu,” alisema Dk Hoseah na kuongeza;

“Sheria yetu imetufunga mikono kwa kuwa kumpeleka mtu mahakamani siyo uamuzi wangu, bali ya DPP.”

Awali Dk Hoseah alisema sheria hiyo katika kifungu cha 57 inamzuia kuwapeleka mahakamani watuhuhumiwa wakubwa wa rushwa, mpaka awafikishe kwa Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (DPP).

Kifungu hicho cha 57 (1) kinasema kuwa shtaka lolote la kosa lililoelezwa kwenye Sheria ya Takukuru lazima lifunguliwe kwa ruhusa ya maandishi kutoka kwa DPP. Kifungu cha 57 (2) kinamtaka DPP ndani ya siku 60 kutoa au kukataa ruhusa ya kushtakiwa.

Dk Hoseah alisema, hiyo ni moja ya changamoto zinazoikabili taasisi yake na kwamba wananchi wasubiri mabadiliko ya kiutendaji kama sheria itabadilika na kumruhusu kufanya hivyo.

Maelezo ya Dk Hoseah yanaungwa mkono na sehemu ya taarifa ya awali ya Mpango wa Nchi za Afrika wa Kujitathmini (APRM) ambayo inaeleza kwamba kikwazo cha ufanisi katika vita ya rushwa nchini Tanzania ni sheria inayowazuia Takukuru ipate kibali cha DPP kabla ya kufungua kesi kubwa za rushwa.

“Ni wala rushwa wadogo wadogo tu ndiyo wanaoweza kushtakiwa na Takukuru, lakini makosa makubwa ya rushwa yanayohusu viongozi au watu wa karibu na viongozi wakubwa ni mara chache sana kufunguliwa kesi mahakamani,” inasema sehemu ya taarifa hiyo na kuongeza:

“Mfumo huu ni kama unainyima mamlaka ya kiutendaji Takukuru na kimsingi, unakandamiza juhudi za chombo hiki kupambana na rushwa”.

Hii siyo mara ya kwanza kwa ofisi hizi mbili kuvutana kuhusu udhaifu katika sheria ya Takukuru, lakini mara zote Serikali imekuwa ikisisitiza kwamba lazima mashtaka kwa watuhumiwa wakubwa wa rushwa wapate yapate kibali cha DPP kabla ya kufikishwa mahakamani. 


Chanzo: Kizitto Noya.

No comments:

Post a Comment